Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami nichangie kwenye Wizara hii nyeti ya Nishati.

Kwanza naomba kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo anatupambania na kuhakikisha tunapata fedha za kuendesha miradi ili kuimarisha nchi yetu. (Makofi)

Pili, nimpongeze ndugu yangu Waziri wa Nishati Mheshimiwa January Makamba pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu na timu yote ya Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kupambania nchi yetu iweze kuwa na nishati bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi naomba nijikite kwenye Power Master Plan. Kwenye Power Master Plan tunatakiwa ikifika mwaka 2025 tuwe na megawati zipatazo 5,000 sasa ukiangalia ni lazima tupate vyanzo vingi vya kujazia pale. Katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri ametaja vyanzo vingi, lakini mimi nilikuwa napenda sana kusisitizia chanzo cha umeme joto. Umeme joto ni umeme unaopatikana chini ya ardhi, Tanzania tuna vyanzo vingi. Katika hotuba ya Mwenyekiti wa Kamati amevitaja vyanzo vinne na katika vyanzo hivi vinne tunapata megawati 200. Lakini mpaka sasa mpangilio wa umeme joto bado uko nyuma sana, sasa hapa nilikuwa nataka kutoa ushauri kwamba umeme joto huu kinachosababisha ile mitambo ifanye kazi ni ule mvuke unaotoka chini ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mvuke ule kwa jinsi ilivyo sasa hivi uko chini ya Wizara ya Madini. Sasa unakuta wale wadau wa maendeleo ambao wao ni rahisi sana kuchangia kwenye miundombinu, wanakuwa hawawezi kutupa misaada ya fedha kuendeleza joto ardhi hili. (Makofi)

Kwa hiyo, nilikuwa nashauri kwenye sheria zetu za nchi tubadilishe sheria iwe kama vile kwenye mafuta na gesi, mvuke huu uwe nao chini ya Wizara ya Nishati isiwe chini ya Wizara ya Madini. Kwa hiyo huo ulikuwa ni ushauri wangu. Lakini vilevile naomba kushauri tujipange vizuri kwa hizi rare mineral stones ambazo zenyewe zinatengeneza umeme jadidifu. Sasa hivi dunia inakwenda zaidi kwenye umeme jadidifu, umeme ambao unatumika kwenye magari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nchini tuna madini mengi yakiwemo madini ya nickel, niobium pamoja na graphite na kwenye jimbo langu kuna graphite nyingi ya kutosha. Sasa nilikuwa nafikiri kwamba ni wakati muafaka Serikali kuja na mbinu sahihi ya kuangalia mwenendo wa madini haya na kuangalia sheria zetu zilivyokaa ili tuweze kujipanga, tuingie kwenye ushindani wa dunia wa huu umme jadidifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kwenda kuongelea suala la REA. Kwa kweli nashukuru sana kwa mipangilio mizuri ambayo Mheshimiwa Waziri ameitangaza hapa ya kuweza kutafuta mbinu sahihi ya kufanya umeme vijijini kwa mara moja ili wananchi wetu waweze kupata manufaa mengi. Kwa hiyo, namuomba kwenye area hiyo ambayo amekuja na hiyo mbinu ambazo amezitaja kwamba, kuna makampuni yatapewa yafanye engineering, construction na finance hilo ni jambo bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba juhudi hizo ziongezwe kwa sababu kwa kweli vijijini tuna vitongoji vingi sana, ni vikubwa ambavyo bado havina umeme. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu kuna takribani ya vitongoji 400 ambavyo vimeshakuwa vikubwa na vinahitaji umeme na havina umeme. Vingine viko katika maeneo ambayo viongozi wakubwa wanapita, kwa hiyo mara nyingi vinatoa picha mbaya. Wananchi wakifika pale wanalalamika hawana umeme na umeme unawekwa kwenye kila kijiji, lakini vile vitongoji havina umeme. Kwa hiyo, ni jambo ambalo nilikuwa naomba tulifanyie nguvu ili tuweze kuiboresha nchi yetu vijiji vyote vipate umeme, kwani kule itavutia maendeleo na viwanda vidogo vidogo ambavyo vitasababisha maendeleo kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni TANESCO; kwa kweli wananchi wanajitahidi sana kutaka kujiunga na umeme. Nikichukulia mimi kwenye Jimbo langu kwenye hizi center kubwa za Mkata, Kabuku na Segera kuna wananchi wengi wameshaweza kuweka umeme kwenye nyumba zao na wameomba, lakini vifaa havijakuwa vya kutosha vya kuwaunganishia umeme. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Wizara yetu hii ya Nishati ifanye mbinu ya haraka kuhakikisha wananchi hawa ambao wako tayari na ni wateja ambao wataongeza pato kwenye TANESCO na nchi yetu kwa ujumla waweze kupatiwa umeme haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache nashukuru sana ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)