Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Mohammed Said Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Konde

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara hii ya Nishati. Awali ya yote, niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Nishati Mheshimiwa January Makamba pamoja na Naibu wake, lakini pamoja pia na watendaji wake katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli dira ambayo wameionesha ya kutuhakikishia Watanzania kupata umeme wa uhakika ni nzuri sana, mipango yao kwa kweli mimi binafsi naipongeza. Pia hii imeonesha, pale ambapo katika michango yetu ya leo Wabunge, baada ya kupata semina ambazo zimetupa uelewa mkubwa, nimeona pia Wabunge wengi sana wameelewa mipango ya Wizara. Kwa hiyo, hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitaanza kwa sehemu ya Umeme wa Joto Ardhi yaani geotherm. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake hapa ameonesha kwamba tutapata umeme wa megawatt 195 ya Umeme wa joto ardhi, lakini mimi kama Mjumbe wa Kamati tulivyofuatilia tumeona kwamba bado Sheria ya JotoArdhi haijawa sawasawa, haijatekelezwa. Sasa najiuliza maswali, ni wapi hasa Waziri anaweza kuja kutekeleza kuzalisha umeme wa jotoardhi wakati bado haijatambulika kwamba bado ni sehemu ya madini ama ni sehemu ya nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waziri anapokuja ku-windup atueleze tayari amefikia wapi kwanza sheria haijaletwa, lakini la pili hakuna miundombinu na la tatu pia bado fidia kwa wanaomiliki maeneo haya yenye jotoardhi haijafanyika. Kwa hiyo, tunakujaje kuzalisha umeme huu wakati haya mambo ya msingi bado. Tunaomba anapokuja ku-windup atufahamishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa REA, tunawapongeza sana mpango wao ni mzuri kwa kuhakikisha kila kijiji, kila kitongoji kinapata umeme unaostahiki, lakini kuna tatizo kidogo ambalo limejitokeza. Tulivyofanya ziara Kamati tuliona kwamba REA imepeleka umeme kijijini lakini nyumba zilizounganishwa ni mbili. Ina maana hapa hakuna maandalizi mazuri, watu hawakuandaliwa na pale tayari kuna mkandarasi tayari ameshalipwa, waliopata umeme ni watu wawili ama watatu, lakini zipo nyumba za jirani hazipata kwa sababu hawakuandaliwa. Nashauri kabla ya kufika pale wananchi waandaliwe, wafanye fitting ili wote wa-enjoy ule umeme wa REA unaokwenda pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia ni hili suala la ujazilizi; naona REA kwanza tulianza mita moja, halafu tukaenda mita mbili, halafu tunaenda ujazili, yaani tunakwenda mwisho tutafika hata majina mengine hatuyafahamu. Kwa hiyo, nashauri kwamba sisi lengo letu si mita moja, si ujazili lengo letu ni kuwapa umeme wa uhakika wananchi. Kwa maana hiyo tuhakikishe ile sehemu ambayo tuna deal nayo, basi wapate umeme wote sio tunarudia, hili jambo linatutia hasara kama Taifa, kesho tunarudia, kesho mkandarasi huyu, kesho mkandarasi huyu, linatutia hasara. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili pamoja na timu yake waliangalie ili kuondoa hasara kwa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niende kwenye suala la bei za umeme; hili suala la bei za umeme, nazungumzia umeme wa mijini, sizungumzii umeme wa vijijini ambao huo tumeshaujua ni Sh.27,000. Mheshimiwa Waziri watu wa mijini ambao tayari wana umeme, wale wenye uwezo tayari wameshaweka umeme kwa maana hiyo watu ambao hawajaweka umeme, hawana uwezo kwa nini sasa tumekwenda kuweka bei ya shilingi 320,000; shilingi 500,000 au shilingi 600,000 bila kuangalia hawa maskini ya Mungu, watu wanaishi mjini wanasaidiwa na watu wa vijijini. Kwa maana hiyo lazima hizi bei za umeme kwa sehemu za mijini bado tuziangalie, hii shilingi 320,000 ni kubwa mno, maskini ni wengi pale, tuna umaskini mkubwa katika nchi hii hata kama watu wanaishi mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba bei hii ya shilingi 320,000 ni kubwa sana, hata kama hawatalipa shilingi 27,000 lakini iangaliwe ilipwe ya nafuu ameshauri hapa Mbunge wa Manonga kwamba wao walikuwa wanalipa shilingi 170,000, hiyo kidogo ni affordable, lakini huwezi ukalipa 320,000 hata kazi huna na wewe unataka umeme, unataka kuuza ice-cream, unataka kuuza biashara ndogondogo, lakini hamna. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba aliangalie hili ili tupate bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia pale ambapo mwananchi ameshalipa kuunganishia umeme, kunakuwa na muda mrefu anafuatilia muda mrefu, tunaomba Waziri aje na commitment hapa baada ya kulipa atachukua muda gani kuunganishiwa umeme kwa sababu watu wanachukua mpaka miezi miwili, mitatu, tayari wameshalipa lakini hawapati umeme. Kwa hiyo, Waziri atuambie muda halisi hasa baada ya kulipa ni shilingi ngapi na baada ya hapo nini kitafuata kama mwananchi hakupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa sikuona sehemu ambayo kutakuwa na ukarabati wa mabwawa kama vile Hale, Kidatu, Nyumba ya Mungu, Rusumo ambayo haya ni mabwawa yetu ambayo sasa hivi yanatuzalishia umeme, hakuna ukarabati, kwa maana hiyo anapokuja ku-windup atueleze kwamba haya mabwawa ambayo sasa hivi ndiyo tunafaidi keki yake, kuna mpango gani wa kuyaendeleza kwa sababu sasa hivi unapokwenda pale ukiangalia ile mitambo imechakaa. Kwa nini tusiipangie mipango ili ikawa nayo ni mazuri iendelee kutupa umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la mafuta; kwa kweli suala la mafuta napongeza bei ambazo zimetangazwa kwa sababu zimekuja kuleta unafuu mkubwa kwa Mtanzania. Kwa mfano, Dar es Salaam imepata ruzuku ya kila lita ya petrol Sh.306 lakini diesel Sh.320. Hii ni nafuu kubwa Mheshimiwa Rais anapaswa kupongezwa, lakini pia Wizara imefanya kazi nzuri, tunategemea kwamba huu mpango utakuwa ni endelevu na wananchi wapate nafuu waweze kufaidika na hii hali nzuri ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nataka kuzungumzia hii TPDC. Hii TPDC ina mchango mkubwa kwa Taifa, tuliiunda wenyewe na kwa ajili ya kufanya biashara ya mafuta, lakini cha kushangaza mtaji wake wote umemegwa na TANESCO na sababu ni nini? TANESCO wanauziwa umeme kwa kutumia gesi, lakini hawalipi, sasa leo unakuja kutuambia unaanzisha vituo vya TANOIL, yaani unaandaa nguo za mtoto lakini mama unampiga viboko atazaaje huyu mama… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)