Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nami niungane na Wajumbe wote au Wabunge wote kumpa salamu za pongezi sana Mheshimiwa Rais wetu Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan mama maendeleo kwa zawadi kubwa au heshima kubwa ambayo imeendelea kutupa nchi kuhakikisha kwamba nchi ya Tanzania imeweza kufahamika katika usimamizi wa miradi lakini pia kwakipekee kabisa juu ya usimamizi wa fedha za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo pia nichukue nafasi hii kuwashukuru sana na kuwapongeza sana Wabunge wote waliochangia katika hoja ambayo imeletwa na Mheshimiwa Waziri wetu wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambayo kwa jumla au kwa rekodi tulizonazo waliochangia kwa mdomo walikuwa watu 27 na waliochangia kwa maandishi ni watu wawili. Binafsi yangu kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri niwashukuru sana Wajumbe wote kwa michango yao mizuri, lakini kabla sijaanza kujibu hoja ambazo zimeelezwa nataka nikuhakikishie na Bunge lako kwamba mawazo yote yaliyotolewa, ushauri wote sisi kama Wizara tunaichukua na tutakwenda kuyafanyia kazi ili kuhakikisha kwamba ardhi yetu au rasilimali ardhi yetu inakuwa salama na wananchi wetu wanaendelea kufaidi matunda ya kuwepo kwa Rais Samia Suluhu Hassan katika nchi hii ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutoa majibu haya nitajaribu kujibu kwa jumla. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wajumbe sitatumia nafasi hii kutaja majina ya mmoja mmoja, lakini nadhani katika maelezo moja kati yenu mtakuwa mnajua kwamba hili jambo niliuliza na linatolewa majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika eneo la migogoro ya ardhi; nataka nitoe taarifa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri kwamba Serikali imekuwa inafanya hatua nyingi sana za kuhakikisha kwamba migogoro ya wakulima na wafugaji, migogoro baina ya vijiji vyetu, lakini migogoro juu ya matumizi ya ardhi yameendelea kushughulikiwa na katika kufanya hivyo Kamati ya Mawaziri Wanane imeendelea kufanyakazi kama ambavyo imeelezwa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo pia yamefanyika mabadiliko ya sheria, lakini yapo maelekezo yaliyotolewa na Mheshimiwa Rais juu ya jinsi gani migogoro hii inakwenda kutatuliwa ili kwa wananchi amani na utulivu vipate kurudi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo tumeendelea kufanya ziara za mara kwa mara; na katika kufanya hivyo migogoro mingi imetatuliwa lakini kwa kipekee kabisa nataka niwahakikishie ndugu wajumbe au Wabunge kwamba migogoro ile ambayo imetajwa katika mjadala wetu kwa mfano ule wa Efatha kule Rukwa, nataka nikuhakikishieni Waheshimiwa Wabunge kwamba kilio chenu, sauti yenu imesikika si tu ndani ya Bunge lakini hata kwa wananchi wetu katika eneo la Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ya Wizara yalishatolewa juu ya jinsi gani tunaweza tukautatua mgogoro ule lakini pia hatua za kimsingi juu ya utatuzi zilishafanyika lakini tunatambua kama Wizara kwamba zipo kesi ambazo zilifanyika lakini maamuzi yaliyofanyika ya mwisho ya mwaka 2018 ya kugawa maeneo kwaajili ya wananchi haya yanataka twende tukayasimamie ili yaweze kutatua mgogoro huo. Lakini pamoja na hilo nataka niwahakikishieni ndugu wajumbe mliotoa sauti yenu kwamba sisi kama Wizara tutafika baada ya Bunge hili na kubwa zaidi ni kuja kutatua kero hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia limezungumza jambo la Mbarali, nalo pia nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mtenga lakini pia dada yangu Mheshimiwa Bahati kwamba nalo tunalitambua Kamati ya Mawaziri imefika nako tutakwenda ili kwenda kukutana na wananchi tuzungumze ili tujue tunatatuaje si hilo tu pamoja na migogoro mingine yote katika eneo la nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu Wabunge nawashukuruni sana kwa mawazo wenu mazuri juu ya jinsi gani hii Wizara inaweza kuongeza makusanyo ya maduhuli, lakini pia nataka nikuhakikishieni kwamba zipo hatua za msingi ambazo Wizara imekuwa inazichukua kuhakikisha kwamba maduhuli yanakusanywa. Kwa mfano, katika hatua ambazo zimefanyika katika mwaka huu wa fedha ni pamoja na kuendelea na kazi ya kupanga na kupima kwa sababu utakapopanga na kupima maana yake tunakwenda kuzalisha hati ambazo hati zile zinaenda kututolea pesa na makusanyo yanakwenda kuhakikishiwa, lakini pamoja na hilo pia sasa tupo katika utaratibu wa kubadilisha mfumo wetu wa kidijitali ameeleza ndugu Kunambi jana juu ya umuhimu wa kuhakikisha kwamba ule mfumo ILMIS unatandazwa Tanzania nzima na ule mfumo utakapokuwa umetandazwa Tanzania nzima ndiyo tutakwenda kujihakikishia makusanyo yenye uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hilo tu pia ipo mifumo mbalimbali ambayo tunajaribu kui-harmonize pia ikiwa na mifumo mingine ya ukusanyaji wa maduhuli ikiwemo ya TRA, lakini pia kuangalia kama ipo mifumo mingine rafiki ambayo inaweza ikatusaidia katika kuhakikisha kwamba makusanyo yanahakikishiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo pia nataka kukuhakikishia kwamba tunaendelea kutoa elimu, si tu kwa wataalamu wetu lakini pia kwa wananchi kuelewa umuhimu wa kuwa na hati ili hati hizo zitakapokuwa zinalipiwa basi Serikali yao iendelee kukusanya maduhuli na kufikia malengo makubwa kama ambavyo tumesema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo kupitia wahisani mbalimbali fedha zimeendelea kukusanywa, lakini pia kupitia programu mbalimbali kwa mfano sasa hivi katika kipindi hiki cha Sensa ya Makazi tumeendelea pia kupima na kutambua nyumba zetu ikiwa ni moja ya hatua ya kuhakikisha kwamba tunazimbua nyumba hizo na ili tuweze kukusanya maduhuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwashukuru ndugu wajumbe au ndugu Wabunge kwa mawazo yao mazuri na msukumo walionao kuhakikisha kwamba tuna-harmonize mipaka baina ya nchi yetu na nchi marafiki. Lakini nataka nikuhakikishieni pamoja na mawazo mazuri ipo miongozo toka Umoja wa Mataifa Afrika kwamba mpaka tunafika mwaka 2027 mipaka baina ya nchi zote zinazozungukana iwe imeweka vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuhakikishie na Bunge lako kwamba Serikali yako chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan tunaendelea kufanyakazi kubwa ya kuhakikisha kwamba mipaka yetu inaendelea kuwa salama, lakini timu yetu ya watalaamu inaendelea kufanyakazi na watalaamu wa nchi marafiki au nchi majirani ili kuhakikisha kwamba mambo yote yanakaa vizuri na hivi karibuni ndugu Wabunge mnaweza mkawa mashahidi ujumbe wa watalaamu toka Kenya na Tanzania ulikutana kwa ajili ya kukuhakisha kwamba haya matatizo au changamoto zinazotokea katika eneo la mpaka wetu ikiwemo kule Jasini kama alivyozungumza Mheshimiwa Mbunge nalo pia ni moja ya jambo ambalo tunaenda kulitatua. Nataka kuhakikishieni kwamba Serikali imetoa maelekezo na sisi ndani ya Wizara maelekezo hayo tumeendelea kuyasimamia na wataalamu wetu wapo site kuhakikisha kwamba jambo hili