Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini pia nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuwa hapa tukiwa salama. Kwa namna ya pekee kabisa naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoendelea kufanya, hususan katika eneo hili la Wizara ya Nishati, hasa katika kuhakikisha kwamba, miundombinu inaendelea kuimarishwa, lakini pia kupeleka fedha katika miradi ya kimkakati tuliyokwishaianza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Waziri wa Nishati pamoja na Naibu wake, Mheshimiwa Makamba na Mheshimiwa Stephen, lakini pia Katibu Mkuu pamoja na Naibu Katibu Mkuu, Wakurugenzi watendaji wote ambao wako chini ya Wizara hii, Wenyeviti wa Bodi pamoja na watumishi wote ambao wako katika Wizara hii. Kwa kuwa, sio rahisi kumtaja kila mmoja, basi niseme tu kwamba, nawapongeza na hasa ikizingatiwa kwamba, Wizara hii wafanyakazi wengi ni wahandisi wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema kwamba, ulimi ni kitu ambacho wakati mwingine kinaponza na ukiangalia Wizara hii tulivyoichukulia wakati inapokea madaraka, yaani wakati Mawaziri hawa wapya wanapokea madaraka, ilikuwa kidogo tuna hali ya wasiwasi itakuwaje? Mambo yataendaje? Kwa hiyo, kukawa kunatokea maneno ya hapa na pale, lakini kusema kweli utulivu ulioendelea na pia viongozi hawa jinsi ambavyo wameendelea kupokea wajibu wao na kuutendea haki, tunaona sasa haya mabadiliko makubwa ambayo yanaendelea. Vilevile tunaona hata Waheshimiwa Wabunge ambao walikuwa wakali sana kwa kipindi cha nyuma, sasa wanaiunga mkono bajeti ya Wizara hii bila kusita na wala sio kwa unafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru kwa semina mbalimbali zilizotolewa kwa ajili ya kuelimisha zaidi. Semina hizi zilikuwa na lengo la kujenga uelewa zaidi na sio kwa ajili ya kuwapofusha Wabunge, Wabunge wa Bunge hili ni Wabunge makini sana, huwezi kuwapofusha. Ni watu ambao wakisimamia jambo lao wamelisimamia, lakini wakielewa watakuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kidogo kuhusiana na Bwawa la Mwalimu Nyerere. Napenda kuipongeza sana Wizara kwa kazi hii na hapa namkumbuka Mwenyekiti wake wa Bodi ambaye katika Shirika la TANESCO ambaye amekuwa ni muasisi wa masuala ya Matokeo Makubwa Sasa. Hapo ni kwamba, unachagua jambo moja zito na unalifanyia kazi kwa nguvu zako zote ili liweze kuzaa matunda mengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hili kwa mtu yeyote ambaye ni dereva mzuri anapoachiwa gari lililokuwa lime-park mahali au linaendelea kutembea, hawezi kuchukua tu akaliendesha bila kuangalia lina maji, lina oil, lina kitu gani ili liweze kwenda vizuri. Hilo ndilo lililofanyika, baada ya mabadiliko ya kiuongozi kulikuwa na muda kidogo wa kutathmini mradi huu uende vipi, changamoto ni zipi na mahali labda pengine tuboreshe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mradi mkubwa kama wa Mwalimu Nyerere, jamani ule mradi tusiuchukulie sawa na kujenga nyumba yako au kufanya tu ni mradi wa kawaida ambao unaufikiria, unahitaji umakini wa hali ya juu. Mabadiiliklo yoyote ambayo yanafanyika au marekebisho yoyote yanayofanyika hapo si kwamba, wale wa mwanzo hawakuwa na maana au hawa wa mbele ndio wanajua zaidi, ni katika kuufanya mradi huu ambao unatumia trilioni za Watanzania zaidi ya sita, uweze kuwa imara, uweze kuwa utakaokuwa na tija na utakaoweza kudumu kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkumbuke kwamba, hata zile mashine nyingine zinaenda kuwekwa chini huko kwenye maji. Kwa hiyo, lazima vitu vingine viwekwe vizuri kiasi kwamba, hata zikishafungwa zile mashine kama turbines hutegemei kwamba, kesho tena utaanza kusema kwamba, ngoja niangalie, sijui tuangalie ilikaa vibaya, sijui kitu gani, lazima uende kwa mahesabu yote na usije ukapotea. Kwa hiyo, nawapongeza sana na nazidi kusisitiza waendelee kuwa watu makini, pale ambapo wanaona kuna dosari wasisite kusema na kufanyia kazi hata kama itatugharimu kuongeza muda kidogo au pesa kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwamba, wamefanya jitihada ya kupeleka wataalam wetu kwenda kufuatilia utengenezaji wa zile mashine umba na turbines ambazo ziko kule, hilo ni jambo jema sana. Niseme tu kwamba, ndugu zetu wote ambao tuko humu na walioko nje sisi Kamati yenu ya Nishati na Madini tuko makini, ndio maana hatupigi kelele nje, tunapigia kelele ndani. Tunapokuwa kule kwenye Kamati kule ni patashika nguo kuchanika, kila jambo lazima tulione na tunatembelea hiyo miradi na tumetembelea, tumeona