Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

MHE. PROF. PATRICK A. NDEKIDEMI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nami nitoe shukrani zangu za pekee kwa kunipa fursa mwanamme wa pili kuchangia katika hoja hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Rais wetu kwa kuona umuhimu wa kuiondoa idara hii kutoka Wizara ya Afya na kuifanya idara kamili na niendelee kwa kumpongeza sana Waziri wetu Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima na Naibu wake Mheshimiwa Mwanaidi Ali Khamis kwa kazi nzuri pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, mimi nitaanzia pale alipomalizia mwenzangu Profesa Manya kwamba wazee, nataka nichangie kuhusu wazee. Wazee wako kwenye kundi maalum katika hii Wizara lile kundi maalum linajumuisha wazee, vijana, machinga na watu wenye ulemavu. Sasa mimi ngoja niongelee wazee kwa sababu na mimi ni mzee na hawa wazee hawajapata mtu wa kuwasemea kwa sauti kubwa huku Bungeni kwa sababu moja kubwa muhimu kwamba labda sisi Wabunge wazee ambao tuko huku tunakimbizana kutetea hoja za kwenye Jimbo, akinamama wanatetea hoja zao, kwa hiyo hawana mwakilishi huku lakini leo ngoja niwaongelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wazee ni watu muhimu sana kwenye jamii yetu, tuki-define wazee ni mtu mwenye miaka kuanzia 60, 70 na hata kwenye vitabu vitakatifu vya Qurani na vya kikristu wanasema wazee tuwaangalie ni kundi muhimu sana. Wazee ni amana kubwa na ni utajiri katika Taifa letu, hawa wazee wameshirikiana na Mwenyezi Mungu kwenye kuhakikisha kwamba sote tuliopo hapa tumeumbwa tukawa watu na tuko huku duniani, kwa hiyo hii ni kazi nzuri ambayo wazee wetu wamefanya.

Mheshimiwa Spika, pamoja na haya wazee kwenye nchi yetu ya Tanzania wamekuwa na busara kubwa sana. Rais wetu wa kwanza aliyetuletea uhuru Mwalimu Nyerere aliwashirikisha wazee, walimpa busara na kuhakikisha kwamba wanamshauri mpaka tukapata uhuru. Kwa hiyo, kile chochote tunachoringia nchi hii sasa hivi, majivuno yetu naomba tuwahusishe wazee kwamba wamefanya contribution kubwa sana kwenye mafaniko ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, katika sensa ya mwaka 2012 idadi ya wazee hapa nchini ilikuwa takribani milioni 2.5 ambapo wakinamama walikuwa milioni 1.3 na wazee wanaume walikuwa milioni 1.2. Idadi hii ni ndogo ukilinganisha kwamba Tanzania yetu ina watu karibu milioni 45 wakati wanahesabiwa mwaka 2012. Kwa hiyo, idadi ya wazee ni kama 5.6% tu; kwa nini idadi hii ni ndogo? Idadi hii ni ndogo kwa sababu zifuatazo; kwanza kabisa wazee wengi kule vijijini na mijini ambapo tumeshaona vijana wengi hawana kazi siku hizi wana umaskini mkubwa wa hali ya juu na wengi wao hawana hata pesa ya kununua chakula.

Mheshimiwa Spika, pia wazee wengi kule vijijini wanakumbwa na magonjwa ya uzee kama tezi dume kwa wanaume, kansa za matiti kwa akinamama, kansa za vizazi, magonjwa ya pressure na magonjwa mengine kisukari na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Waziri amesema kwamba wameshatambua wazee kama milioni 1.5 kwenye hotuba yake na wameshawapatia bima za afya, hiyo tunashukuru sana, lakini kusema ukweli hizi huduma wazee hawazipati kama ambavyo tungependa iwe na kutokana na hali hii mbaya ya kwamba wazee hawapati huduma wameishia kuuza rasilimali zao. Kwa mfano mzee anaona niuze shamba au niuze nyumba niliyokuwa nayo kwa sababu watoto wengi hawana uwezo wa kuangalia wazee, anauza shamba, anauza gari, anauza nyumba ili aokoe maisha yake asife, kwa hiyo hiyo ni changamato.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine kubwa ni kwamba wazee wengi wameshatelekezwa kule kwenye jamii, watu wengi siku hizi hawawaangalii sana wazee na hatumlaumu mtu, labda ni kwa sababu za kiuchumi na kipato sio cha kueleweka. Pia kwenye maeneo mengine kuna mauaji ya ukatili kwa wazee wetu, mtu ameshalitumikia Taifa letu hili lakini anaishia kuuawa kikatili kabisa kwa mambo ya kishirikina na kandalika.

