Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Ardhi. Nami niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kupewa tuzo, maana yake mchango wake umetambulika duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Mama yangu Mheshimiwa Angeline Mabula na Naibu wake Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete na niwaambie kwamba wananchi wa Ludewa wanawashukuru sana kwa kuwapa fedha kwa ajili ya kurasimisha makazi kiasi cha shilingi milioni 400 na zaidi ambazo zimetumika pale Mlangali wameshapima zaidi ya viwanja 3,000. Halikadhalika Makao Makuu ya Wilaya Ludewa kazi ya upimaji inaendelea. Kijiji cha Amani wananchi wanawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa baadhi ya maeneo wanamashaka na kwamba tunavyopeleka mipango miji watu wa TANESCO wanadhani wanataka kuwaongezea bei ya umeme yaani maeneo yale ambayo yamepangwa kuwa planning areas watu wa TANESCO wana-charge gharama kubwa za umeme. Lakini tunaendelea kuwaelimisha na wanawaalika sana kwenda kuwatembelea na wanawaomba mshirikiane na Waziri wa TAMISEMI kuhakikisha watu wa TARURA wanasaidia kufungua zile barabara ili Mji wa Mlangali uweze kuwa wa kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Amani ambao wanasubiri sana uwekezaji mkubwa wa Liganga napo paweze kuwa na mji wa kisasa kwamba tusiishie tu kurasimisha, wanaomba tuwasaidie kuhakikisha kwamba barabara zinafunguliwa vizuri ili miji iweze kuwa na mvuto wa kisasa na vilevile wanaomba sana taasisi mbalimbali za kifedha ambazo zinawezesha wananchi kwenda kutoa mikopo kama TADB na CRDB waweze kwenda kuwakopesha pembejeo za kilimo. Kwa sababu sasa Wizara ya Ardhi imeongeza thamani ya ardhi yao kuhakikisha kwamba wanapata hati. Kwa hiyo, hongera sana Mheshimiwa Waziri, wananchi umewatengenezea furaha pale Ludewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika Mheshimiwa Waziri wananchi wa Ludewa wanaomba sana pale Makao Makuu ya Wilaya kulikuwa na eneo la kituo cha mabasi na kulikuwa na soko, kulikuwa na vibanda vimegawanywa kwa wananchi waweze kujenga na kufanyia biashara, ni kama uwezeshaji wa kuchumi kwa wananchi. Sasa bahati mbaya kumetokea hali ya kutoelewana kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa na wananchi wale wafanyabiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wanaomba sana umtume Kamishna wako wa Ardhi aweze kwenda pale na ikiwezekana utolewe muongozo ambao utaonesha haki na wajibu wa kila upande katika kumiliki viwanja hivi vya maeneo ya stand na soko, vibanda vya biashara, kwamba ukitolewa mwongozo utaepusha migogoro, wananchi kupelekana mahakamani na Serikali kwa sababu wananchi ni mali ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze pia kwa bajeti hii nimeweza kuipitia vizuri. Nimeona mikakati ya Wizara ya Ardhi ni mizuri sana, mipango yao imekaa vizuri ila sasa uwezeshwaji, Serikali inapaswa kuunga mkono sana Wizara hii tuweze kuwaongezea bajeti kwa ajili ya kuweza kupima nchi hii. Kwa uzoefu nilionao, mimi naamini kama Wizara ya Ardhi itawezeshwa kwa fedha na vifaa kuweza kupima nchi hii kama mipango yao ilivyo, tutapunguza migogoro ya ardhi kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kama ardhi inakuwa imepimwa, mwananchi amelindwa kwa kupewa hati miliki, ni nani atakuja pale kwenda kuvamia eneo la mwananchi? Kwa sababu itakuwa hata rahisi kutatua migogoro ya ardhi. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba sana Serikali iweze kuwaongezea fedha Wizara hii ili waweze kufikia malengo ya kupanga, kupima nchi hii ili kuweza kuepusha migogoro, lakini vilevile kuwawezesha wananchi kiuchumi. Wananchi wanakuwa na dhamana ambayo inawatambua, inawafanya watambulike kwenye taasisi mbalimbali za fedha nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile nimepitia hotuba ya bajeti hii ukurasa wa 174, nimebaini Wizara hii ina upungufu mkubwa sana wa watumishi. Naomba nitoe mfano hapa, kwa upande wa Maafisa Ardhi mahitaji ni Maafisa 1,206 waliopo ni 605, upungufu ni watumishi 601, kwa hiyo, waliopo ni asilimia 50.2 ya mahitaji. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iweze kutoa vibali vya ajira ili maafisa hawa, kwa sababu mitaani wamo. Chuo cha Ardhi - Tabora kinazalisha wale Maafisa Ardhi Wasaidizi wazuri, Chuo cha Ardhi Morogoro na Chuo cha Ardhi Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba vibali viweze kutolewa kwa sababu hata hawa Wapima ambao tunatarajia hizi fedha tunazopeleka wao ndio watakaoenda kufanya kazi. Mahitaji ni Wapima 1,978; Wapima waliopo ni 618, upungufu ni 1,360. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kuangalia jambo hili kama tatizo ili iweze kuajiri wataalam. Hata halikadhalika wa Mipango Miji naona nao mahitaji ni 1,036, waliopo ni 330, upungufu ni 706, waliopo ni asilimia 22 ya mahitaji yote. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iweze kutoa vibali ili tumuongezee nguvu Mheshimiwa Waziri na Naibu wake Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete waweze kutimiza malengo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika kule Tume ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi; nashukuru naona na Ludewa wameikumbuka tunaweza kupata hapo vijiji vichache. Naomba sana nao waweze kuongezewa fedha ili waweze kupanga mipango ya matumizi bora ya ardhi ili kuepusha muingiliano wa watumiaji mbalimbali wa ardhi. Hii itasaidia sana kuepusha migogoro ya ardhi na niwapongeze kwa kuanzisha ofisi za Kanda. Naomba wazisimamie vizuri ili ziweze kupanga na kupima vijiji, ile mipango kina ya vijiji iweze kuandaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba sana Wizara hii ya Ardhi iweze kushirikiana na watu wa TRA, ile kodi ya majengo uaami ule utaratibu tuliouweka mwaka jana kwamba tuta-charge kupitia LUKU, mita zile za umeme. Pale nafikiri hela nyingi bado hazikusanywi, kwa hiyo, naomba tuweze kutumia wataalam wetu kuhakikisha mapato yale tunaweza kuyapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)