Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Nishati Ndugu January Makamba na Naibu wake Engineer Stephen Byabato pamoja na jopo la wataalamu wa Wizara kwa kazi kubwa wanazofanya kupeleka umeme na nishati nyingine muhimu kwa wananchi wetu hapa nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utahusu umuhimu wa kupeleka huduma ya gesi asilia katika Jimbo la Moshi Vijijini na huduma ya umeme katika maeneo ambayo hayajaunganishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya bajeti Waziri ameeleza kwamba kuna mradi wa gesi asilia utakaojengwa kupeleka huduma hii Mombasa nchini Kenya. Katika hotuba yake, ameeleza kuwa mikoa ya Pwani, Tanga Kilimanjaro na Arusha itanufaika na mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Moshi Vijijini limepakana na Mlima Kilimanjaro, wananchi wengi hutegemea nishati ya kuni kutoka katika misitu ya Mlima Kilimanjaro na maeneo mengine ya jirani. Wanasayansi wamesema kwamba matumizi ya kuni kwa kiasi kikubwa yamesababisha uharibifu wa mazingira na nishati mbadala inahitajika kukabiliana na changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ujio tarajiwa wa mradi wa gesi asilia Mkoani Kilimanjaro, ninaishauri Serikali ianze kwa kusambaza miundombinu ya gesi hii katika vijiji vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro ili kuunusuru mlima na ukataji wa nishati ya kuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali kupeleka umeme vijijini, bado wananchi wengi wa Jimbo la Moshi Vijijini hawajapatiwa nishati ya umeme. Hivyo basi ninaiomba Wizara ya Nishati isaidie kutatua changamoto za nishati ya umeme katika jimbo langu la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yenye changamoto ya umeme Jimbo la Moshi Vijijini ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kimochi, Kitongoji cha Kiwalaa kilichopo Kijiji cha Sango, Kitongoji cha Iryaroho kilichopo katika Kijiji cha Mowo na Kitongoji cha Maryaseli katika Kijiji cha Lyakombila havina umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali ikamilishe ujenzi wa miundombinu ya umeme katika maeneo niliyotaja hapo juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Okaoni, vijiji vya Sisamaro, Omarini na Mkomilo vinahitaji kuunganishwa japo baadhi ya maeneo nguzo zimepita ila bado kuunganishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Kindi, Kijiji cha Chekereni Weruweru, Vitongoji vya Miembeni, na Kisiwani havina umeme kabisa, ninaiomba Serikali ipeleke huduma kwenye vijiji hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kayta ya Kibosho Kirima, Mbunge ametokea kata hii. Kama nilivyoomba mwaka jana katika Kijiji cha Boro kwenye vitongoji vya Boro Kati na Boro Juu (anakotokea Mbunge), voltage za umeme ni kidogo sana na hupelekea kushindwa kuendesha vifaa vya ndani kama friji na vyombo mbalimbali vya ndani. Mashine za welding (kwenye vitongoji hivi) na pump ya kuvuta maji katika shule ya sekondari Masoka hushindwa kufanya kazi kutokana na umeme kidogo. Wajasiriamali wameshindwa kuweka mashine za kusaga unga, mashine za kutengeneza matofali na miradi mingine midogo inayohitaji umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafunzi wa bweni wa sekondari ya Masoka hushindwa kupata huduma ya umeme ili wajisomee usiku kutokana na umeme kidogo. Umeme huwaka kuanzia saa tano usiku. Ninaiomba Wizara isaidie kutatua changamoto hii, kwani pamoja na maombi yangu mwaka jana, bado Wizara haijatusaidia kutatua changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kibosho Mashariki, kama nilivyoomba kwenye bajeti ya mwaka jana inahitaji huduma katika Kijiji cha Sungu Vitongoji vya Kyareni na Nkoitiko havijaunganishwa; katika Kijiji cha Singa, Kitongoji cha Singa Juu hakijaunganishwa; na katika Kijiji cha Mweka, kitongoji cha Mweka Juu na Omi havijaunganishwa. Ninaiomba Serikali ipeleke huduma kwenye vijiji na vitongoji vilivyotajwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Kibosho Kati, kama nilivyoomba kwenye bajeti ya mwaka jana, Vijiji vya Uri na Otaruni umeme una nguvu kidogo (low voltage) na kunahitajika transfoma. Katika Kijiji cha Otaruni, Kitongoji cha Ngoroshi hakuna umeme na tunaomba wananchi wapatiwe huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoomba kwenye bajeti ya mwaka jana, katika Kata ya Uru Mashariki, Kijiji cha Materuni, Kitongoji cha Wondo hakijaunganishwa, ninaiomba Serikali ipeleke huduma kwenye kitongoji hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Mbokomu kama nilivyoomba kwenye bajeti ya mwaka jana, Kitongoji cha Mmbede Kyaroni, Tema na Masanga na baadhi ya maeneo ya Korini Kati havijaunganishwa, pia ninaiomba Serikali ipeleke huduma kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoomba kwenye bajeti ya mwaka jana, katika Kata ya Mabogini sehemu ambazo hazijapata umeme hadi sasa ni Vitongoji vya Sanya "Line A" na Mjohoroni vilivyopo katika kijiji cha Mabogini; Kitongoji cha Uru - katika Kijiji cha Muungano; katika Kijiji cha Maendeleo, Vitongoji vya Mshikamano na Uarushani; Mgungani - katika Kijiji cha Mtakuja, na katika Kijiji cha Mserekia hakuna umeme katika Vitongoji vya Mbeya kubwa, Mbeya ndogo, Remit, Mkwajuni, na Mafuriko. Kijiji cha Mji mpya, Kitongoji cha Utamaduni hakijaunganishwa. Ninaiomba Serikali ipeleke huduma kwenye maeneo yaliyotajwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.