Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa hii nafasi muhimu sana ya kuchangia bajeti hii muhimu kwa Watanzania. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa fedha shilingi 100,000,000,000 alizotoa, imeonesha kabisa kwamba Rais wetu anajali maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa mara ya kwanza tangu niwe Mbunge nimeshuhudia Waziri anawasilisha hotuba yake ya Bajeti bila kumleta mke wake humu ndani, badala yake Mheshimiwa Waziri ametuletea hivi vipaumbele vya bajeti imeonesha kabisa huu Waziri yupo serious. Mambo ya kuja kuuza sura hapa yeye hana, yeye yupo serious na kazi. (Kicheko/Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, nimesoma hotuba yake ya bajeti yote, jamani Wabunge naomba mnisikilize. (Kicheko/Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwenisongole wewe ndiye unayechangia, endelea kuchangia kiti kinakufuatilia.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, okay, ahsante.

MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa, karibu.

T A A R I F A

MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji, akinamama wanaoletwa hapa Bungeni wanakuja kwa heshima zote, ni walezi wa familia, wanajaliwa na hawa waume na hawa wanawake na ndio maana wanaletwa hapa, hawaji hapa na wala hawaletwi hapa kwa ajili ya kuuza sura. Haya ni matusi makubwa sana kwa wanawake, naomba arekebishe maneno yake, maneno ya hovyo kabisa haya. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lucy Mayenga, ni taarifa au unataka afute maneno yake.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, afute.

MWENYEKITI: Nazungumza na Mheshimiwa Lucy Mayenga, kiti kikizungumza unanyamaza.

MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, arekebishe maneno yake Hansard ikae sawa, haiwezekani wanawake wanaokuja hapa Bungeni, ikaonekana wanakuja kuuza sura.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lucy Mayenga ulitumia taarifa, kwa hiyo Mheshimiwa Mwenisongole taarifa unapokea?

GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona Mheshimiwa Lucy Mayenga hajanielewa, mimi nimempongeza January Makamba, yeye alichokisia…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Kuhusu Utaratibu

KUHUSU UTARATIBU

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama kufuatia kauli aliyotoa mchangiaji ambayo ni ya maudhi, wakati anachangia amempongeza Waziri wa Nishati, lakini ameenda mbele zaidi akadhihaki kwa kusema kwamba Mawaziri ambao wanawaleta wenza wao hapa wanawaleta kuja kuuza sura na hawapo serious. Sasa kanuni zetu zinakataza lugha za kuudhi kwa hiyo ningependa mzungumzaji afute kauli, hiyo kauli aliyotoa ambayo inaudhi na inakera. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Esther Matiko amesimama kwa kifungu cha Kuhusu Utaratibu, Kanuni ya 75 bila shaka inayotaka kufahamu ni kanuni gani ambayo imevunjwa maana ndio msingi wa kifungu hiki. Labda nikusomee: “Mbunge yeyote anaweza kusimama wakati wowote na kusema maneno “kuhusu utaratibu” ambapo Mbunge yeyote ambaye wakati huo atakuwa anasema atanyamaza na kukaa chini na Spika atamkata Mbunge aliyedai utaratibu ataje Kanuni au sehemu ya Kanuni iliyokiukwa”.

Mheshimiwa Esther Matiko ni kanuni gani imekiukwa.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni ya 71(1)(j).

MWENYEKITI: Kanuni ya 71(1)(j) inayosema lugha za kuudhi ni pamoja na hatatoa lugha ya matusi au ishara inayoashiria matusi au kumsema vibaya Mbunge au mtu mwingine. hatotumia lugha ya kuuzi au inayodhalilisha watu wengine.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, yes, 71(1) (j).

MWENYEKITI: Mheshimiwa George Mwenisongole amesimama Mheshimiwa Matiko hapa kukutaka ufute maneno uliyotumia ya kutambulisha kwa sababu tunao utaratibu Bungeni hapa wa kuruhusu wageni mbalimbali kuja wakiwemo viongozi pamoja na wanaoambatana na viongozi wenzetu. Kwa hiyo kuwaita waanauza sura ni maneno yasiyofaa, kwa hiyo futa maneno yako hapa ili uendelee kuzungumza. (Makofi)

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nafuta kauli ya kuuza sura, lakini nabaki na msimamo wangu wa kumpongeza Mheshimiwa Waziri…

MWENYEKITI: Sasa sikiliza Mheshimiwa Mwenisongole, ukifuta ukasema lakini nitakukalisha usiendelee kuzungumza.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa nafuta kauli. (Makofi)

MWENYEKITI: Haya, endelea kuchangia.

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

La pili nampongeza Mheshimiwa Waziri, nimesoma hotuba yake yote ya bajeti, katika hotuba yake ya bajeti kwa mara ya kwanza tangu nimekuwa Mbunge asilimia 99 ya fedha anazoomba zote zinakwenda kwenye miradi ya maendeleo, sijawahi kuona hiki kitu, ni asilimia moja tu ya bajeti yote ya Wizara ya Nishati inakwenda kwenye matumizi ya kawaida. Hiki ndicho ambacho sisi na Watanzania tunataka kukiona, hiki ndio kilio cha Watanzania kuona fedha za wananchi nyingi zinakwenda kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kaka yangu January, Mheshimiwa Waziri nina mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Serikali ili ilisaini mkataba wa REA na wakandarasi mwezi Juni, mkataba wa miezi 18 na sisi kama Wabunge na wananchi wote tulifurahi tukiamini kwamba vijiji 3,448 vilivyobaki kwenye mpango wa REA vinakwenda kumalizika na kwa mara ya kwanza umeme utafika katika vijiji vyote Tanzania. Hata hivyo, cha kusikitisha hawa wakandarasi hawa ambao kwa kweli sijui wamepata wapi hiyo jeuri, waliposaini mkataba wa miezi 18 walipewa miezi sita, hiki kipindi kinaitwa mobilization period na walilipwa 25 percent ya gharama yao, wakaambiwa mobilization period ni kipindi ambacho mkandarasi anatakiwa afikishe vifaa vyote site au ahakikishe vifaa na taratibu zote zimefika site.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo vifaa ambavyo mkandarasi wa REA anavihitaji ni nguzo, transformer, LUKU na nyaya ambavyo vyote vinazalishwa hapa nchini. Kwa mshangao hawa wakandarasi mwaka huu mwezi Machi wanatuambia vifaa vimepanda, kwamba umeme wa REA hauwezi kuendelea kwa sababu gharama za vifaa zimepanda, lakini cha kushangaza hata Waziri naye anakubaliana na sababu hizi ambazo hazina mashiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walikuwa wapi katika kipindi cha mobilization period kupeleka vifaa kwanini wasiseme kipindi hicho, Miezi sita wao kupeleka vifaa site imefika, leo hawawezi kuja wakatuambia umeme wa REA umeshindwa kufika kwa sababu vifaa vimepanda, hivyo vifaa vimepanda mwaka huu. Kwa hiyo, ni kwamba maamuzi ya Waziri kukubaliana na hizi hoja za Wakandarasi si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu ya CCM imeahidi umeme utafika vijijini kufikia Disemba, vilevile Mheshimiwa Waziri katika hotuba yako hujatuambia sasa umeme huu wa REA utaisha lini na hawa Wakandarasi wanadai kiasi gani sasa za kupanda. Pia katika majadiliano na Wakandarasi si kuna kitu kinaitwa variation ambayo mnaweza mkakaa na Wakandarasi mkajadiliana variation ambayo imepanda, hata ukiangalia bidhaa zote za hawa Wakandarasi wanazozihitaji zinazalishwa hapa nchini! Sasa transformer zipi, nyaya zipi, LUKU zipi au nguzo zipi zimepanda kiasi cha kusababisha huu mradi wa REA usiendelee? Kwa kweli ni jambo ambalo inabidi tuwe makini sana na Wakandarasi otherwise watatuletea historia ya mtu na Ngamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ngamia alikwenda kwa mtu mmoja akamuomba aingize mguu, yule mtu akamkubalia baadaye akasema naomba niingize na kichwa yule mtu akamkubalia, mwisho wake ngamia akaingia nyumba nzima akatoa! Tukiendelea kuwakubalia Wakandarasi kwa kila hoja wanayokuja hatutaweza kufanikisha kufikisha umeme vijijini, huu ni udhaifu ambao unataka kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine cha mwisho wananchi tunaotoka maeneo ya mpakani tunayo advantage ya kufaidika na bidhaa zinazouzwa bei ya chini upande wa pili wa mpaka. Kwa mfano, sukari imepanda Tanzania lakini ukienda Zambia ipo chini, mafuta ya kula yamepanda huku ukienda Zambia yapo chini na vitu vya namna hiyo, lakini cha kushangaza sasa gharama hizi za mafuta ambazo zimepanda Mkuu wangu wa Mkoa yeye ameunda taskforce kupambana na wananchi wanaokwenda Zambia kuchukua vitu kwa bei nafuu wanasema hao ni walanguzi, sasa mimi nilitegemea angeunda taskforce kupambana na wafanyabiashara wasiowaaminifu ambao wanapandisha vitu ambavyo havihusiani hata na bei ya mafuta. Mimi niiombe Serikali itoe kauli kwa Wakuu wa Mikoa wote ambao maeneo yao yanapakana na nchi za Jirani, wananchi wana-advantage ya kuishi maeneo ya mpakani waruhusiwe kwenda kufuata bidhaa nje kwa bei nafuu, hawa siyo walanguzi! Mtu akienda akichukua kilo kumi kwa sababu anachukua kilo kumi au ishirini kwa sababu hataki kwenda kila siku kununua sukari, kwa hiyo anachukua nyingi ili haifadhi na anamchukulia na jirani yake, lakini sasa tukisema kila mtu anayekwenda kufuata vitu vya bei nafuu ni walanguzi hii tutakuwa hatuwatendei sawa wananchi wanaoishi mipakani. Naomba Mheshimiwa Waziri uliangalie kwa sababu Nishati ya Mafuta imepanda na imesababisha vitu vingi kupanda. Kwa hiyo, niombe hili suala ambalo jingine ambalo wananchi tunaoishi maeneo ya mpakani tunahitaji kuwa na hiyo advantage. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo Mheshimiwa Waziri mimi nitaunga mkono hoja pale nitakapopata maelezo ya kutosha kwa nini tunawapa kichwa hawa Wakandarasi na sababu zao ambazo hazina msingi za kutuambia kwamba vifaa vya REA vimepanda wakati havijapanda na vyote vinapatikana hapa nchini. Ahsante sana. (Makofi)