Mheshimiwa Spika, changamoto hizi ambazo nimezitaja hapo juu zimesababisha hawa wazee wetu wafe mapema, wanakufa mapema kabla ya wakati wao. Sisi kama Watanzania na Taifa la Kitanzania nimuombe Waziri wetu ni jukumu letu sasa kuhakikisha tunawaangalia hawa wazee wapate huduma zao ili wasife mapema kama ambavyo imezoeleka huko.

Mheshimiwa Spika, wajibu wa kuwalea wazee uko kwenye vitabu vitakatifu, Qurani inasema tuwaangalie wazee na hata Biblia zinasema tuwaangalie wazee kwa hiyo ni wajibu wetu. Mimi niipongeze sana Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wao wameshaanza kuwapa pensheni wazee kule. Kule wazee wanapata pensheni kidogo na mzee hahitaji kitu kikubwa ukienda kule kijijini anakuomba naomba pesa kidogo ninunue sukari. Kwa hiyo, tukianza hata na kuwapa kilo mbili za sukari hawa wazee wetu najua tutafika mahali na mambo yatakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi nyingine kama za Botswana, Swaziland, Seychelles, Mauritius, Afrika Kusini zimeshaanza kutoa pensheni kwa wazee kuwatunza wazee wao na nchi kama Kenya, Uganda na Zambia ziko kwenye mchakato wa kuhakikisha pia wanawapa wazee wao pensheni kwa nini sisi watanzania tusifanye hicho kitu jamani na siyo wengi watu milioni 2.5 tushindwe kuwapa kilo moja au mbili ya sukari.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba nitoe ushauri wangu kwa Serikali. Ushauri wa kwanza kuna sera ya wazee iliwekwa tangu mwaka 2003 naiomba Serikali ishirikiane na wadau wengine ikiwepo Help Age ni Shirika la Kimataifa linalosaidia sana mambo ya wazee warekebishe ile sera iendeane na wakati wa sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, kitu cha pili ninaishauri Serikali mwarobaini wa hii kitu sera tumeshaitunga tutunge sheria ya wazee mtu ambaye hatatekeleza sheria basi atachukuliwa hatua. Kwa hiyo namuomba Waziri uhakikishe kwamba sheria ya wazee ipo kwa sababu tangu hii sera itoke mwaka 2003 mpaka leo bado hamna sheria ya wazee.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ushauri wangu naomba chonde chonde huku Bungeni wazee hatuna wawakilishi ikiwezekana zile nafasi wazee kwa sababu ni kundi maalum nao wapatiwe wawakilishi wao waje huku Bungeni waje waongelee mambo ya wazee. Mimi hapa napambana na Jimbo, wale wengine wanapambana na mambo ya akinamama na kadhalika, vijana wanapambana na mambo ya vijana kwa hiyo wazee ingependeza nao wapate uwakilishi huku Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikiwezekana naishauri Serikali kama ikiwezekana tupawe pensheni hawa wazee hela kidogo tu ya kununua sukari nao ili maisha yaende mbele; na ushauri wangu mwingine ni kuhusiana na Bima ya Afya napendekeza iwe bima itakayoweza kuwasaidia hawa wazee wapate huduma zote bure, siyo anakwenda anaambiwa hii dawa haipo kwenye bima, hapana, bima kama tunasema wazee hawa milioni 2.5 wanapata bima basi wapate huduma zote za kiafya.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali watokomeze kabisa hii tabia ya kumaliza vizee vyetu, wazee unakuta tu labda ana pressure ya macho yamekuwa mekundu anaambiwa ni mchawi wanamuua. Kwa hiyo naomba kabisa Serikali isimame kidedea ihakikishe tunawalinda wazee wetu. Wazee ni utajiri, wazee ni tunu ya Taifa letu naomba tuwaheshimu, tuwahudumie kama Taifa na kwa kufanya hivyo tutapata baraka kwa Mungu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja.