Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyetujalia afya njema sote kuwa hapa. Pia, shukrani za kipekee niwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Rufiji kwa namna ambavyo wameniamini na wakanichagua kwa kishindo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwa mara ya kwanza Jimbo la Rufiji tumeweza kuandika historia kwa sababu katika nchi hii toka tumepata uhuru na toka mfumo wa vyama vingi ulipoanza haijawahi kutokea Rufiji kwa Mheshimiwa Rais kupitia Chama cha Mapinduzi kupata kura nyingi. Kwa hiyo, nawapongeza sana wananchi wote wa Jimbo la Rufuji. Pongezi pia nikupe wewe Mwenyekiti, naamini kwa uzoefu na uwezo ulionao wa kisheria utatusaidia na utaliongoza Bunge hili vizuri kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kwa Mpango huu wa Maendeleo kama ulivyowasilishwa, binafsi nina masikitiko makubwa sana kwa sababu sielewi sisi wananchi wa Jimbo la Rufiji tuna matatizo gani katika nchi hii kwa sababu katika Mipango yote ya Maendeleo Rufiji tumeachwa mbali kabisa. Labda nilikumbushe Bunge lako kwamba Rufiji tumechangia asilimia kubwa ya upatikanaji wa uhuru wa nchi hii, tukizungumzia Pwani lakini na Rufiji kwa ujumla.
Pia Rufiji inabaki kuwa ni miongoni mwa Wilaya pekee ambazo tumeshawahi kuendesha Vikao vya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi lakini sasa ukiangalia Mipango mingi ya Maendeleo imetuweka mbali kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianzia suala zima la kilimo kama lilivyozungumzwa katika ukurasa wa 17, napata tabu kabisa kwa sababu Mpango huu wa Maendeleo hauzungumzii kabisa ni namna gani Rufiji itarudi katika ramani ya kilimo. Sote tunafahamu kwamba Rufiji miaka ya themanini ndiyo Wilaya pekee ambayo ilikuwa na uwezo wa kulisha nchi hii. Tunalo Bonde la Mto Rufiji, bonde hili ni zuri sana na tunaiomba Wizara pamoja na Kamati zinazohusika basi kufikiria ni namna gani wataweza kuliendeleza bonde hili. Pia tunafahamu kuna baadhi ya miradi kwa mfano ule mradi wa RUBADA ambao ulikuja pale Rufiji, naamini kabisa mradi huu ni mradi ambao watu wameutengeneza kwa ajili ya kujipatia pesa na hauna faida yoyote kwa Wanarufiji. Kwa hiyo, naomba kwanza Serikali ikae chini na kufikiria ni namna gani wataweza kupitia kumbukumbu zote walizonazo ili kuangalia ufisadi mkubwa ambao umeshawahi kufanywa katika mradi huu wa RUBADA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Rufiji tunayo ardhi nzuri na ardhi kubwa isiyokuwa na tatizo lolote la migogoro ya ardhi, tunaiomba Serikali sasa kufikiria mpango wa kuanzishwa Chuo cha Kilimo Rufiji ili sasa kiweze kusaidia suala zima la kilimo kwa sababu tunayo ardhi nzuri sana. Pia mchakato wa uanzishwaji wa viwanda vya kusindika mazao, naishauri Serikali uanzie Rufiji kwa sababu tunayo ardhi nzuri yenye rutuba na tunalo bonde zuri. Niseme tu katika nchi hii hakuna ardhi iliyo nzuri kama ya Jimbo letu la Rufiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija katika suala zima la viwanda, kumbukumbu zangu zinanionesha kwamba Mheshimiwa Rais pamoja na Makamu wake tarehe 9 Septemba, Makamu wa Rais alituahidi mchakato wa ujenzi wa viwanda Rufiji. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali katika Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa hivi viwanda ambavyo vitajengwa kuanzia Rufiji kwa sababu kila aina ya kilimo sisi tunacho na tunaishauri Serikali sasa mchakato huu uanze haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye tatizo la maji. Ukurasa wa 46 wa Mapendekezo ya Mpango huu wa Maendeleo umezungumzia suala la maji. Sisi wananchi wa Jimbo la Rufiji pamoja na Majimbo ambayo tunakaribiana, nazungumzia Kisarawe, Mkuranga, Kibiti pamoja na Rufiji yenyewe, tuna shida kubwa sana ya maji. Labda niseme katika Jimbo langu ya Rufiji ni 5% au 6% tu ya wananchi ndiyo wanaopata maji safi na salama. Katika eneo dogo la Tarafa ya Ikwiriri ambayo ndiyo walikuwa wakipata maji safi mota imeharibika huu ni mwezi wa tatu. Mchakato wa tathmini ya utengenezwaji wa mota upo katika Wizara hii ya Maji, huu ni mwezi wa tatu hatujui Katibu Mkuu wa Wizara hii anafanya mchakato gani ili kuweza kuharakisha mota hii kuweza kutengenezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyoweza kuona maeneo mengine, Ziwa Viktoria wana uwezo wa kutoa maji sehemu moja na kupeleka sehemu nyingine katika Mikoa mbalimbali na sisi tunaishauri Serikali sasa Mpango huu wa Maendeleo kufikiria mchakato wa kuboresha huduma ya maji kwa kutoa maji katika Mto wetu wa Rufiji na kusambaza katika Wilaya zetu zote ambazo zinazunguka katika Jimbo la Rufiji, hii itasaidia sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo, kwa mfano kule Ngarambe kuna tatizo kubwa sana la maji. Akinamama pamoja na watoto wanawajibika kuamka alfajiri kwenda kuchota maji na wengine hawarudi majumbani, wanachukuliwa na tembo, wanauwawa na maeneo mengine wanachukuliwa na mamba! Kwa hiyo, shida ya maji katika Jimbo la Rufiji ni kubwa sana. Tunaomba Mpango huu wa Maendeleo kulifikiria suala hili la maji kwa kuliboresha vizuri kwa kutumia Mto wetu wa Rufiji katika kuliweka sawa.
