Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendelo endelevu na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa kuanzisha mikopo inayotolewa kwa ajili ya kupanga, kupima na kumiikisha (KKK) ardhi. Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ni mnufaika wa programu hii na imekopeshwa shilingi 1,857,586,634. Mji Mdogo wa Mbalizi kumepimwa viwanja 35,000 kwa gharama ya shilingi 1,273,038,500 na Kijiji cha Mwashoma Kitongoji cha Inolo vimepimwa viwanja 565 kwa gharama ya shilingi 584,548,134 na umefanyika kwa ufanisi mkubwa sana. Kutokana mahitaji makubwa na faida itayopatikana kwenye mauzo ya viwanja hivi, ipangiwe matumizi yanayolenga kuendeleza ardhi ikiwemo kuweka miundombinu kwenye maeneo yanayopimwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mafanikio katika utekelezaji huu wa mwanzo, napendekeza Serikali iweke kipaumbele cha kuendeleza programu katika maeneo mengine hususani yanayolizunguka Jiji la Mbeya kutokana na mahitaji makubwa ya makazi yaliopimwa. Napendekeza Serikali iendeleze programu hii katika vijiji vya Swaya, Lupeta, Nsenga, Ifiga, Nsongwi Mantanji, Nsongwi Juu, Izumbwe, Iwindi, Igoma, Ilembo, Idimi na Haporoto. Upimaji kwenye vijiji unaharakisha kuwa miji (growing towns) utawezesha kupunguza na hata kuondoa kabisa makazi holela na pia kuongeza wigo wa walipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na programu ya makazi, Serikali iweke usimamizi wa matumizi bora ya ardhi ya kilimo ambayo inaendelea kupotea kwa matumizi ya makazi. Katika kupangilia matumizi mazuri ya ardhi, ihusishe Wizara za Kilimo, Wizara za Maji na Wizara inayosimamia mazingira. Kwa vile binadamu tunaongezeka ni muhimu kuhakikisha ulinzi kwa kuhifadhi ardhi inayofaa kwa kilimo na pia kutenga ardhi kwa ajili ya wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hatua zinazochukuliwa na Serikali kurejesha mahusiano mazuri kati ya TANAPA (Hifadhi ya Kitulo) na wananchi wa Kata za Ilungu, Igoma, Ulenje na Inyala, bado suluhu haijapatikana. Kuna mgogoro wa miaka mingi wa mpaka kati ya TFS na wananchi wa Kijiji cha Mwashoma. Pia kuna mgogoro wa TANAPA (Hifadhi ya Kitulo) na wananchi wa Kijiji cha Kikondo ambao eneo lao lilichukuliwa na TANAPA bila kulipa fidia. Pamoja na changamoto hiyo ya GN za Hifadhi ya Kitulo, pia kuna utata wa mpaka wa Wilaya ya Mbeya na Wilaya ya Makete na inahitajika Wizara ya Ardhi kupitia upya mipaka na kurekebisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mgogoro huu kuchukua muda mrefu na kusabisha uvunjifu wa amani, kuna ahadi ya mwaka 2015 alitoa Mheshimiwa Hayati Magufuli na kumwelekeza Waziri wa Ardhi wa wakati huo kupitia upya mipaka, ili wananchi wa Kijiji cha Kikondo waachiwe eneo leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.