Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Nishati, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Spika, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Nishati kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendelo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/26 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati kwa kuendelea kutekeleza kwa ufanisi mkubwa miradi ya umeme ikiwemo miradi ya kusambaza umeme vijijini (REA) na ujenzi mkubwa wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) litakalozalisha umeme wa megawati 2,115. Miradi hii ya kusambaza umeme vijijini imeiweka Tanzania katika nafasi ya juu Afrika na imeweza kuchochea kasi ya ukuaji wa viwanda na uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto za vita ya Ukraine na Urusi na kupelekea kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli, napongeza Serikali kushirikisha Wizara ya Nishati, Wizara ya Fedha, EWURA na wadau wengine kuweka mkakati wa kuanzisha Mfuko wa Kudhibiti Mabadiliko ya Bei za Mafuta (Fuel Price Stabilization Fund) ili kukabiliana na kupanda kwa bei za mafuta. Pia Serikali inachukua hatua stahiki za kuanzisha Hifadhi ya Taifa ya Kimkakati ya Mafuta (Strategic Petroleum Reserve-SPR) ili kukabiliana na dharura na kuimarisha usalama na uhakika wa mafuta kwa Taifa. Mkakati huu uende sambamba na uanzishaji wa bandari kavu Mbeya na ujenzi wa matenki makubwa kuhifadhi mafuta kwa nchi jirani za Zambia, DR Congo, Malawi na pia kwa matumizi ya Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na REA kuendelea kutekeleza miradi ya kupeleka umeme kwenye makao makuu katika vijiji vyote vya Jimbo la Mbeya Vijijini bado kuna uhitaji mkubwa wa umeme kufika kwenye vitongoji vyote. Napendekeza kuendelea kwa kasi utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa REA III (REA III, Round II) na kufikisha umeme katika vijiji vyote vilivyobakia na pia kuendelea na utekelezaji wa Mradi wa Ujazilizi (Densification). Napendekeza utekelezaji utoe kipaumbele kwa kata za Itawa na Shizuvi ambavyo hakuna kijiji kilichowashiwa umeme, na pia kwenye vitongoji vinavyolizunguka Jiji la Mbeya ikiwemo Mina na Lusungo Kata ya Iwindi, Kijiji cha Shongo, Kijiji cha Wambishe kwenye shule zote ikiwemo Shule ya Sekondari Iwiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vijiji vilivyopatiwa umeme kwa kiasi kikubwa imechochea ukuaji wa viwanda hasusani viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo. Nashauri TANESCO iongeze speed ya kuunganisha umeme na pia kushughulikia maombi ya wateja wengi wanaosubiri umeme ikichukuliwa hii ni fursa pia kwa TANESCO kuongeza mapato ya shirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na vyanzo vya sasa, napendekeza Serikali itekeleze miradi ya vyanzo vingine kama vile vyanzo vya Jotoardhi, Umeme wa Jua, Upepo na Makaa ya Mawe ili nchi yetu iendane na mahitaji makubwa ya umeme kwa hapa Tanzania na hata nchi zingine za Afrika. Ni muda mrefu sasa, TANESCO kupitia Kampuni tanzu ya Uendelezaji wa Jotoardhi nchini (TGDC) inaanze uzalishaji katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo eneo la Ziwa Ngozi, Kata za Ijombe na Bonde la Songwe Mkoani Mbeya ambapo ndipo yalipo makutano ya Bonde la Ufa la upande wa Mashariki na lile la Magharibi.

Napendekeza Serikali iharakishe utekelezaji wa miradi hii ya Jotoardhi na ule wa Makaa ya Mawe wa Mchuchuma na Kiwira ili tuweza kuzalisha umeme zaidi kwa mahitaji ya ndani na nchi za nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.