Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu Dkt. Dorothy Gwajima na Naibu wake Mheshimiwa Mwanaidi Ali Khamis na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, wazee ni amana na utajiri wa jamii; wazee ni wadau wa kwanza walioshirikiana na Mwenyezi Mungu katika kazi ya uumbaji. Wazee ni wadau muhimu wa malezi na makuzi ya watoto na vijana na Taifa letu kwa ujumla. Wazee ni watunzaji wa mapokeo hai na wanayo misingi ya jamii na mambo wanayopaswa kuwarithisha vijana.

Mheshimiwa Spika, wazee ni walezi kwa watoto na vijana; wazee ni urithi, amana na utajiri kwa jamii kwani uzoefu na busara zao ni ushuhuda wa kinabii kwa siku hizi.

Mheshimiwa Spika, wazee ni sehemu muhimu sana kwa jamii yoyote ile. Uzoefu na busara za wazee ni kiungo na hamasa kwa maisha ya wanajamii.

Mheshimiwa Spika, wazee wa Kitanzania wamelitumikia Taifa kwa muda mrefu tena kwa namna mbalimbali ikiwemo kuwaletea na kuhakikisha wanapata mafanikio ambayo tunajivunia sasa. Tanapaswa tutambue kwamba wazee hao wamelitumikia Taifa kwa muda mrefu. Tena wamechangia mafanikio makubwa ambayo Tanzania inajivua kwa wakati huu!

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto mbalimbali za maisha ya uzeeni bado wazee wa Tanzania wana nafasi na mchango mkubwa kwa ustawi wa jamii. Wazee ni alama ya utimilifu wa maisha ya mtu na jamii katika ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012, Tanzania ilikuwa na jumla ya watu 44,929,002 ambapo wazee walikuwa 2,507,508 (ambapo wanawake walikuwa 1,307,358 na wanaume 1,200,210) sawa na asilimia 5.6%. Kwa idadi hii Tanzania ina wazee wachache.

Mheshimiwa Spika, sababu za uchache wa wazee katika jamii yetu ni kama zifuatazo; hapa nchini Tanzania katika maeneo mengi hasa yale ya vijijini, uzee umeambatana na umaskini, magonjwa na unyanyapaa unaohusishwa na uchawi. Vitu hivi vimekuwa ni sababu ya kuwatenga na kuwakosea heshima wazee katika baadhi ya jamii zetu za Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, wazee wa Tanzania wanakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo; wengi wanakabiliwa na umaskini wa hali na kipato vijijini na mijini, na baadhi hukosa hata fedha za kununua chakula; wazee katika umri wao, wengi wao wanakumbana na changamoto za magonjwa ya wazee (tezi dume, kisukari, kansa ya kizazi na aina nyinginezo za kansa, shinikizo la damu); upatikanaji duni wa madawa na vifaa tiba kwa wazee na wanapokumbana na changamoto hizi na kukosa msaada, wazee huishia kuuza rasilimali zao kama mashamba na nyumba ili kupata huduma muhimu ambazo hawana uwezo kuzigharamia.

Mheshimiwa Spika, pia baadhi yao kutelekezwa na jamii inayowazunguka na mauaji ya kikatili kwa kisingizio cha imani za kishirikina.

Mheshimiwa Spika, kuwepo kwa wazee pamoja na uchache wao, kunaashiria uhitaji wa ongezeko la huduma mbalimbali kwa wazee. Kutokana na ukweli huu, tunahitaji kuzingatia sana jinsi nchi yetu itakavyoshughulikia matatizo ya watu wetu kuzeeka.

Mheshimiwa Spika, hii ni kutokana na ukweli kwamba hata muumba wetu alionesha kuwajali wazee na hata dini zetu mbili kubwa hapa nchini za uislamu na ukristo zinatuelekeza kuwapenda, kuwajali na kuwatunza wazee.

Mheshimiwa Spika, wajibu wa kuwahudumia au kuwasaidia wazee ni wa kila mmoja. Tuna jukumu kama Taifa au kila mmoja wetu katika jamii kuwashukuru, kuwaenzi na kuwabariki wazee kutokana na mchango wao katika ustawi wa Taifa letu. Hii ni pamoja na kuwapatia kipato kila mwisho wa mwezi ili wewezi kujikimu.

