Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa hii. Kigoma tuna kilio cha umeme tangu nchi yetu ipate uhuru miaka 60 iliyopita, Kigoma na Katavi hatujaunganishwa kwenye grid ya Taifa. Viongozi wa Taifa wa ngazi za Kitaifa wamekuwa wakifanya ziara mbalimbali katika Mikoa ya Katavi na Kigoma na kutoa ahadi ya kuunganisha mikoa hiyo katika grid ya Taifa kwa muda mrefu, lakini mpaka sasa hivi miradi hiyo haijakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri mwaka 2019 tarehe 25 Machi, 2019, Serikali iliahidi ifikapo mwezi Aprili, 2020 Kigoma itakuwa imeungwa na umeme wa grid ya Taifa na ilisema tayari bilioni 87 zipo tayari kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo, leo tuko mwaka 2022 mradi huo haujakamilika, hizo bilioni 87 zilienda wapi? Haitoshi tu, mwaka jana tarehe 26 Novemba, 2021, Serikali ilitangaza kwamba itaunganisha umeme wa grid ya Taifa kwa Mikoa ya Katavi na Kigoma kwa mwaka 2022, wananchi wa Kigoma na Katavi wanasubiria kwamba je, ni kweli ifikapo Desemba 31 mwaka huu mikoa hiyo itakuwa imepata umeme wa grid ya Taifa? Tuna kilio cha muda mrefu, umeme ndiyo kila kitu, huwezi kupata uchumi wa viwanda bila umeme, umaskini wa Mkoa wa Kigoma na Katavi umesababishwa na ukosefu wa miundombinu ikiwa ni pamoja na umeme. Mikoa hii inazalisha sana, lakini imekosa umeme, kwa hiyo haiwezi kuvutia wawekezaji wa viwanda pasipo na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Waziri kwenye vipaumbele vyake 12 ambavyo amevileta hapa Bungeni, amesema kipaumbele namba moja ni kutekeleza miradi mbalimbali ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji umeme ikiwepo kupeleka umeme wa grid ya Taifa kwenye Mikoa ya Katavi na Kigoma. Najiuliza nimeona vyanzo vya Kigoma kuunganishwa na umeme wa grid wa Taifa ni kutoka Nyakanazi kuja Kigoma, kutoka Urambo kuja Kigoma, kutoka Sumbawanga kwenda Kigoma na maporomoko ya Mto Malagarasi. Inanichanganya kwamba hivi vyanzo vyote vinatokea kwa wakati mmoja? Naomba Waziri atakapokuja kutoa hitimisho lake awaeleze wananchi wa Kigoma, katika hizo njia zote nne ni njia ipi hasa ambayo ameipa kipaumbele cha haraka sana ifikapo Desemba tuwe tumepata umeme wa grid ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa tunatakiwa tujiulize gharama ya kuendesha umeme ule wa generator Kigoma kila mwezi, Shirika linapata hasara ya zaidi ya milioni 700, ukizidisha kwa mwaka Shirika la TANESCO linapata hasara zaidi ya bilioni 8.4, kwa miaka kumi ni bilioni 84 kulikoni? Ukiangalia gharama ya kuunganisha umeme wa grid ya Taifa kutoka kituo cha Urambo kwenda Kigoma ni bilioni 69, kwa nini huu mradi hautekelezeki wakati Taifa linaendelea kupata hasara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna haja ya kuangalia, kutakuwepo na watu wanaofaidika na ununuzi wa mafuta, kutakuwepo na maslahi ya supplier anaye-supply mafuta ya kuendesha hii mitambo ya generator. Tunaomba sana wananchi wa Kigoma na Katavi wanalalamika, wana maombi makubwa sana, wana imani kubwa sana na Mheshimiwa Waziri, ana muda mfupi tu lakini ameweka kipaumbele kwa mikoa yetu. Nilikuwa nimejiandaa kukamata shilingi ya Waziri, tunasubiri, endapo itafika mwaka kesho, mikoa yetu haijaunganishwa na grid ya Taifa tutakuja kukamata shilingi ya Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo, ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante. (Makofi)