Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi. Awali ya yote na mimi niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Angeline umefanya kazi kubwa sana katika Wizara hii, hongera sana. Mimi nakumbuka ukiwa Naibu Waziri tumefika hadi huko Masasi kwenye vitongoji huko kutatua migogoro, ukiwa na nguvu timamu kabisa kwakweli hongera sana mama yetu. Lakini pia nampoingeza pia Naibu Waziri, kwa muda mfupi tu ame-cope na Wizara hii, hongera sana Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza makatibu na naibu katibu. Pia naipongeza Serikali kwa kufanya uamuzi ule wa kumrejesha Mkurugenzi wa Shirika la Nyumba. Uamuzi ule ni wa manufaa sana kwa nchi yetu. Waswahili wanasema uchungu wa mwana anaujua ni mzazi. Tunajua mkurugenzi yule ndiye aliye lihuisha lile Shirika, kwa hiyo mambo mengi na miradi mingi alikuwa anaifahamu. Kwa hiyo nawapongeza sana nakupongeza Waziri lakini naipongeza Serikali kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niungane na wenzangu pamoja na Bunge hili kwa uzito mkubwa kumpongeza Rais wetu kwa ushindi Mkubwa wa hii Tuzo ambayo ameipokea. Ushindi huu ni mkubwa kwa nchi yetu lakini kwa maendeleo ya Taifa letu. Kwa niaba yangu mimi mwenyewe lakini kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Mbinga Vijijini natoa hongera sana sana sana kwa Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitajikita kwenye maeneo mawili. Eneo la kwanza ni eneo hili la maduhuli ya Serikali. Ninaipongeza Serikali, naona wanafanya jitihada mbalimbali za makusanyo lakini bado tupo nyuma sana kama taarifa ya Waziri inavyosema na hata taarifa ya Kamati imeeleza hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka uliopita tulitarajia kukusanya kwa asilimia 100, lakini kwa bahati mbaya sana tumefikia asilimia 42. Hata hivyo bado mwaka huu nimeona tumejiwekea malengo ya ongeleko la asilimia 11. Mimi hofu yangu tu ni kwamba, ikiwa mwaka jana hatukufikia malengo hata kwa nusu kwanini awamu hii tumejiwekea malengo yanayozidi tena kwa asilimia 11? Ipo mikakati gani, mikakati ipi tumejiwekea ya kwenda kuyafikia haya malengo ya mwaka huu? Kwa hiyo niombe Wizara kwa dhati kabisa, wenzangu wamesema hapa, na mzungumzaji aliyetangulia amesema hapa; sisi kule vijijjni wananchi wetu wapo tayari kumiliki ardhi lakini tunanyimwa fursa hii wananchi wetu hawana hati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa hawana hati tunawanyima fursa nyingine lakini pia sisi Serikali tunajinyima fursa ya kupata haya maduhuli ambayo pengine tungefikia haya malengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe niiombe sana sana sana Serikali, kama tumejiwekea ongezeko hili la asilimia 11 basi tuone na mikakati ya dhati kabisa, kabisa kabisa; na mimi nawaamini, ninamuamini Mheshimiwa Waziri lakini ninamuamini Mheshimiwa Naibu Waziri, uwezo huo mnao, nawaomba sana tufanya mabadiliko. Tumeona kwenye kilimo mambo yanakwenda, tuone pia hapa kwenye ardhi; hili ongezeko hili la asilimia 11 tuweze kulifikia. Na hatuwezi kulifikia kwa kuzungumza tu hapa, tunataka tuone mikakati ya dhati. Hivyo nikuombe Mheshimiwa Waziri utakapokuja kuhitimisha hoja hapa kesho utueleze mikakati inayowezesha kufanikisha mpango huu kwa sababu fursa zipo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni kuhusu migogoro. Ninaiona jitihada ya Serikali ya kutatua hii migogoro ya ardhi, ipo, lakini migogoro hii utatuzi wake unachelewa sana. Tumesikia kuna Tume, kuna Kamati lakini majibu mpaka leo hakuna. Na tutambue ndugu zangu, kucheleweshwa kwa haki hizi tunawachelewesha Watanzania fursa nyingine; tunawachelewesha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na wanasema haki iliyocheleweshwa ni sawa na haki iliyopotea. Kwa hiyo niwaombe sana ndugu zangu, niombe Wizara tufanye juu chini migogoro hii itatuliwe kwa wakati. Nitaomba pia Mheshimiwa Waziri utupe hatua gani utachukua ili kuharakisha utatuzi wa migogoro hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano kwenye jimbo langu pale upo mgogoro tangu miaka iliyopita na mimi nimeukuta. Wamekuja viongozi, upo, mpaka leo hii, katika Kijiji cha Ndika. Ndika hii niliisemea mwaka jana, na naishukuru Wizara, kwa sababu mlikuwa wote na Mheshimiwa Lukuvi, alijaribu kutoa maelekezo yalipunguza migogoro zaidi kwa sababu ilifikia hatua watu walikuwa wanarushiana risasi pale. Risasi zilipigwa na mapanga yalipigwa kwasababu maeneo ya watu ya kulima yamechukuliwa bila hata yakufuata utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi hapa niombe sana mnisaidie mgogoro huu huishe, kwa sababu mpaka ninavyosema sasa hivi wananchi wamejipanga kuacha kupeleka watoto shule wakisema tutapelekaje watoto shule wakiwa wana njaa? Kwa sababu maeneo yao waliyokuwa wanalima siku zote hawalimi tena, ni miaka zaidi ya mitano hawalimi wanakaa tu kusubiri Serikali itatuondolea kero hii, Serikali itatatua mgogoro huu, mgogoro hautatuliki mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana Wizara. Jitihada mwaka jana ilionekana lakini haijafikia mwisho. Kwa hiyo niombe sana Kijiji cha Mkuka, Kijiji cha Mkuani lakini pia kata ya Jirani ya Langilo na kata ya Kipapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi inafika sehemu, kwa sababu watu wa TFS wao ndio wanaoonekana kufanya ulinzi eneo lile, wananchi hata kupita njia wanahofu. Na ni kweli ukipita wanakufanyisha mazoezi ya kichurachura sijui na nini! Kwa kweli niombe Wizara tutatue migogoro hii haraka haraka. Kwa kuchelewesha kutatua migogoro hii, kama nilivyosema pale mwanzo, watu wanakosa fursa ya kimaendeleo kwa sababu hawazalishi. Watu wanakosa chakula, na ndiyo maana sasa wamesema Mheshimiwa Mbunge sisi hatutapeleka watoto wetu shule, hatuwezi kupeleka watoto shule wakiwa na njaa. Miaka mitano hadi sita mgogoro tu wa eneo la wakulima hautatuliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya, amekuja naye muda mfupi pale ameanza kuchukua hatua. Kwa ushirikiano wetu, kwa maana ya Wizara naye pengine tutayafikia haya majibu haraka au kwa wepesi zaidi. Kwa hiyo, nawaomba sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujumuisha hapa, unipe majibu ya namna ambavyo tunaenda kumaliza huu mgogoro. Kwa leo nilikuwa sina mengi, nilitaka nisema haya, nawashukuruni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)