Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa leo nianze mchango wangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendeleza miradi mikubwa iliyopo kwenye sekta ya nishati. Nikitaja michache ni pamoja na Mradi wa Umeme wa Maji wa Julius Nyerere - JNHPP MW 2115 ambao sasa upo 60%; Mradi wa Gesi Mtwara na Miradi ya REA Awamu ya tatu Mzunguko wa Pili ambao vijijini vyote nchini vitapata umeme, pia tunaenda kuanza umeme jazilishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ikitekelezwa kikamilifu tutakuwa na umeme wa kutosha kwa mahitaji yetu ya sasa na kuwa na ziada itakayotusaidia kwenye uchumi wa viwanda. Utekelezaji wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ukikamilika utasaidia sana uchumi wa wananchi wetu kuanzisha viwanda vidogo vidogo na vya kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali iharakishe utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika sekta hii ya nishati ili kuchochea maendeleo ya wananchi na nchi kwa ujumla. Kwa sasa mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili utekelezaji upo chini ya 20% na kwenye Jimbo langu la Hanang kati ya vijiji 42 hakuna hata kimoja ambacho umeme umewashwa na mkataba bado miezi sita tu. Wananchi wangu wa Hanang wanasubiri mradi huu kwa hamu kubwa, naomba Wizara iwabane wakandarasi ili utekelezaji ufanyike kwa kasi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Hanang ni kati ya maeneo katika nchi hii ambapo umeme unakatika sana, kwa wastani tunapata umeme kwa 50% kwa sababu ya ukatikaji wa mara kwa mara. Niliiomba Wizara ya Nishati itusaidie kutatua kero hii kwa kujengwa kwa kituo cha kupooza umeme Hanang ili isaidie Wilaya yetu ya Hanang na maeneo ya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Naibu Waziri wa Nishati Mheshimiwa Byabato akijibu swali langu la msingi hapa Bungeni aliahidi kuwa kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023 watatenga shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya kujenga kituo cha kupooza umeme eneo la Mogitu-Hanang lakini kwenye bajeti hili halionekani. Naomba sana ahadi hii iliyotolewa hapa Bungeni itekelezwe ili isionekane Wanahanang wamedanganywa kupitia Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naunga mkono hoja.