Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara ya Fedha na Mipango kwa bajeti hii ya mwaka 2022/2023. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nimpongeze mtani wangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba - Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri - Mheshimiwa Hassan Chande, Katibu Mkuu na timu nzima kwa kazi kubwa wanayofanya katika Wizara yetu ya Fedha na Mipango, lakini pia kwa ushirikiano mkubwa sana katika Kamati yetu ya Bunge ya Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba nimpongeze Mheshimiwa Makamu Mwenyekiti kwa kusoma taarifa vizuri, lakini na Wajumbe wa Kamati kwa ushirikiano mkubwa sana sana wanaonipa katika kuongoza Kamati yetu ya Bunge ya Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie katika maeneo yafuatayo; eneo la kwanza ni eneo la utendaji kazi kwa TRA. Niipongeze TRA kwa kazi nzuri, mwaka 2019/2020 tulikusanya wastani wa shilingi trilioni 1.5 kwa mwezi, lakini 2020/2021 tuna wastani wa shilingi trilioni 1.89 ni kazi kubwa tunayofanya. Tunawapongeza sana wenzetu hawa wa TRA pamoja na changamoto zote walizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili kuboresha ukusanyaji huu wa mapato ya TRA kuna mambo kadhaa ambayo nitayashauri; la kwanza, ni kuimarisha Block Management System; hili ni eneo ambalo wafanyakazi wa TRA hutembelea wafanyabiashara katika maeneo mbalimbali katika nchi yetu na katika eneo hili kuna mambo mawili; jambo la kwanza, ni kuwabaini wafanyabiashara wapya ambao bado hawajaingia kwenye mfumo wa kodi na hili likifanikiwa basi tutakuwa tumepanua wigo wa walipakodi katika Taifa letu na hatimaye kuongeza mapato ya TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye eneo hili kuna wafanyabiashara wengi sana wadogo na wa kati ambao bado hawapo kwenye mfumo na ninaamini TRA wakati huu imeajiri sasa wafanyakazi wa kutosha, hii itasaidia sana kuwabaini wafanyabiashara wa kati na wadogo ambao pia hawa hawana access za mikopo katika benki zetu. Kwa hiyo, niwaombe sana Wizara ya Fedha iwabaini hao wafanyabiashara wa kati na wadogo na pia iwajengee mazingira mazuri ya kupata mitaji katika benki zetu za biashara, kwa maana ya kupata mikopo yenye masharti nafuu na riba nafuu ili kubaini wanaolipa kodi katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili katika hii Block Management ni kutoa elimu kwa wafanyabiashara ambao tayari wamesajiliwa. Tukitoa elimu ya kutosha kwa walipa kodi wetu itaongeza voluntary tax compliance, itaongeza umahiri wa kulipa kodi, lakini bila kutumia gharama kubwa kwa maana kwamba ulipaji wa kodi wa hiyari. Kwa hiyo, niombe sana Wizara ya Fedha iwezeshe TRA katika eneo hili ili waweze kutoa elimu ya kutosha na hatimaye kupata kodi katika maeneo yetu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni kufanya marejeo katika mikataba ya kutotoza kodi mara mbili yaani Double Taxation Agreement. Nchi yetu iliridhia mikataba na nchi mbalimbali katika kutotoza kodi mara mbili na nchi hizo ni kama ifuatavyo na naomba noisome; Mkataba wa kwanza ni Tanzania na Zambia mwaka 1968; Tanzania na Italy mwaka 1973; Tanzania na Norway 1976; Tanzania na Sweden 1976; Tanzania na Finland 1976; Tanzania na Denmark 1976; Tanzania na India 1979; Tanzania na Canada 1995; na Tanzania na nchi ya Afrika Kusini mwaka 2005. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mikataba hii yote ilikuwa na nia njema kabisa ya kuvutia wawekezaji (Foreign Direct Investment), kubadilishana teknolojia pamoja na huduma mbalimbali. Lakini mikataba yote hii ni ya muda mrefu sana mkataba wa kwanza wa mwaka 1968 ni miaka mingi karibia miaka 50 na kitu lakini hata wa mwaka 2005 ni miaka 17. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naliomba sana kwa kuwa suala hili ni la kisera naiomba sana Wizara ya Fedha, ni muda muafaka wa kufanya marejeo katika mikataba hii. Katika eneo hili kuna uwezekano mkubwa sana wa kupoteza mapato, kwa hiyo, niishauri sana Wizara ya Fedha iridhie ifanye marejeo ya mikataba hii ya muda mrefu ili tupate mapato ambayo tunastahili katika maeneo hayo ya mikataba ya kodi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni mafunzo kwa watumishi wa TRA. Mafunzo kwa watumishi wa TRA ni jambo la msingi sana hasa kwenye mawanda ya ukaguzi wa kodi, natambua kule kwa Idara ya Walipakodi Wakubwa kuna Kitengo cha International Taxation Unit. Naomba sana bila kuwekeza kwenye elimu na mafunzo kwa watumishi wa TRA itakuwa ni jambo gumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna International Taxation Unit kama nilivyosema, lakini kuna mambo ya digital economic sasa, kuna transfer of pricing, kuna base oration and profit shift. Kwa hiyo, kuna haja kubwa ya kuhakikisha watumishi wa TRA wanapata mafunzo ya ndani na pamoja na nje ya nchi. Sio vibaya pia wakaenda hata wakafanya field attachment kwenye nchi ambazo zimefanya vizuri kwenye maeneo ya ukaguzi ili na sisi kama Taifa tuwe na wabobezi wa kodi waweze kukagua maeneo mbalimbali ikiwemo na maeneo hayo ambayo nimesema ambayo ni ya kwenye biashara za Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili linakwenda sambamba pia na ukaguzi wa kodi za ndani, najua wanafanya kazi nzuri, lakini bado kuna haja ya kuongeza mafunzo kwa wafanyakazi wa TRA katika ukaguzi wa ndani. Tax Audit huwa ni a very good tool ya Voluntary Tax Compliance, kwa hiyo, ni vizuri wenzetu hawa wakapata elimu ya kutosha, ili waweze kuwafikia walipakodi wetu na hatimaye waweze kukagua kodi mbalimbali katika maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, nitazungumza kwa ufupi eneo la mfumo wa kodi za ndani; tunaipongeza TRA kwa kuwa na mfumo imara sana wa Kodi ya Forodha unaitwa Tanzania Customs Integrated System (TANCIS) unafanya kazi nzuri ya kuonesha mizigo bandarini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye kodi za ndani kuna changamoto ya mifumo, mara nyingi utaona mfumo haufanyi kazi. Kwa hiyo, niombe sana Wizara ya Fedha iwezeshe TRA kupata mfumo wa kisasa kabisa wa kodi za ndani kama alivyosema Mheshimiwa Tarimba. Ule kama nilivyosema ni mfumo mzuri, lakini ni lazima iwezeshwe ili tuwe na uhakika mfumo huu kufanya kazi, masaa yote na walipakodi wetu waweze kupata urahisi wa kulipa kodi kama ambavyo inatarajiwa.

Mimi baada ya kusema hayo nishukuru sana niipongeze tena Wizara na niiombe tu Wizara iiwezeshe TRA, ili iweze kukusanya makusanyo ya kutosha ili kuweza kufadhili miradi yetu ya maendeleo na huduma kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)