Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango - Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa - Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa sera ya maendeleo ya jamii ikienda sambamba na ustawi wa jamii na maendeleo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/22 – 2025/26 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, Shule ya Maadilisho ilianzishwa mwaka 1972 baada ya Serikali kubadili matumizi ya miundombinu iliyokuwepo kutoka Kikosi cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na kuwa shule ya kulelea/kuadili vijana watukutu wanaolazimika kutengwa na jamii kufuatia vijana husika kufanya makosa mbalimbali katika jamii. Kwa sasa shule bado ina vijana wachache chini ya 30 ambao wanalelewa/kuangaliwa/kuadiliwa wakiwa chini ya uangalizi wa wafanyakazi 16. Majengo mbalimbali pamoja na yale ya shule ya msingi yaliyopo hapo hayatumiki kikamilifu. Kwa upande wa shule ya msingi, idadi ya wanafunzi ni 102 ukilinganisha na uwezo wa shule hiyo wa zaidi ya wananafunzi 350. Pamoja na miundombinu mbalimbali zipo ekari zaidi ya 448 ambazo zinaweza kutumika kwa ajili ya shughuli za mafunzo ya kilimo na pia kukipatia chuo mahitaji yake ya msingi ya chakula na shughuli nyingine za maendeleo. Kutokana na mabadiliko ya kijamii kuna umuhimu mkubwa wa kuboresha matumizi ya hii shule kuwa Chuo cha Maendeleo ya Jamii na ufundi na pia eneo la Kituo cha Afya.
Mheshimiwa Spika, naomba Serikali kuboresha matumizi ya Shule ya Maadilisho iliyopo Irambo, Kata ya Ulenje, Wilaya ya Mbeya kuwa eneo maalum ili kuanzisha mafunzo ya maendeleo ya jamii, ufundi na hivyo kuiwezesha nchi kutumia nguvu kazi na rasilimali ya vijana kikamilifu na kwa ajili ya maendeleo ya jamii na uchumi wa nchi yetu kwa ujumla. Pamoja na kuwepo kwa shule hii ya sasa, eneo hili liwe kwa ajili ya Shule na Chuo cha Ufundi na Maendeleo ya Jamii pamoja na jamii yote ya Kata ya Ulenje na Tanzania yote.

Mheshimiwa Spika, ombi hili limejikita katika ukweli kwamba kwa kutoa elimu ya maendeleo ya jamii na ufundi kwa vijana, Tanzania itakuwa inaongeza ajira na pia ueledi kwa vijana katika kujenga nchi hasa kutokana na ukweli kwamba nguvu kazi kubwa iko katika vijana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.