Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Fedha. Kwanza nami niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, kwa kazi kubwa anayoifanya na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, nimefuatilia hotuba ya Waziri na yapo maeneo matano, kama muda utaniruhusu nitaomba kuchangia.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kwenye bajeti hii tumeona Ofisi ya Msajili wa Hazina ikichangia shilingi bilioni 629 kutokana na magawio ya mashirika ya umma ambayo Ofisi ya Msajili wa Hazina inayasimamia, na nitumie fursa hii kumpongeza binafsi Msajili wa Hazina, Bwana Mgonja, na timu yake yote.

Mheshimiwa Spika, lakini niombe sana Serikali, tulisema hapa kwenye taarifa ya Kamati na ninaomba niseme hapa, mpaka ninapozungumza hapa yako mashirika 30 yasiyokuwa na Bodi za Wakurugenzi. Sasa kwenye mashirika haya, kwenye cooperates, Bodi ya wakurugenzi ndiyo kama Bunge lako hili.

Mheshimiwa Spika, unapokuwa na shirika ambalo lina management, halina bodi, hata zile hoja walizokuwa wanazungumza akina Mheshimiwa Subira Mgalu za kiukaguzi, hata zikifikishwa kwa afisa masuuli na bodi hakuna tija inakuwa iko chini sana. Niiombe sana Serikali iongeze kasi na itengeneze mfumo mahususi wa kuhakikisha mashirika haya bodi zinapomaliza muda wake basi kuwe na bodi mpya ili succession plan iweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni eneo ambalo ningeomba niongee kwa msisitizo mkubwa. Ni eneo la kilimo. Kilimo cha nchi yetu kina¬-employ zaidi asilimia 65 ya watu. Ndio sekta inayoajiri watu wengi zaidi, lakini kilimo kina mchango mkubwa kwenye GDP ya nchi yetu takribani 29.1%. Tulipata taarifa hapa kwamba Benki Kuu imetenga shilingi trilioni moja kama stimulus fund ya kusaidia kupata mikopo ya riba nafuu kwenye mabenki.

Mheshimiwa Spika, taarifa nilizonazo mimi mpaka hivi tunavyozungumza hata shilingi moja bado haijatoka Benki Kuu kwenda kwenye benki yoyote ya kibiashara ikiwemo Benki ya Kilimo. Nimuombe Mheshimiwa Waziri akija ku-wind up hapa atueleze hii trilioni moja iliyokuwa imetengwa na Benki Kuu kwa ajili ya kusaidia mikopo ya kilimo, maana wote mnafahamu mkulima, hapa ameongea Mheshimiwa Maganga, hizi rfiba anazoziongelea kwenye benki za biashara wanakopeshwa wafanyabiashara, wanakopesha watu wenye security, hakuna sehemu mkulima anaweza kupokelewa akakopeshwa na kama atakopeshwa kwa riba hizi anazoongea Mheshimiwa Maganga hakuna mkulima anaweza kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ndio maana tuliipongeza sana Serikali ilivyotenga hii trilioni moja tuliamini sasa muarobaini wa mikopo ya kilimo unaenda kupatikana, lakini mpaka sasa pamoja na kwamba masharti yaliyotengenezewa ile shilingi trilioni moja moja kwa moja yali-exclude Benki ya Kilimo kwa sababu inakosa zile sifa zilioainishwa kwenye masharti yale ya Benki Kuu tungetegemea kuona mikopo hii ya kilimo kwenye benki nyingine yanatoka.

Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa waziei akija ku-wind na sio vyema, kaka yangu, Yanga mwenzangu, kushika shilingi, lakini nitakuwa sina jinsi. Atueleze hii shilingi trilioni moja ni wakulima wangapi wa benki ipi wameshapata mikopo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inawezekana sisi watu wa Dar es Salaam hatuna wakulima, lakini tunazungumzia nchi mzina, tunazungumzia Waheshimiwa Wabunge ni wakulima humu ndani, na sisi chakula cha Dar es Salaam kinatokana na kilimo cha nchi nzima. Kwa hiyo, tungependa kuona jambo hili linafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu, eneo la sensa. Niipongeze Serikali maandalizi yanaenda vizuri, lakini bado kuna kitendawili cha wale watakaotumika kufanya sensa ile ya watu na makazi. Tumeona kwenye postcode, postcode kule kwetu kuna asilimia imetekelezeka kwa utendaji mzuri na kuna asilimia imefeli kutokana na kupata watu, kweli tuna matatizo ya ajira, kweli vijana wetu hawana ajira, lakini unapata mtu ambaye hana weledi wa kiutumishi, anapewa kazi kwa kuwa ina posho ataomba, lakini unakuta mtu anatoka Msasani anakuja kuhesabu watu Gongo la Mboto, tija inakuwa iko chini.

Mheshimiwa Spika, ni ushauri tu kwa Serikali, sensa za miaka ya nyuma zilikuwa zinatumia sana walimu. Walimu si tu kwamba wana weledi, lakini ni watumishi, wanaaminika, wanaishi maeneo yale, wanaheshimika na jamii. Kwani walimu wa nchi hii wamekosa nini? Wamekosa sifa gani kutumika kwenye maeneo haya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi niseme inawezekana tukachukua jambo hili kama tumetengeneza solution ya ajira ya vijana ambao hawana ajira, kweli tunataka kuwatetea, lakini tuangalie tija ya sensa.

Mheshimiwa Spika, na nitumie fursa hiyohiyo kutoa wito kwa wananachi kujitokeza kwa wingi sana kuweza kushiriki zoezi la sensa kwa sababu sensa hii ndio inaenda kujenga msingi wa maendeleo na utengaji wa fedha za miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, sio kwa umuhimu wake, kumekuwa na kilio kirefu cha wafanyabiashara wanapoenda kutafuta TIN Number. Mamlaka ya Mapato Tanzania inataka kuwe na assessment, kuwe na makadirio ya mapato na akipewa TIN Number ile robo ya kwanza alete marejesho. Anazitoa wapi na hajaanza biashara? Akina Mheshimiwa Katimba wamewahi kuchangia Mabunge ya nyuma, Wabunge wengi wamechangia, hivi kuanza na assessment ya zero tunapata tatizo gani?

Mheshimiwa Spika, ili mtu yule akianza biashara aje a-declare mapato aanze kulipa. Sasa unavyompa mtu TIN Number leo, ndio maskini wa Mungu labda kastaafu ama hana ajhira ama anajiajiri, kapata kiusajili chake, anataka TIN Number unamwambia wewe utaleta shilingi 400,000 kwa mwaka na robo ya kwanza ulete shilingi 100,000 anaitoa wapi? Ni kilio kikubwa, ni kilio kikubwa kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wa nchi hii ambao tunaomba sana Serikali iliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali ni mbia katika biashara hizi, mbia ambaye hatoi mtaji wala haji kufanya biashara kwenye maeneo haya, kwa hiyo, inatakiwa afahamu kwamba, mtu anapojitolea kufanya biashara ndio amejitolea kuwa mbia mpya wampokee vizuri watengeneze mazingira ya kumsaidia kufanya biashara, ili akipata yeye na kodi imepatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemsikia Mheshimiwa mmoja amechangia hapa kuhusiana na EFD machine. Kule kwangu kuna mfanyabiashara mmoja amenitumia message amefungiwa biashara kule Kigogo Fresh Pugu. Unamfungia mfanyabisahara duka kwa kuwa hana EFD machine, haya, sasa ameshafunga, unapata wapi kodi?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo elimu itoke, lakini tuangalie mfumo mzuri wa kuwasaidia wafanyabiashara hawa waweze kufanya biashara vizuri.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. JERRY W. SILAA: Kengele ya pili? (Makofi)

SPIKA: Sekunde 30. Malizia sentensi.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia nikushukuru wewe, sio kwa sura ile ya Mheshimiwa Maganga kwa kunipa nafasi ya kusema, maana nafasi zipo na zinapatikana, lakini niendelee kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)