Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Nishati.

Awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai, lakini pili naomba nitoe pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kutekeleza miradi ya kimkakati ikiwa ni pamoja na Bwawa la Mwalimu Nyerere na miradi mingine ya kugawa umeme nchini ile miradi mikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nimpongeze Waziri wa Nishati na Naibu Waziri, lakini Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa namna wanavyojitahidi kusimamia Wizara hii ya Nishati. Lakini vilevile kwa jinsi walivyoiandaa randama ambayo imeeleza mambo mengi na kama yatatekelezwa itatusaidia sana kuondokana na changamoto ya umeme hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya malengo ambayo Wizara wamesema watayatekeleza ni kuhakikisha kwamba wanaimarisha miundombinu ya usambazaji wa umeme nchini. Katika bajeti ya mwaka jana tulikubaliana kwamba Wizara itatekeleza mradi wa REA (kusambaza umeme vijijini) ndani ya miezi 18. Sasa hivi takribani ni miezi 11 sisi ambao tunatoka katika maeneo haya mradi unatakiwa utekelezwe kwa upande wangu mimi kwa Jimbo la Mbinga Mjini mradi umetekelezwa kwa asilimia 0.3 na huu ni mwezi wa 11 tumebakiza miezi saba. Najiuliza ni miujiza gani wenzetu wataifanya kuhakikisha kwamba hii miezi saba iliyobaki tutakamilisha kutekeleza miradi hii ya REA katika vijiji vyote vilivyobaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Jimbo la Mbinga Mjini ninavyo vijiji 23 ambavyo havijapata umeme wa REA na katika vijiji hivyo kuna kata moja nzima haijapata umeme, lakini katika kata hiyo kuna umeme wa Masista wa Chipole megawati saba unatoka katika eneo hilo na umegawika katika maeneo mengine, lakini hiyo kata mpaka leo haijapata umeme. Huwa inanipa shida sana ninapopita kwenye hilo eneo naulizwa inakuwaje umeme umetoka katika hili eneo, lakini wale wahusika hawajapata umeme hata kijiji kimoja.

Kwa hiyo, nimuombe Waziri atakapohitimisha taarifa yake hii anieleze kwamba ni namna gani ndani ya hii miezi saba atatekeleza kupeleka miradi katika vijiji 23 vilivyopo katika Jimbo la Mbinga Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilikuwa nataka nichangie ni upande wa TANESCO. Shirika letu la TANESCO linafanya vizuri katika kusambaza umeme nchini, lakini changamoto iliyopo kubwa ni kukatikakatika kwa umeme katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukatika huko kwa umeme mara nyingi changamoto inayojitokeza kutokana na miundombinu mibovu. Nilikuwa nawashauri Serikali iangalie uwezekano wa kuimarisha hiyo miundombinu ili wananchi waendelee kupata umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto nyingine ya upatikanaji wa vifaa vya kusambazia umeme katika maeneo mbalimbali. Wananchi wetu wanaomba kuingiziwa umeme katika maeneo yao, lakini unakuta inaweza ikachukua wiki mbili au mwezi mzima hata wengine miezi mitatu hawapati umeme kwa wakati na changamoto inayoonekana iliyopo ni upatikanaji wa vifaa vya kuingiza umeme katika nyumba za wananchi wetu. Kwa hiyo, nilikuwa naiomba Serikali ihakikishe kwamba hii changamoto inaondoka ili wananchi wetu waweze kupata umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ambao tunaishi maeneo ya mjini na ambayo yanapanuka kwa kasi shirika letu la TANESCO lina changamoto kubwa ya kushindwa kusambaza umeme kwenye maeneo yale ambayo wananchi wanaendelea kujenga nyumba mbalimbali. Kwa hiyo, nilikuwa naomba na nilishauri shirika liendelee kwenda na kasi ya miji yetu jinsi inavyopanuka.

Kwa upande wa Mkoa wa Ruvuma umeme umesambazwa katika maeneo mbalimbali, lakini kuna changamoto kubwa kwamba unakuta umeme umesambazwa kutoka Songea mpaka Nyasa, lakini hakuna auto closure zile ambazo zinasaidia umeme ukikatika sehemu moja au ikitokea hitilafu umeme ule usikatike eneo lote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba TANESCO iangalie uwezekano wa kudhibiti hiyo changamoto ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu kama umeme unakatika eneo moja, eneo lingine liendelee kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tunaendelea kusambaza umeme katika maeneo mbalimbali lakini nilikuwa naomba TANESCO au Serikali iendelee kufungua vituo vidogo vidogo katika maeneo yale ambayo umeme unapelekwa ili wawepo wasaidizi ambao wanawasaidia wananchi kuondoa changamoto ndogo ndogo zinazojitokeza ikitokea hitilafu au ukikatika umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nichangie pia kidogo kwenye suala la mafuta; kwanza naomba niipongeze Serikali kwa kutoa ruzuku kwa ajili ya kupunguza ukali wa bei ya mafuta nchini na hiyo tunaiona kuanzia leo angalau kiasi fulani kuna unafuu. Lakini pamoja na hiyo nilikuwa naomba niishauri Serikali kwanza kuimarisha Shirika letu la TPDC ili kuhakikisha kwamba sasa tunakuwa na shirika ambalo litaendelea kutusambazia mafuta kwa bei nafuu. Lakini vilevile tuweke mkakati wa kuhifadhi mafuta ya kutosha nchini ili yaweze kutusaidia pale ambapo patakuwa na changamoto ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo mimi naomba niishie hapo mchango wangu na ninaunga mkono hoja. (Makofi)