Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia Wizara hii ya Nishati. Namshukuru Waziri na Naibu Waziri na viongozi wote, Katibu Mkuu wa Wizara na wote wanafanya kazi nzuri, wengi tumewapongeza wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa najiuliza mambo mengi, nikichangia hapa huwa mnaniona. Najiuliza kuhusu Waziri Makamba, wakati Mheshimiwa Makamba anawania Urais mwaka 2015 nilisoma sana hotuba yake. Moja ya hotuba yake aliyokuwa anaisema ni kwamba akiwa Rais atashughulikia mafisadi na wala rushwa katika nchi hii, akasema nchi yetu inaweza kwenda mbele au ikarudi nyuma kutokana na matumizi mabaya ya fedha za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikuombe kwa hilo ambalo ulilokuwa unalisema kipindi hicho, kwenye Wizara yako tunataka kukuona kwa miaka hii ambayo mama amekupa, tuone unatekeleza yale ambayo ulitaka kuwa Rais, leo nilikuwa nataka nikupe ushauri. (Makofi)

Lingine ambalo nikuseme Mheshimiwa Makamba ni kwamba ni moja ya vijana bora wa Afrika waliosoma chuo kikubwa duniani Harvard University ni vijana bora waliosoma na Watanzania na wale ambao walipelekwa na CCM. Umekaa Harvard miaka mingi, nategemea sasa ukija hapa uta-apply mambo makubwa ingawa Watanzania hawayaoni, lakini wanayaona hiki ulichotutengenezea hapa leo ni jambo kubwa sana na mabanda uliyoleta juzi hapa ni jambo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ndugu yangu Makamba umesoma Harvard, Harvard ambayo ina vitabu ma-cover yake yamefunikwa na ngozi ya binadamu unaogopa nini? Harvard ambayo ina watu ambao wanafanya sayansi jumla ya miili iliyoko pale ni 23,000 unaogopa nini Harvard ambayo maraisi saba wa Amerika wamesoma pale, unaogopa nini kutekeleza mambo haya? Nina imani na wewe kwamba sasa tumepata mtu wa kutupeleka kwenye mwanga ni wewe, ukishindwa ni uzembe wako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nishauri tu sasa wasomi hawa wakisoma sana wanataka kila kitu wafanye sayansi ndio shida sasa, kwa mfano hivi karibuni wakati unatoa hotuba yako umetuambia mambo mazuri sana, lakini moja umesema utaunda tume ya kwenda kuchunguza maeneo ya mjini yanayofanana na vijijini uyape umeme. Uunde tume miezi sita, hayo ndio matatizo ya wasomi. Kumbe sisi Wabunge tunaweza kuwa tume, ukasema baada ya hapa kila Mbunge alete maeneo ambayo yanafanana na vijijini yanayohitaji umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wenyewe ni tume hapa, hizo hela za tume tupe sisi tuweke mafuta mzee, halafu baadaye wewe tuma watu wako wilayani na mkoani wakachunguze haya maeneo. Nakujua msomi kazi yake ni kuhakikisha kwamba hawezi kufanya jambo lazima alifanye kwa utafiti, sasa u-apply geopolitics ya Marekani na Tanzania ni vitu viwili tofauti, sisi hapa hatuna hela, wenye hela ambazo ungezitumia kuunda tume ungetupa sisi tuunde pale kwenye Jimbo langu nina vitongoji zaidi ya 37 havina umeme, hizo hela zingekuja upande wa pili.

Kwa hiyo, mimi nakushauri uangalie upya kwamba tume ya nini, sisi wenyewe Wabunge ni tume, leta makaratasi hapo leta fomu hapo tujaze halafu fuatilia uone kama ni ukweli ama sio ukweli, kwa hiyo jambo litakuwa liko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri nimeangalia hivi vipaumbele vyako kweli nimesikitika sana yaani kabla sijafanya utafiti nimesikitika mno, hivi najiuliza vipaumbele viko 12 Bwawa la Nyerere liko wapi ambalo lina shilini trilioni 6.55 liko wapi kwenye vipaumbele hivi ambavyo umevitoa? Lakini nikajua kwamba pengine umejumlisha kwenye kipaumbele Na. 1 haiwezekana, kwa sababu political is all about perception unaweza ukasema mtu akaangalia akasema Bwala la Nyerere limeachwa haliko kwenye vipaumbele tutasemaje sisi watu wa CCM tutasemaje, lakini kumbe umeliweka humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofunua ukurasa wa pili nikakuta unasema miradi ya kusafirisha umeme, ukasema miradi ya uzalishaji wa umeme iliyopo katika hatua za utekelezaji; Bwawa la Nyerere ambalo umelitaja hapa shilingi trilioni 6.55 umelitengea shilingi trilioni 1.44 maana yake hili bwawa fedha yake imechukuliwa ni karibu ya nusu ya bajeti yako yote ambayo ina shilingi trilioni 2.9. Kwa hiyo hapa umelifanya vizuri, lakini nikuombe kipaumbele cha kwanza ni Bwawa la Nyerere, hili bwawa likiwepo maana yake matatizo ya umeme yanaisha, nikuomba hii karatasi ibadilishwe iwekwe upya Bwawa la Nyerere liwekwe la kwanza, lifanane na hiyo tunayokuwa tunazungumza hapa, lakini kwenye bwawa hili mimi najiuliza mambo mengi sana, nimesikia kuna changamoto ya Bwawa la Nyerere, najiuliza ni changamoto gani hizo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kama kuna changamoto tuletee, sisi tunaamini wataalam na wanasheria nguli wa Tanzania waliokwenda kufanya mikataba ya ujenzi wa Bwawa la Nyerere wamejiridhisha na kila kitu. Kwa hiyo mkandarasi anapaswa kufuata ile mikataba waliyoweka, sasa kama kuna changamoto zinatoka wapi?

Mimi nikuombe kama inawezekana waite wote waliofanya mikataba, wanasheria wote nguli, kaa nao na mkandarasi pengine mkandarasi ameona sasa wewe umeenda anakupa mambo mapya, mikataba iliyoko pale walioifanya wamefanya kwa uhakika zaidi, ifuate na mkandarasi afuate mikataba atekeleze mradi. Akikuzingua na wewe mzingue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sasa nirudi kwenye jimbo langu, mimi nakushukuru sana tena sana na Watanzania na Wabunge niwaambie huyu Makamba ni moja ya vijana ambao tunatakiwa kumtumia sana, tatizo tu kwamba ana-apply geopolitics ya Marekani, sasa arudi kwenye polepole ya Tanzania, asiwe na magharama makubwa ya kutekeleza miradi lakini ana uwezo wa kutengeneza vitu vyovyote vile, ana uwezo wa kufanya jambo hilo, nikushukuru kwa sababu ya mabanda yako uliyoleta hapa tumetembelea mabanda yote, nimekutana na TANESCO mkoa nilikuwa na Wajumbe wa Serikali za Vijiji nilikuwa na Wenyeviti wa Vijiji karibu 30 wamejiridhisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo maeneo yote ya Kurusanga, Kata ya Salama Kurusanga na maeneo yote ya Mgeta, Gogea, Bukoba na maeneo yote ya Machimolo pale Janungu na maeneo yote ya Nyamswa yote kwenye vijiji vyote ambayo tumeleta utaenda kuyatekeleza na bahati nzuri wamenipa uhakika huo. Kwa hiyo wananchi wa Jimbo la Bunda, wananchi wa Tarafa ya Chamliho wajiandae kupokea umeme wa Makamba ambao sasa utatuweka kwenye mambo mazuri katika mwanga utakaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho ambalo naliona hapa ni suala la kuweka umeme vijijini, hivi tuna kitu kinaitwa REA, kuna ka mradi kanaitwa densification, kamradi kale kalikuwa kanafadhiliwa na watu wa nje hivi kamekufa au kapo? Maana yake siku hizi sikaoni sana kanaendelea labda ukija hapa utanipa majibu kale kamradi ka-densification kamefia wapi? Kalikuwa kanaenda kama kamradi kanatelekeza umeme kwa msaada wa hela za nje, sasa tujue kamradi kanaenda wapi, kanakuja au kanaenda sehemu nyingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine ambacho nakiona hivi tunapeleka umeme vijijini, unaenda unaweka transfoma ya volti 50 halafu inabeba watu 20, sasa watu wanafika mpaka 50, mpaka 70 transfoma ni hiyo hiyo haibadilishwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, transfoma ya kilovolti 100 inabeba watu mpaka 300 haibadilishwi, sasa kwa nini umeme usikatike? Lazima ukatike tu, haiwezekani kuweka transfoma ya kubeba watu 20 halafu watu wakatumia 60, wakatumia 100 haiwezekani. (Makofi)

Kwa hiyo, kama ni tume ya kuunda ni hiyo sasa kaunde tume ya kutazama maeneo gani ya transfoma zina matatizo ambazo zinafanya umeme unakatikakatika. Sasa umeme unapokatika unatuletea shida sana na mimi Mheshimiwa Makamba nikuambie sasa watu wa REA na watu TANESCO uwaambie siku Yanga na Simba zinacheza umeme usikatike na siku tukienda kule Arusha umeme usikatike, siku tunaenda kucheza na Coastal umeme usikatike, sasa hilo liwe agizo kwamba sasa siku tunafanya mambo yetu umeme usikatike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi namkushukuru sana Mheshimiwa Waziri Makamba kwa kweli uwezo unao, sasa ukishindwa kutekeleza hii Wizara wakati mama amekupa amekuamini na sisi tumejilizisha na kisomo chako....

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mnenaji hapa anazungumza kwamba January Makamba ana uwezo mkubwa, lakini ningependa nimuongezee taarifa kwamba hata Mkurugenzi wa TANESCO Maharage Chande ni mmoja ya vichwa vigumu tulivyokuwa navyo hapa Tanzania, kijana mbunifu, lakini pia yupo Mwenyekiti wa Omary Issa mwanzilishi wa Celtel Tanzania namfahamu vizuri, ni mmoja ya vichwa vigumu sana tulivyonavyo hapa nchini ahsante sana, nataka nimuongezee tu kwamba hilo TANESCO ipo salama, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwita Getere, unapokea hiyo taarifa?

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea lakini nilitaka kujua labda analeta Simba ambaye imemfukuza kocha kumbe ameleta mambo mazuri, naipokea. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwneyekiti, nashukuru kwa yote hayo na naunga mkono hoja. (Makofi)