Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula na Naibu wake Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa kwanza utahusiana na umuhimu wa diplomasia ya uchumi katika kipindi hiki hapa Tanzania. Kutokana na hali ya kudorora kwa uchumi wa dunia na Tanzania yetu kunakochangiwa na ugonjwa wa UVIKO-19, mabadiliko ya tabianchi na vita vya Urusi na Ukraine, Tanzania inatakiwa kutumia mbinu za kidplomasia ili kujinasua na athari hizi. Kwenye hili, nchi yetu inatakiwa kujielekeza katika kujenga uchumi wa kujitegemea na kutafuta fursa za uwekezaji ili kukuza uchumi wetu kupitia diplomasia ya uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Rais wetu kwa juhudi zake za kuifungua nchi yetu kimataifa. Kwa kipindi kifupi, Rais wetu amefanikiwa kurejesha heshima ya nchi yetu Barani Afrika na nje ya Afrika kama ilivyokuwa kipindi cha awamu za kwanza, pili, tatu na nne. Rais wetu ametembelea mataifa mbalimbali Barani Afrika na nje ya Bara letu pamoja na kushiriki mikutano ya kimataifa kama njia na mbinu ya kuongeza ushirikiano na mataifa mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishauri Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Balozi zetu waelekeze nguvu kwenye kusaidia juhudi za Rais wetu kuitangaza vyema Tanzania ili tufanikiwe kuipaisha nchi yetu kiuchumi na kisiasa. Juhudi zifanyike kushawishi kupitia diplomasia ya kiuchumi kuvutia uwekezaji, biashara za kimataifa na utalii. Tukiongeza nguvu, Tanzania yetu itakuwa na ushawishi Barani Afrika kama zilivyo nchi za Nigeria, Afrika Kusini na Misri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufanikisha hili, ninaishauri Serikali itoe mafunzo maalumu kwa Mabalozi wetu pamoja na wasaidizi wao ili wawe na uelewa wa diplomasia ya uchumi pamoja na mbinu na mikakati ya kuitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili ni kuhusu malalamiko niliyopokea kutoka kwa mwanafunzi wa Sudan aliyemaliza Shahada ya Uzamivu (PhD) katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela iliyoko Arusha, Tanzania. Msomi huyu ni mwalimu wa chuo kikuu huko Sudan. Alipowasilisha vyeti vyake chuoni Sudan ili abadilishiwe cheo, alielekezwa na uongozi wa chuo apeleke vyeti vyake vikathibitishwe kuwa ni halali na ubalozi wa Tanzania huko Khartoum. Alipokwenda kwenye ubalozi, alikuwa na nakala halisi za cheti chake cha PhD, pasi yake ya kusafiria iliyokuwa na kibali cha kuishi Tanzania, kadi ya kitambulisho cha uanafunzi kutoka Chuoni Mandela, barua iliyomsajili chuoni Mandela, na nakala ya dissertation yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwasilisha ushahidi wote huu, Ubalozi wa Tanzania hawajamsaidia na imechukua muda mrefu sana kupata huduma hii na analalamika huenda akachelewa kupandishwa daraja.

Mheshimiwa Naibu Spika, mteja huyu analalamika kuwa atajisikia vibaya sana kama itamlazimu kutuma vyeti vyake Tanzania kuthibitishwa ili hali kuna ubalozi unaoiwakilisha nchi yetu Sudan.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishauri Serikali iwaelekeze mabalozi wetu watekeleze majukumu yao kwa wakati ili kuepuka kero za kulalamikiwa kwani hali kama hizi zinaharibu taswira nzuri ya nchi yetu kwenye uso wa kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa tatu ni kwenye eneo la umuhimu wa Wizara kukuza matumizi ya lugha ya Kiswahili duniani. Lugha ya Kiswahili imetumika kwa mafanikio makubwa sana kuliunganisha Taifa letu. Kiswahili ni lugha ya Taifa na hutumika katika shughuli zote za Serikali likiwemo Bunge. Hivi karibuni sheria imepitishwa na kuelekeza Kiswahili kitumike mahakamani. Kenya inatumia Kiswahili kama lugha ya Taifa, Uganda wanatumia Kiswahili kama lugha ya Jeshi na Polisi. Kiswahili kinatumika Mashariki mwa Congo, Rwanda, Burundi, Visiwa vya Ngazija, baadhi ya maeneo ya Malawi, Zambia, Msumbiji na Somalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lugha hii imekuwa inatumiwa katika kusambaza habari katika vituo mbalimbali ulimwenguni kama vile Sauti ya Amerika, BBC, Deutsche Welle, Monte Carlo, RFI na nchi nyinginezo kama vile Uchina, Urusi na Iran. Aidha, imekuwa ni mojawapo ya lugha muhimu zinazofundishwa katika vyuo vikuu nchini Marekani Uingereza, Ulaya bara, Urusi, Uchina na Barani Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchini Afrika Kusini Baraza la Mawaziri limeidhinisha Kiswahili kifunzwe katika shule za umma na za kibinafsi. Kwenye hili, Kiswahili imekuwa lugha ya kwanza ya Kiafrika inayotoka nje ya Afrika Kusini kufunzwa katika nchi hiyo. Vilevile Umoja wa Afrika na Jumuiya ya SADC imeidhinisha Kiswahili kitumike kama mojawapo ya lugha za kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Wizara ya Mambo ya Nje na Uhusiano wa Afrika Mashariki itatekeleza azma hii kwa kushirikiana na wadau wengine, Kiswahili kina nguvu ya kupanuka katika nchi ambazo hazijawahi kukizungumza na kina nguvu ya kuliunganisha Bara la Afrika na nchi nyingine duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kasi ya ukuaji wa Kiswahili, ninaishauri Serikali kupitia kwenye Wizara hii iwe na mkakati mahsusi wa kueneza lugha ya Kiswahili kupitia Balozi zilizo katika nchi mbalimbali duniani ili Kiswahili kiwe moja ya lugha kuu duniani. Naishauri Wizara iendeleze kwa nguvu zote kuendeleza na kutangaza kiswahili pale alipoachia Marehemu Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.