Mheshimiwa Spika, jambo kama hili linafanyika huko Zanzibar na nchi nyingine Kusini mwa Jangwa la Sahara kama vile Botswana, Lesotho, Mauritius, Namibia, Seychelles, South Africa na Swaziland. Mataifa haya yamefanikiwa kuwapatia wazee wao pensheni, na nchi nyingine kama Kenya, Uganda na Zambia ziko kwenye mchakato.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali isikwepe jukumu la kuwatunza wazee kwa sababu nguvu zao za uzalishaji mali zimepungua kutokana na kazi waliyoifanya wakiwa vijana kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa familia zao na Taifa kwa ujumla. Tunao wajibu wa kuwajali wazee wetu kwa hali na mali ikiwa ni sehemu ya matunda ya uwajibikaji wao kwetu na kwa Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, hivyo, ninatoa ushauri ufuatao kwa Serikali; kwanza, Serikali iboreshe Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003 kwa kushirikiana na wadau; sheria inayosimamia masuala yote ya wazee iaandaliwe na kuanza kutumika mara moja; kama ilivyo kwa makundi yote maalumu (vijana, walemavu na akina mama), wazee wapatiwe nafasi za uwakilishi kutetea maslahi yao katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ianze mchakato wa kuwalipa pension wazee wetu ambao hawana msaada wa aina yoyote ule wa kipato. Jambo hili jema na lenye baraka linatekelezwa huko Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, pia wazee wapatiwe bima ya afya inayoweza kupambana na changamoto zote za kupambana na magonjwa ya uzeeni ili wazee wafaidi huduma hizo kama ilivyokusudiwa kwenye sera wa kuwapatia huduma za afya ya mwaka 2007; Serikali ihakikishe mafao ya wastaafu yanalipwa kwa wakati ili kuwaondolea wazee usumbufu wa kufuatilia; Serikali na wananchi wote kwa ujumla kulinda na kutetea haki za wazee, ikiwemo kuthamini mchango, uzoefu na ushiriki wao kwa maendeleo ya Taifa; Serikali iendelee kutekeleza mkakati wa Kitaifa wa kutokomeza mauaji ya wazee na kuhakikisha wazee wanalindwa dhidi ya ubaguzi, uonevu, ukatili na mila potofu na wasiokuwa na msaada, Serikali na wadau mbalimbali waangalie jinsi ya kuwasaidia wale wasiokuwa na makazi, tiba na msaada wa mahitaji ya msingi.

Mheshimiwa Spika, nchini Tanzania kuna Sera ya Wazee iliyotungwa mwaka 2003 lakini hadi sasa haijatungwa sheria ya kusimamia utekelezaji wa sera hiyo. Sheria ya kuwalinda wazee ndio itakuwa muarobaoni wa changamoto za maisha wanazokabiliana nayo hasa ya kiuchumi na afya kwani wanapoishiwa nguvu za uzalishaji, hukosa mahitaji ya msingi anayostahili binadamu.

Mheshimiwa Spika, licha ya Tanzania kuwa na sera ya Taifa inayotaka wazee wasiojiweza kupatiwa matibabu bure, lakini utekelezaji wake bado ni wa kiwango cha chini na baadhi ya maeneo, wazee wamelazimika kuingia mifukoni kwa ajili ya kununua dawa. Wengi ya wazee hao wanasema Sera ya Taifa ya mwaka 2007 inayofungua milango kwa wazee wasiojiweza kupatiwa matibabu bure haitekelezwi ipasavyo na kwamba baadhi ya Waganga Wafawidhi wa Mikoa na hata wale wa Wilaya wamekuwa wakiwatoza fedha licha ya sera hiyo kueleza bayana.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee niipongeze Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kutunga Sheria ya Masuala ya Wazee Na. 2 ya mwaka 2000; kuweka utaratibu wa kuwapatia pensheni jamii na vitambulisho vya kupatiwa huduma mbalimbali wazee wenye umri wa kuanzia miaka 70.

Mheshimiwa Spika, hapa kwetu Tanzania wazee ni utajiri, hatutakiwi kuwatenga wala kuwadharau bali wanabaki kama miamba na walezi wakuu wa mila, desturi na tamaduni njema katika jamii yetu. Katika harakati za kupigania Uhuru wa Taifa letu, Mwalimu Nyerere alielekezwa na wazee mbinu za kutumia na hatimaye tukapata uhuru. Kutokana na umuhimu wa wazee, hata Maraisi wa awamu zote zilizopita wakiwa na jambo huwaita wazee na kuteta nao. Pamoja na umuhimu wao, inasikitisha kuona kwamba wazee hawajaangaliwa kama kundi maalumu kwenye Taifa letu na wanasahauliwa katika maslahi yao.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja.