Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai pia namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutoa ruzuku kwenye mafuta, fedha zile ambazo amezitoa ambazo angalau zimeshusha kidogo bei ya mafuta hapa nchini tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Nishati pamoja na timu yake kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya ninawaomba wazidi kuongeza nguvu ili tuweze kuyaona manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia suala la gesi asilia. Mtwara Gas Plant ina jumla ya visima 11 ambavyo vinauwezo wa kuzalisha megawatt 22 za umeme kwa siku. Lakini kati ya visima hivyo visima Tisa ni vya muda mrefu ni vya kati ya 2006 na 2007 na life span ya mashine hizo ni miaka 10. Kwa hiyo, utaona kwamba muda wa mashine hizo umeshapita kiasi kwamba uzalishaji wa umeme umekuwa ni wa chini sana. Tunaomba Wizara ijipange kutafuta replacement ya vile visima Tisa ambavyo ni vya muda mrefu ambavyo pia vinaiingizia Serikali gharama kwa sababu ya matengenezo yasiyoisha kwa sababu muda wake pia umeshapita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nataka kupata commitment ya Serikali ni lini mradi wa megawatt 300 ambao unatakiwa kwenda kujengwa kule Mtwara utaanza? Nimeona kwenye hotuba ya Waziri imewekwa lakini hii si mara ya kwanza inawekwa, imewekwa muda mrefu sana kila wakati inawekwa lakini haitekelezwi. Kwa hiyo, tunaomba Waziri atakapokuja kuhitimisha atuambie ni lini hasa ujenzi wa megawatt 300 Mtwara utaenda kuanza kwasababu unafaida kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme wa Mtwara haujatulia, umeme unaofika Mtwara ni mdogo, pamoja na Mtwara tunazalisha gesi lakini umeme wetu unaoingia pale ni mdogo sana unakatika kila wakati. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri atuambie ujenzi halisi wa megawatt 300 utaanza lini Mtwara? Anapokuja kuhitimisha hotuba yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane pia na mzungumzaji aliyepita aliyezungumzia suala la REA katika maeneo yetu. Ni kweli kabisa Wakandarasi wa REA walipewa kazi ile mwaka jana kati ya Agosti na Septemba, kipindi kile mfumuko wa bei haukuwa mkubwa kama ulivyo sasa hivi, mfumuko umeanza karibuni, sasa wanakuja na kisingizio cha kwamba vifaa vimepanda bei, walikuwa wanafanya nini kipindi chote ambacho kimepita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Jimbo la Newala Vijijini kwa mfano, ambako mkandarasi anayeitwa Central Electrical International Limited amepewa kazi ya kuweka umeme katika Jimbo la Newala Vijijini, Newala Mjini, Tandahimba, Newala lakini Mkandarasi yule kwakweli tumechoka kwa sababu ufanyaji wake wa kazi haueleweki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Jimbo la Newala Vijijini, Vijiji 107 ndivyo ambavyo vipo kwenye Jimbo lile lakini ni vijiji 33 tu ndivyo vyenye umeme, Mkandarasi amepewa scope ya kazi anaifahamu lakini ninavyoongea sasa hivi amefika Kata mbili tu ambazo zina vijiji 11 hali ambayo inatia wasiwasi kwamba je, ikifika Desemba 2022 kweli atakuwa amemaliza vijiji vyote 74 ambavyo havina umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri nakuomba Kaka yangu msimamie Mkandarasi aliyepewa kazi Mtwara, Tandahimba, Nanyamba na Newala afanye kazi kwa juhudi ikiwezekana usiku na mchana, kwa sababu watu tupo gizani, lakini umeme huu unamanufaa makubwa sana kama utawafikia wananchi wale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wanashindwa kujiajiri kwa sababu hawana umeme, kungekuwa na umeme wangeuza ice-cream, wangechomea ma-gate wangefanya kazi mbalimbali lakini wanashindwa kwa sababu umeme haupo. Nasi tumeahidi katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwamba tutaongeza ajira zipatazo zaidi ya 8,000 kufikia 2025 lakini ajira hizi zingine zinatokana na sekta binafasi ikiwemo hii ya umeme kwamba vijana wangeweza kujiajiri wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba sana Waziri wetu asimamie umeme ufike kwenye vijiji kupitia REA ili wananchi wale nao waweze kunufaika waone matunda yanayotokana na kazi ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo maeneo niliyotaja ambayo yapo gizani yanapakana sana na nchi jirani nchi ambayo hali yake tunaifahamu, nimeshaongea hapa umeme huu si luxury umeme ni ulinzi ukiondoa suala zima la kazi lakini umeme ni ulinzi utatulinda kwa kuwepo kwake. Kwa hiyo, tunavyofanya hawa Wakandarasi waliopewa kazi wanaenda polepole wanahatarisha usalama wa raia wa maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mwanzo umeme unaofika maeneo ya Mtwara na Lindi ni mdogo sana, kule tunafahamu kabisa kwamba ndiko gesi asilia inakotoka kwa wingi kutoka kule Msimbati, Songosongo gesi hii inaenda kuchakatwa Kinyerezi inarudishwa kule. Kwa hiyo, umeme taunaopata ni mdogo sana. Tulitaraji miradi hii wananchi wanaotoka katika maeneo yale wai-own wao wenyewe kwa maana ya kwamba waone manufaa yanawafikia moja kwa moja. Tuliambiwa kwamba watapata umeme wa majumbani lakini kiasi ambacho kimefika cha matumizi ya umeme majumbani ni kidogo sana, ni kidogo mno na sijui mradi ule umeishia wapi kwa sababu ulikuja mara moja tumeona kimya mpaka leo. Naomba sana Serikali kupitia Waziri mjipange muhakikishe umeme huu unawafikia wananchi wa Lindi na Mtwara, waone manufaa ili wawe walinzi wazuri wa miradi hii kwa sababu inatoka kule kwao watusaidie kulinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni gridi yetu ya Taifa umeme huu ukienda unaishia Tunduru Gridi ya Taifa kule ipo Tunduru, kwa hiyo, umeme unaofika Masasi kupitia gridi ya Taifa hauna nguvu. Niombe sana Serikali ione uwezekano wa kujenga sub-station maeneo yale ya Masasi ili wananchi waweze kupata umeme wa uhakika kwa sababu kuna kukatika katika sana kwa umeme kutokana na umbali unakotoka umeme hadi kuwafikia walaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja lakini Mheshimiwa Waziri anapokuja aje na majibu ambayo nimeyaomba niyasikie anatujibuje. Ahsante. (Makofi)