Mradi wa Mwalimu Nyerere unaenda vizuri. Sasa hivi power house yaani nyumba ya umeme inajengwa inaendelea vizuri, hizo mashine zinaendelea kutengenezwa, sehemu ya station ya kituo cha umeme inatengenezwa, line ya umeme kutoka kule kwa Bwawa la Mwalimu Nyerere mpaka Chalinze na yenyewe inajengwa, lakini pia tumesisitiza kwamba, hata tukizalisha huu umeme mega wati 2,115 kama hakuna viungo vya kupeleka umeme kwa hawa watumiaji itakuwa ni hakuna maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jinsi ambavyo mfumo huu unafanya kazi hakuna tofauti na mwili wa binadamu. Unaweza ukawa na kichwa, huna shingo, wewe ni hopeless, unaweza ukawa na shingo na mikono huna kichwa, haisaidii. Kwa hiyo, ni lazima mfumo mzima uangaliwe. Nashukuru sana bajeti ya safari hii imeendelea kuwa vilevile nzuri, lakini kubwa zaidi ni kuhakikisha kwamba, sasa ile mifumo mingine ya usambazaji umeme, usafirishaji umeme wa KV 400 na yenyewe inakamilika kwa pamoja, iendelee kufanyiwa kwazi kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimefurahi ni kuona ni kwa namna gani tulipokuwa tunalalamika umeme unakatikakatika, Serikali imetoa fedha ya kutosha kwa ajili ya kufanya matengenezo na marekebisho muhimu ili umeme uendelee kuwafikia wananchi. Sasa hivi naomba Waheshimiwa Wabunge, ukisema umeme unakatikakatika, malizia kusema ni eneo gani ili tukashughulikie, kwa sababu, ukisema kwa ujumla yawezekana utakuwa hutendi haki, sema kwamba, eneo fulani ili liende likashughulikiwe na mambo yazidi kuwa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo mwaka huu ni mwaka wetu wa sensa. Mwaka wa sensa tutaangalia takwimu za aina mbalimbali, moja ya takwimu itakuwa ni namna gani Watanzania wameweza kunufaika katika nishati za aina mbalimbali. Kwa hiyo, niwaombe, wenzetu watu wa REA ambao wamefanya kazi kubwa sana waendelee kuhakikisha katika hii miezi miwili tuliyonayo umeme usambazwe kwenye majumba ya watu ili itakapofikia kujua ni watu wangapi wana umeme, basi idadi yetu iongezeke na izidi kuonesha nchi hii ni nchi yenye nguvu na yenye dhamira katika kuleta maendeleo ya wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambalo napenda nisisitize kuhusiana na hizi mita janja ambazo tutaanza kuzitumia. Niwaombe sana kwamba, mita janja kimsingi ni ghali kidogo na kama ni ghali hatutegemei wote watapewa kwa mara moja. Kwa hiyo, nafikiria kwamba, mita janja waanze kupata wale ambao watakuwa na uwezo wao wa kuchangia, kwa sababu zile zitakuwa na bei kubwa zaidi pengine takribani mara tatu ya mita za kawaida. Sisi wa maeneo ya vijijini acha tupate hata kama ni mita hizi za kawaida, lakini la msingi tupate umeme kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi kwenye upande wa mafuta; napenda kuipongeza sana Wizara kwa jinsi ambavyo imechukua hatua ya kujaribu kupoza makali ya mafuta. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ile shilingi bilioni 100 ambayo ameitoa kwa ajili ya kusaidia marekebisho hayo. Sasa naona kuna mpishano kidogo, wafanyabisahara wanasema kwamba, ile bei ilivyowekwa sasa mafuta yamepungua wao wanapata hasara kwa sababu, walinunua mafuta mengi. Wafanyabiashara tusameheni, acheni ujanja, wakati ule bei ilipotangazwa ikaongezeka mlikuwa pia na madumu mengi mmeyahifadhi, mbona hamkusema kwamba, ngojeni kwanza tuuze kwa bei ndogo haya madumu mengi tuliyoyahifadhi, halafu badaye tutapandisha bei? Acheni ujanja, (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema hivi hata kama hiyo bahati mbaya ipo, ndio hivyohivyo hata wananchi iliwakuta bahati mbaya kupanda bei kubwa sana. Sasa hivi na ninyi bebeni mzigo kidogo, lakini mwisho wa yote tutaenda wote vizuri. Kwa hiyo, ninachosema ni kwamba, kimsingi nia ni njema, kusiwe huyu anasema hili, anasema hili, huko ni kuyumbisha, hakuna suala la kuyumbisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niombe kuendelea kusisitiza, najua pengine sitapata tena nafasi ya kuchangia. Bajeti inayokuja ya Serikali ipunguze kama ni kodi wapi kokote itakakojua, lakini katika miradi ya umeme, maji na afya, katika maeneo yale muhimu ambayo tunapeleka fedha za tozo, jamani acha tujifunge mkanda. Kwenye corona tulisema tusijifungie tukavuka na hivyohivyo kwenye masuala haya ya kupanda bei mafuta na nini acha tujifunge mkanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule vijijini tunahitaji maendeleo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya kwa mchango wako.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)