Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi. Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa tuzo muhimu ambayo ameweza kuipata ambayo inaendelea kuitangaza nchi yetu na kuendelea kuboresha mambo mbalimbali katika nchi yetu, pili napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Ardhi pamoja Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nijikite kwenye Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi. Mwaka 2006 katika Mkoa wetu wa Lindi Serikali iliridhia kuingiza mifugo kutoka katika Bonde la Ihefu, hii ilisababisha mifugo mingi kuhamishiwa katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Lindi. Katika Wilaya ya Kilwa peke yake kati ya mwaka 2006 hadi 2007 mifugo isiyopungua Laki Moja iliingia katika Wilaya ya Kilwa. Pia hii ilisababisha sasa Serikali Kuu kupitia Wizara ya Ardhi pamoja na Halmashauri yetu ya Wilaya ya Kilwa pamoja na Taasisi ya BTC (Belgium Technical Cooperation) kuweza kushirikiana kwa pamoja kuweza kupima na kuweza kuboresha matumizi ya ardhi iliyopo katika Wilaya yetu ya Kilwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ardhi iliweza kupimwa jumla ya hekta 337,500 kwa ajili ya kulisha ng’ombe wapatao 168,750, lakini kwa vipindi tofauti kati ya mwaka 2007 hadi sasa takribani miaka 15 iliyopita, mifugo mingi imeendelea kuingia katika Wilaya ya Kilwa pamoja na Mkoa wa Lindi kwa ujumla. Wilaya ya Kilwa peke yake mifugo inayokadiriwa kufikia 350,000 imeingia, vilevile wale waliokuwepo tangu mwaka 2006 wameendelea kuzaana na mifugo mingi imeingia kwa kupitia njia za holela, mingine imepita kupitia Pori la Akiba la Selous, mingine imeingia kutokea Mkoa wa Pwani, kwa hiyo, sasa hivi kuna takribani ng’ombe, ng’ombe peke yake wanakaribia 500,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, imesababisha hali kuwa ngumu sana ya maisha ya wakulima wetu, pia wafugaji wenyewe kwa sababu, mpango wa matumizi bora ya ardhi umeshapitwa na wakati kwa sababu una zaidi ya miaka 15 tangu ulipofanyika. Na kwa mujibu wa utaratibu mpango wa matumizi bora ya ardhi unatakiwa uwe reviewed angalao kila baada ya miaka 10, kazi ambayo haijafanyika na hiyo imesababisha kuwepo na changamoto kubwa, mapigano ya mara kwa mara, lakini mifugo kuweza kutangatanga hovyo katika Wilaya nzima ya Kilwa na Wilaya zote za Mkoa wa Lindi. Kwa hiyo, sasa hivi tuna hali ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda utambue ndani ya miezi 12 iliyopita wananchi wanne walipoteza maisha, wawili katika Kijiji cha Nanjilinji, mmoja katika Kijiji cha Nakiu, pia katika Kijiji cha Kipindimbi kuna mwananchi mmoja alipoteza maisha kwa hiyo, jumla ni wananchi wanne walipoteza maisha ndani ya miezi 12 iliyopita, lakini pia kumekuwa na vurugu za hapa na pale nyingi. Kwa mfano, Tarehe 07 mwezi Aprili mwaka huu katika Kijiji cha Ngarambi, WEO wa Kijiji kile, Afisa Mtendaji Kata, alivamiwa na kundi la wafugaji lakini bahati nzuri alikimbia na badaye alijisalimisha katika Kituo cha Polisi kule Somanga, lakini na wale wafugaji walichachamaa baada ya kuwa mifugo yao ambayo iliingia kiholela katika Wilaya ya Kilwa ilipokuwa imekamatwa, baAdae walimvamia Askari wa mgambo ambaye alikuwa analinda ile mifugo na kumjeruhi, matukio ya namna hii yamekuwa mengi mno kiasi kwamba, yanawakatisha tamaa wakulima wetu, lakini yanawafanya hata wale wafugaji wasiweze kufuga ng’ombe wao na mifugo yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali katika hili ijitahidi kuweza kuona sasa katika zile fedha kidogo zilizotengwa kwa ajili ya maboresho au Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi waweze kutumia hizo fedha, vilevile zije Kilwa tuweze kuona namna ambavyo tunatatua ile migogoro. Nina imani kama mpango wa matumizi bora utafanyika katika Wilaya ya Kilwa ambao katika kipindi kilichopita ule mwaka 2006/2007 ulifanyika katika vijiji 35 tu wakati Kilwa tuna vijiji 90, ni imani yangu kwamba, tutapunguza kwa kiasi