Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angeline Mabula na Naibu Waziri Ndugu Ridhiwani Kikwete pamoja na wataalamu wa Wizara kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitachangia kuhusu migogoro ya umiliki ardhi katika Jimbo langu la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jimbo langu la Moshi Vijijini kuna migogoro ya umiliki wa ardhi baina ya wakulima na wafugaji katika Kata za Mabogini (Kijiji cha Mserekie) na Arusha Chini (Mikocheni na Chemchem) zilizoko maeneo ya tambarare.

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro hii imeshasababisha madhara makubwa ikiwemo vifo na uharibifu mkubwa wa mali kama mazao ya wakulima. Mpaka sasa Serikali ya Wilaya na Mkoa haijaweza kupambana na changamoto hii, kwani tatizo hili linajirudia mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro ya wakulima na wafugaji jimboni kwangu inasababishwa na uhaba unaoendelea kukua wa rasilimali ardhi. Kutokana na hali hii, wakulima wamekuwa wanafungua mashamba kwenye maeneo ya wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro hii kwa kiasi kikubwa husababishwa na yafuatayo; kwanza Serikali haijayapima maeneo ya wafugaji na wakulima na kuyamilikisha kwa wahusika kwa kutoa hati za kimila na za Serikali.

Pili, kubadilika kwa tabia nchi kunakopelekea malisho kukauka na kusababisha uhaba wa chakula cha mifugo na kuwafanya wafugaji kulisha mifugo yao kwenye mashamba ya wakulima; na tatu, kupanuka kwa shughuli za kilimo na makazi ya watu ambapo maeneo ya ufugaji yamepungua.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto hii ninaishauri Serikali kama ifuatavyo; kutokana na migogoro inayoendelea, kuna umuhimu wa Serikali kuingilia jambo hili na kuhakikisha kuwa maeneo husika yamepimwa na kumilikishwa rasmi kwa wahusika. Pia Serikali iharakishe zoezi hili kwa kutumia mifumo ya hati za kimila zinazotambuliwa kisheria na baadaye wapewe hati za Serikali za kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na mazingira ya Kitanzania, ninaishauri Serikali ipitie sera za umiliki wa ardhi zenye utata zinazoweza kuchochea migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji. Sera nzuri na rafiki itasaidia kutoa haki bila malalamiko.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali, Wizara za sekta husika (Ardhi, Kilimo na Mifugo na Uvuvi) zishiriki kikamilifu kwenye zoezi hili na kila Wizara itenge bajeti ya kusaidia kupima ardhi na kushughulikia changamoto hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.