Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie Wizara hii muhimu ya Nishati. Nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri January Makamba, Mheshimiwa Naibu Waziri Stephen Byabato na watumishi wote wa Wizara, viongozi na watumishi wa taasisi mbalimbali chini ya Wizara, REA na nyinginezo kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru pia kabla sijasahau, jambo la juzi la kutuletea wataalam hapa Bungeni wa TANESCO, REA na mashirika mengine lilikuwa ni jambo muhimu sana na zuri sana. Ahsanteni sana. Tumezungumza na wale watu, wametusaidia matatizo yetu kwenye majimbo na kasi imeongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nizungumzie umeme na nizungumzie umeme Bukoba Vijijini. Kama walivyosema wenzangu umeme ni suala la maendeleo siyo suala la anasa, ni tija ya maendeleo, ni uchumi, umeme ni siasa kwa sisi ambao tuko kwenye siasa, unatusaidia mambo mengi yanakwenda, yanasonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pale Bukoba nishukuru kwanza kwamba kasi ya maendeleo ya umeme ni kubwa ni nzuri lakini kuna tatizo kubwa sana. Bukoba na Kagera nzima kama walivyoongea wengine hapa wachache, umeme unazimika sana, ukiamka asubuhi ukakuta umeme unawaka, utakuwa na bahati kama utafika saa nne haujazimika. Saa sita utazimika tena, kwa siku unazimika mara nane, mara 10 au mara 20. Kwa hiyo, inakuwa ni matatizo makubwa na kama una kiwanda kidogo hutaona tija yoyote, itakuwa ni hasara kubwa kuwa na umeme kwenye kiwanda chako. Kama una taa zako zitaungua, kama ni fridge itaungua na vitu vingine vya umeme, unakuwa huna tija na umeme huo kwa sababu umeme unazimikazimika mara nyingi sana kwa kutwa moja usiku na mchana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu inafahamika, sababu ni kwamba umeme wa Bukoba unatoka Uganda tunaununua nchi jirani ya Uganda. Uganda wenyewe wana shida ya umeme, wana mgao. Kwa hiyo, wanapoleta umeme Bukoba ni umeme kidogo kuliko mahitaji yaliyopo na Kagera kwa ujumla. Kwa hiyo, wakipunguza kidogo, basi umeme unazimika kwenye maeneo yetu. Sasa mfumo, ile gridi ya Taifa imekaribia kufika kwenye maungio kule Bukoba, umeshaingia mkoani nafikiri uko sehemu za Muleba au nyuma kidogo pale. Naomba Wizara ifanye kazi kubwa ya kuongeza kasi kusudi mfumo huu, gridi ya Taifa iunganishwe na Mkoa wa Kagera tuondokane na umeme wa kutoka nchi jirani ambao hautoshi, matokeo yake ni kuzimika umeme mara kwa mara, hivyo, inakuwa shida kubwa sana kwa watumiaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nashukuru kwanza, kwamba kasi kama nilivyosema ya kufunga umeme kwenye vijiji mbalimbali ipo. Pale kwangu kuna vijiji vingi ambavyo havijapata umeme, Kijiji cha Buzi, Kijiji cha Buguluka, Kijiji cha Musira, Kijiji cha Butakya, Bituntu, Sheshe, Lukoma na vingine vingi, lakini kasi ipo, machimbo yamechimbwa na tunaanza kuwa na matumaini kwamba umeme utafungwa, nashukuru kwa hilo. Hata hivyo, tusifikiri kwamba kwa kufunga umeme kwenye vijiji hivi na vile ambavyo vimeshafungwa tayari, tumepiga hatua kubwa sana, bado kabisa, bado kabisa, vitongoji vingi vingi havina umeme, watu wengi sana hawana umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta kijiji kizima nitakusomea mifano hapa michacho ya kata mbili. Kuna Kata moja inaitwa Kyamulaile. Kata ya Kyamulaile ina vijiji vinne, kijiji Omkihisi kina kaya 490 ni kaya 10 tu zenye umeme. Kijiji cha Kyamulaile yenyewe ina kaya 863, kaya zenye umeme ni 38. Nina Kijiji Mashule, kina kaya 1,085, kaya zenye umeme ni sifuri, hata moja yenye umeme hakuna, lakini kwenye mtandao wa TANESCO na REA wanahesabu na hiki kijiji kina umeme wamekimaliza. Kaya yenye umeme sifuri, walifunga umeme kwenye chanzo cha maji pale wakaondoka. Wananchi wote, kaya zote hazina umeme. Kata ya Nyakibimbili, Kijiji cha Bundasa kina kaya 610, kaya zenye umeme 19. Kijiji cha Bugengele, tuna kaya 368, kaya zenye umeme 28. Kijiji cha Kitaya kuna kaya 330, zenye umeme kaya 27.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo inaonesha kazi ya kufunga umeme bado ni kubwa sana, tunahitaji msukumo mkubwa wa REA wa TANESCO kuongeza kasi. Tusifikiri kwamba kufunga vijiji vyote kama tunavyoambiwa Desemba walikuwa wanafunga vijiji vyote kazi imeisha, kazi bado ni mbichi kabisa, ni kubwa. Mbaya zaidi kule Bukoba wanapokwenda kufunga umeme kwenye kijiji kingine au kitongoji fulani wanapita juu ya nyumba za watu. Juu kuna waya za umeme, chini nyumba hazina umeme, sasa nafikiri kwamba ni rahisi ukishafika pale wateremshie watu umeme ambao wamepitiwa na zile waya ili nao wapate matunda ya kupitishiwa pale waya hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia unafyeka mazao yao, sisi kule mazao yetu ni kahawa na migomba, wanafyeka, yote wanatoa, mtu ana nusu heka, yote inafyekwa, lakini hapati umeme. Sasa unashangaa huyu mtu kwa nini wanamuadhibu na umeme hawampi. Kwa hiyo, nafikiri kwamba ingekuwa bora sana hawa nao wafikishiwe huduma ya umeme kama ambavyo wanapelekewa wale wengine ambao wanapitishiwa pale juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)