Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie bajeti hii na niungane na Waheshimiwa Wabunge wote walioendelea kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri pamoja na Mheshimiwa Waziri January Makamba na Naibu wake Mheshimiwa Stephen Byabato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba nimekutana na Mheshimiwa Waziri na changamoto zangu ameweza kunisikiliza vizuri, lakini bahati mbaya wakati nazungumza na Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Ludewa walionituma hawakuwepo, kwa hiyo, hawakusikia. Kwa hiyo, naomba nirudie niliyoyaongea kwa Mheshimiwa Waziri. Nikiri pia kwamba nimezungumza na Mkurugenzi wa REA changamoto zangu ameweza kuzisikiliza vizuri na nipongeze sana Wizara hii kwa kuandaa wataalam wote kuja hapa viwanja vya Bunge kuweza kutusikiliza. Kwa hiyo changamoto zetu tumeziwasilisha tunaamini zitafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa maana ya wananchi walionituma wasikie nikiwasemea, naomba nianze kwa kumuomba sana Mheshimiwa January Makamba kule Jimboni kwangu Ludewa hasa Tarafa ya Masasi, Serikali imefanya kazi nzuri sana ya kusambaza umeme isipokuwa ni ngazi ile ya vijiji kwenye vitongoji mbalimbali bado kuna malalamiko sana na nilifanya ziara kwenye vijiji vyangu vyote 77 vikiwemo hivi vya Tarafa ya Masasi. Nilikwenda Kitongoji cha Chingole pale Manda kuna wananchi walikuwa hawajaunganishiwa umeme. Kwa hiyo, naomba sana na vitongoji vingine vya Manda viweze kuunganishiwa umeme pamoja na Tarafa yote ya Masasi. Huu mradi wa vitongoji naomba Ludewa nao iweze kupewa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna mradi wa REA ambao uko kwenye tarafa ya Mwambao, kuna mkandarasi mmoja alipewa kazi kwenye Kijiji cha Mkwimbili, Kata ya Makonde, Kata ya Lifuma, mkandarasi huyo anashindwa kuwasha umeme tokea mwezi Aprili kwa sababu niliomba Serikalini wapewe umeme mkubwa wa KV 33, lakini sasa umeme uliotoka Makao Makuu ya Wilaya ya Ludewa kwenda Lupingu ni KV 11. Kwa hiyo sasa waliomba na nashukuru niliongea na engineer wa TANESCO Ludewa amekiri kwamba Mheshimiwa Waziri ameshatoa maelekezo, kwa hiyo naomba amsisitize ili aweze kubadilisha hiyo KV 11 Kuwa 33 ili wananchi wa Mkwimbili, wananchi wa Makonde na wananchi wa Lifuma waweze kuwashiwa umeme mapema iwezekanavyo, kwa sababu zile nguzo tokea ziwekwe wamekuwa wakipiga nazo picha mwaka sasa umeisha, wanatamani sana umeme uweze kuwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa Tarafa ya Mwambao, kuna vitongoji ambavyo vina idadi kubwa ya watu, kuna Kitongoji cha Ndamba na Kitongoji cha Kilindi, Kitongoji cha Ndamba kipo pale Kata ya Makonde na Kitongoji cha Kilindi kipo Lifuma, ni vitongoji ambavyo vina idadi kubwa ya wananchi ambao wapo willing na wameupokea mradi vizuri, lakini hawa wameachwa, naomba nao wafikiriwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Tarafa hii ya Mwambao kuna mkandarasi mwingine ambaye amepewa Mradi wa Kusambaza Umeme Kata ya Lumbila, Kijiji cha Ndoa, Kitongoji cha Kimata, Kitongoji cha Kitewele na Liunji, Mkandarasi huyu bado hajapeleka nguzo kwa muda mrefu sana tokea asaini mkataba. Nilivyozungumza naye alikuwa amezungumza kwamba ameshawasiliana na watu wa meli ya mizigo pale Itungu kwa sababu ipo vizuri inafanya kazi, watapeleka. Naomba ahimizwe ili aweze kufanyakazi ili kule mwambao kwote waweze kupata umeme kama maeneo mengine ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Kijiji cha Kitewele ambacho kipo Kata ya Mawengi, eneo hili lipo jirani na mzalishaji binafsi umeme wa JUHUMA. Kwa hiyo nilishauri ili waweze kufikisha umeme huu ni vizuri wakaingiza kile Kijiji cha Mawengi kwenye Mradi wa REA ili waweze kupata uelekeo mzuri wa kupeleka umeme katika Kitongoji cha Liunji na Kitongoji cha Kitewele. Kwa hiyo kwa Tarafa ya Mwambao tutakuwa tumemaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika niliweza kuzungumza na Mheshimiwa Waziri na Mkurugenzi wa REA kwamba wananchi kwenye vijiji 20 vya Jimbo langu la Ludewa ambao wanategemea umeme wa mzalishaji binafsi Kampuni ya Madope, kwa kweli tunaomba sana Serikali isaidie Kampuni hii ya Madope, kwa sababu jukumu la msingi la Serikali kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na namwona Mwanasheria Mkuu wa Serikali pale, najua atatusomea kama si Ibara ya 8 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, kama ilivyofanyiwa marekebisho yake mara kadhaa, inasema jukumu kubwa la Serikali ni ustawi wa wananchi. Kwa hiyo umeme ni ustawi wa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa jukumu hili ni la Serikali, naomba sana Serikali iweze kumsaidia huyu mzalishaji binafsi Kampuni ya Madope kwa sababu vijiji 20 ni vingi sana kupata mgao wa umeme wa masaa zaidi ya 12. Naamini kabisa wakipewa nyaya kwa sababu ule mradi wa mwanzo zile nyaya zilizowekwa zilikuwa ni aluminum millimeter 50. Wamejitahidi wao kwa nafasi wameweza kuhakikisha Mkiu ile Kata ya Lubonde wanapata umeme masaa yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili waweze kutatua tatizo hilo Kata ya Madilu na Kata ya Mlangali, wanahitaji kupata nyaya ili waweze kubadilisha ile miundombinu, waweze kufikia na Kata ya Madope na Lupanga. Kwa hiyo naomba sana Wizara hii, nikiri kwamba baada ya kuwasiliana na Mkurugenzi wa REA, Bodi ya REA imefika pale wameona hizi changamoto, hilo lazima niwe muungwana, Mkurugenzi mwenyewe amekwenda ameona changamoto na yeye atakubaliana na mimi kwamba kuna haja REA na mimi Mbunge na wale wazalishaji wa Kampuni ya Madope tuna kila sababu ya kupita kwa pamoja na watalaam wa REA kwenda kuzungumza na wananchi, kuwapa uhakika kwamba wale ambao wateja wapya hawajaunganishiwa umeme kule Lupanga wawe na uhakika kwamba hadi lini matatizo haya yatakuwa yametatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niendelee kuishukuru Serikali, tulikaa kikao na Mkurugenzi wa REA kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri waliweza kutoa Shilingi Milioni 307, Milioni 150 zilitolewa lakini hizo zilizobakia wamewadhamini Kampuni ya Madope kuweza kuchukua nyaya kwa mzalishaji. Naomba Mkurugenzi wa REA atusaidie kuongea na yule mzalishaji ili nyaya hizi ziweze kutolewa haraka ziwawezesha Kampuni ya Madope kuunganisha umeme kwenye gridi ya Taifa, ule mkataba ambao wanauzia Serikali, itawasaidia kupata mapato yatakoyoweza kutatua changamoto ndogondogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukitatua tatizo la mgao wa umeme kwenye hivi vijiji 20 na tukaenda kusaidia yule mzalishaji binafsi wa JUHUMA ambaye anazalisha umeme pale Mawengi, unakwenda Milo itasaidia sana kuweza kumaliza kero za umeme kwenye Jimbo la Ludewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo haya ninayoyasema ni maeneo ya uzalishaji mkubwa sana. Pale Mlangali idadi ya watu ni kubwa, pamekaa kibiashara, kwa hiyo, kukosa umeme pale kwakweli ni kuwaadhibu sana wale wananchi. Nimepita juzi wakanisimamisha, nilikuwa natoka kwenye ziara jimboni, kilio chao kikubwa wananchi wa Mlangali, Madilu, Madope, Lupanga na pale Lugarawa ni umeme na katika maeneo haya kuna vituo vya afya, kuna taasisi, kuna chuo cha afya, kuna chuo cha VETA pale Shaurimoyo kinajengwa na Serikali imetoa bilioni tano na milioni mia nne, kipo kwenye Kata hii ya Lugarawa. Kwa hiyo, kuna taasisi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili niendelee kuomba sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Nape ametuwekea booster pale Milo ya TBC lakini pale hakuna umeme. Nimshukuru Meneja wa TANESCO, Mkoa wa Njombe ameshawasilisha kwenye bajeti hii na ndiyo maana naunga mkono hoja kwa sababu kuna fedha nimeona zinakuja jimboni kwangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, naunga mkono hoja, naomba tu changamoto zote za Jimbo la Ludewa ziweze kutatuliwa na kukatika kwa umeme kuweze kuisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.