linatatulika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi wamezungumzia juu ya tatizo ambalo Wabunge wanalipata juu ya usalama wa mazingira yetu haya tunayofanyia kazi hasa ukizingatia eneo la Bunge ni dogo, lakini pia usalama wa maisha yetu hasa tunapovuka barabara na matumizi ya vyombo vyetu tunapotoka Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kwamba jambo hili linakaa vizuri Ofisi yako ya Bunge iliandikia Ofisi yetu na mbele ya Bunge hili nikiri kwamba Wizara yetu imepokea barua yenu na kuifanyia kazi na hapo ninapozungumza katika viwanja 13 ambavyo vinaonekana vilivyo pembeni ya eneo la Bunge viwanja 11 vimekwishafanyiwa tathimini na value yake imekwishajulikana, lakini pia tutakapokuwa tumemaliza viwili vilivyobakia tutaleta ile taarifa kwa mamlaka husika ambaye ni Katibu wa Bunge ili sasa mchakato uweze kufanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, angalizo; katika sheria yetu Sura Namba 118 ya Utwaaji wa Ardhi na Sura Namba 113 ya Ardhi inatuelekeza kwamba unapotaka kutoa ardhi mamlaka husika lazima ihusishwe; hivyo, nataka nitoe angalizo kwetu kwamba pamoja na kwamba utaratibu unaendelea, lakini mamlaka husika ambayo kwa mujibu wa sheria na Mheshimiwa Rais basi naye lazima tumuhusishe katika jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nirejee angalizo alilolitoa au rai iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri wakati anatoa hotuba yake juu ya kuhakikisha kwamba riba au hizo interest za maeneo au hela zinazotakiwa zilipiwe katika utoaji wa maeneo zinafanyika mapema ili kuepusha usumbufu wa kulipiana fidia na riba zingine zisizofaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nizungumzie jambo la Mabaraza ya Ardhi; nikurejeshe katika Mabadiliko Madogo ya Sheria Sura Namba 216 yaliyofanywa katika Sheria Ndogo Namba Mbili ya mwaka 2021 ambapo baadhi ya mambo makubwa yanayokwamisha utolewaji wa haki yalifanyika. Moja ya mabadiliko hayo ilikuwa ni kuhakikisha kwamba wenyeviti wetu wa Mabaraza ya Ardhi sasa wanakuwa ni waajiriwa na si vibarua au watu wanaojitolea kama ilivyokuwa mwanzo na katika kufanya hivyo mafanikio yameonekana sasa; mafanikio yameonekana kwa sababu waliopo ni kwamba wanakataa rushwa kwa vitendo, lakini kwa wale wachache ambao wameendelea kupokea rushwa nataka nikuhakikishie wizara yako, Serikali yako inaendelea kutoa macho katika hao wasio waadilifu na tutaendelea kuwashughulikia kadri ambavyo tutakwenda kupata malalamiko toka kwa wananchi wetu ambao wanalalamika haki kutotendeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hilo katika mabadiliko hayo ambayo yamefanyika sasa, moja ya jambo kubwa ambalo limefanyika ni kuhakikisha kwamba mamlaka yale ya kuamua juu ya kesi nayo pia yamebadilika, Mabaraza yetu ya Kata na Vijiji yamebakia na kazi ya usuluhishi tu, lakini Mabaraza kuanzia Wilaya ndiyo yanaopenda kuamua on issue of meriting, huku chini wanaamua katika mambo ya mahusiano tu, yaani katika maana kwamba kuwapatanisha wananchi na siyo kuleta mgongano ambao utakuja kutusumbua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikuakikishie Bunge lako kwamba katika mwaka wa fedha uliopita Wizara yetu ya Ardhi imeweza kufungua Mabaraza mapya 20 ikiwa ni sehemu ya kuongeza mkazo wa kuhakikisha kwamba haki inawakaribia wananchi na kuwafikia na katika mwaka huu wa fedha Bunge lako litakapotupitishia mafungu yetu tunakwenda kumalizia Mabaraza 59 yaliyobakia.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)