fulani hii migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uzoefu na kazi ambazo zimefanywa za maboresho ya mpango wa matumizi bora ya ardhi kule Kilombero. Kulikuwa na mradi mmoja unaitwa Land Tenure Support Program, umesaidia sana katika Bonde la Kilombero hasa Wilaya za Malinyi, Ulanga pamoja na Mlimba. Kwa hiyo, ni imani yangu kwamba, tukitekeleza vizuri ule mradi basi haya mambo ya mauaji, haya mambo ya watu kujeruhiwa basi yatapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli niseme ningependa kwa kuanzia Kata ambazo zinaongoza ziko 12 ambazo ni Kata ya Somanga, Kata ya Mingumbi, Kinjumbi, Kipatimu, Kandawale, Mitole, Njinjo, Miguruwe, Nanjilinji, Kikole, Likawage pamoja na Kiranjeranje, ikikupendeza kupitia Wizara ya Ardhi basi tuanze na maeneo hayo ambayo yamekithiri kwa migogoro kila kukicha. Nashukuru Mheshimiwa Waziri wakati tunatekeleza ule mradi wa Land Tenure Support Program kule Bonde la Kilombero wakati ule ulikuwa Naibu Waziri na mara kadhaa ulikuja katika Bonde la Kilombero kuhakikisha ule mradi unatekelezwa kwa ufanisi. Na kwa kuwa, ulitekelezwa kwa ufanisi, ulitatua changamoto nyingi sana ambazo zilikuwa zinawakabili wananchi wa maeneo yale ya Malinyi, Ulanga, Mlimba pamoja na Kilombero yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niseme nikuombe Mheshimiwa Waziri basi na sisi utufanyie kama vile ambavyo experience inaonesha kule tuliweza kutatua ile migogoro ya wakulima na wafugaji, kwa sababu ule mradi kupitia wataalam wetu wabobezi, kulikuwa na Dada mmoja anaitwa Siyabumi Mwaipopo, sasa hivi sijui yuko Mbeya, sijui yuko wapi, walifanya kazi nzuri sana. Kwa kweli, nawapa hongera kwa kazi ambayo ilifanyika kule, Kilwa basi tunaomba Mheshimiwa Waziri utuletee ule mradi, hata kama siyo ule, lakini angalao ulete fedha basi ili baadae ule mradi utafanyika kwa mfumo ule wa revolving, kwa maana tutapata hela kupitia zile hati za kimila pamoja na kazi ambayo itafanyika watu watalipia kidogokidogo na mwisho wa siku tutajikuta vijiji vyote 90 tuweze kuvikamilisha kuvipima, lakini vilevile kuweza kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi na pia kupima mipaka kati ya vijiji hadi vijiji ambayo iko mingi tu sasa hivi katika Wilaya ya Kilwa. Siyo katika Wilaya ya Kilwa tu hadi Kilwa na Wilaya za majirani kama Liwale na Rufiji kwa kweli hali siyo nzuri kuna migogoro ya hapa na pale kati ya vijiji vya Wilaya moja kwenda Wilaya nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni imani yangu kwamba, kwa kupitia utaratibu huu wananchi watapata hati za kimila, lakini vilevile watadumisha usalama na amani katika maeneo yao. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri utusaidie katika hilo ili tuondoe hii hali ambayo inaendelea kukua ya mapigano ya mara kwa mara, watu wanajeruhiwa, wanakufa na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri kuna suala la migogoro kati ya vijiji vyetu vya Wilaya ya Kilwa pamoja na Hifadhi ya Pori la Akiba la Selous. Kuna vijiji vinne katika Jimbo langu peke yake, kuna Kijiji cha Nakingombe, kuna Kijiji cha Ntepela, kuna Kijiji cha Zinga, kuna Kijiji cha Nakingombe, hivi vijiji vinne vinapakana na Hifadhi ya Taifa ya Pori la Akiba la Selous kwa hiyo, niombe Mheshimiwa, tuliliongea hili wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja mwezi Oktoba mwaka jana kwa uchungu na masikitiko makubwa sana. Kulikuwa na mgogoro mkubwa sana kati ya TAWA na wananchi wa hivyo vijiji, bahati nzuri ilikuja Tume ya uchunguzi, ingawa majibu hatujayapata mpaka leo na sasa ni ktakribani miezi Sita inakaribia tangu ile Tume ilipokuja kuchunguza ule mogogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba majibu tupate mapema ili wananchi watulie waendelee kufanya shughuli zao za kiuchumi katika hayo maeneo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndulane, muda wetu umemalizika wa siku ya leo.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)