Mhershimiwa Mwenyekiti, nikija katika suala zima la afya, mimi nina masikitiko tena makubwa. Niseme tu kwamba tunayo Hospitali yetu ya Wilaya pale iliyojengwa mwaka 60 lakini toka mwaka 60 hakuna ukarabati wowote ambao umeshawahi kufanywa. Mimi mwenyewe nilishaanza mapambano kuweza kuhakikisha kwamba tunapata wawekezaji kutusaidia. Sasa tunaiomba Serikali kuharakisha huu Mpango wa PPP ili wawekezaji wa kutoka Uturuki waweze kutusaidia kujenga hospitali ya kisasa kabisa ambayo itakuwa na European Standard yenye mashine zote za kisasa. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali kuharakisha Mpango huu wa PPP.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tukija suala zima la elimu, niharakishe kidogo kwa sababu ya muda, niseme tu kwamba sisi wananchi wa Jimbo la Rufiji tuko nyuma sana kwenye suala zima la elimu, hata Serikali imetuacha yaani tumekuwa kama watoto wa kambo, hatujui sisi tuna matatizo gani? Suala la elimu ni shida kubwa hasa ukizingatia Rufiji ni kubwa kuliko hata Mkoa wa Kilimanjaro lakini tuna shule moja tu ya sekondari ya kidato cha tano na cha sita kwa hiyo, hili ni tatizo kubwa. Tunaiomba Serikali kufikiria mchakato wa kuboresha elimu katika Jimbo letu la Rufiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo, kwa mfano kule Mtanange na maeneo mengine watoto hawasomi kabisa kutokana na umbali wa shule za msingi ambapo mtoto inabidi asafiri umbali wa zaidi ya saa tano, saa sita kwenda kufuata shule. Hali hii imewafanya wazazi wengi kushindwa kuwapeleka watoto wao shule. Kwa hiyo, naona kabisa kwamba mchakato huu wa elimu bure sisi wa Rufiji tutaachwa kando kabisa kwa sababu wazazi watashindwa kuwapeleka watoto wao shule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija suala zima la mchakato wa benki, mimi niseme Rufiji ni Wilaya ya sita wakati wa mkoloni na ni Wilaya ya 21 wakati tunapata uhuru lakini utashangaa Wilaya hii ya Rufiji kwa namna ambavyo Serikali imeamua kuiacha hatuna hata benki kabisa. Tunawajibika kusafiri umbali wa zaidi ya kilometa 120, kwa wale wananchi wanaotoka kule maeneo ya Mwaseni na Mloka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaishauri Serikali huu mchakato wa uanzishwaji wa Benki za Ardhi, kama ulivyoainishwa katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi, ukurasa wa 35, tunaiomba Serikali sasa kufikiria benki hizi waanze kujenga katika Jimbo letu la Rufiji kwa sababu tunayo ardhi ya kutosha, hatuna migogoro ya ardhi, ardhi ni bure kabisa tunawakaribisha lakini tunaiomba Serikali pia kuona namna gani ya kuwekeza kwenye suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija katika suala zima la miundombinu, nina masikitiko haya mengine kwamba Rufiji japokuwa ni Wilaya ya zamani lakini tunabaki kuwa ni Wilaya pekee ambayo hatuna hata nusu kilometa ya lami. Kama tulivyoona Mapendekezo haya, hakuna hata sehemu moja ambayo inazungumzia Rufiji tutasaidiwa vipi kuboresha miundombinu yetu. Mama yetu Makamu wa Rais pamoja na Rais mwenyewe alituahidi kwamba tutajengewa lami barabara ya kutoka Nyamwage - Utete, ili iweze kusaidia kupunguza vifo vya akina mama ambao inabidi wakimbie Utete kwa ajili ya kwenda kujifungua. Pia barabara ya kutoka Ikwiriri – Mwaseni - Mloka yenye kilometa 90, tunaiomba Serikali kuharakisha mchakato wa ujenzi wa barabara hii na barabara nyingine kutoka Mwaseni - Mloka - Kisaki pamoja na kutoka Mwaseni - Mloka - Kisarawe. Barabara hizi iwapo zitajengwa zitasaidia kufungua biashara na wananchi wa Jimbo langu la Rufiji wataweza kufanikiwa katika mambo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunaishauri Serikali na tunaiomba iharakishe mchakato wa ujenzi wa Chuo cha Utumishi pale Ikwiriri. Tulishatoa ardhi kubwa lakini mpaka leo hii Wizara husika haijachukua hatua zozote za mchakato wa ujenzi wa Chuo hiki cha Utumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaishauri Serikali kuachana kabisa na mchakato huu wa mambo ya retention. Suala hili litatuletea shida kubwa na tunaiomba Serikali kuepukana nalo, kuacha kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuishauri Serikali kuanzisha community centre. Community centre hizi zitaweza kusaidia wananchi wetu kwa maeneo mbalimbali ya vijiji ili waweze kujifunza mambo mbalimbali kwa ajili ya kunyanyua uchumi wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naomba maombi yangu haya yote kama nilivyozungumza yaweze kuchukuliwa na kufanyiwa kazi. Vinginevyo kama Serikali haitachukua basi sitaunga mkono kabisa mapendekezo mwezi Machi yatakapoletwa hapa Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana. (Makofi)