Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango - Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa - Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Fedha na Mipango, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha ubunifu wa ukusanyaji mapato na usimamizi mzuri wa matumizi ya Serikali ikiwa ni pamoja na uendelezaji wa miradi ya kimkakati na pia utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi kumi ya bajeti ya mwaka huu, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango imesimamia kwa ufanisi ukusanyaji mapato na utekelezaji wa miradi mingi ya miundombinu ya barabara, reli, bandari na kadhalika. Napongeza Serikali kwa mwendelezo mzuri wa utekelezaji wa mradi wa kihistoria wa umeme Mto Rufiji. Mradi wa kihistoria wa ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR pamoja na uboreshaji wa bandari utaimarisha kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi yetu. Umeme, reli na bandari ni nguzo imara ya kiushindani katika uchumi wa Tanzania na nchi za Maziwa Makuu na hata za Kusini mwa Afrika na Kati.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki wakati dunia inapambana na janga la corona virus (covid-19), tumejifunza umuhimu wa kuwepo kwa mikakati mbadala kutokana na nchi nyingi tunazoshirikiana kibiashara na kiuchumi kukumbwa na mtikisiko wa kiuchumi. Biashara ya usafirishaji hasa wa anga imeathirika sana na napongeza mkakati wa shirika la ndege kuanza kutumia ndege zake kusafirisha mizigo. Mkakati huu ambao umetumiwa na hata mashirika makubwa ya ndege utawezesha usafirishaji wa mazao yetu ya kilimo kufikia masoko kirahisi na hapo hapo uhakika wa mapato kwa shirika la ndege hasa kipindi hiki kukiwa na upungufu wa abiria. Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Msajili wa Hazina anapaswa kuendelea kuimarisha mitaji kwa mashirika ambayo yatachochea ukuaji wa uchumi ikiwemo Benki za TADB, TIB na ATCL ili iweze kusimama kibiashara ikiwa ni nguzo muhimu hata kwa sekta zingine.

Mheshimiwa Spika, napendekeza kuhakikisha ujenzi wa SGR unaendelea hata kwa kutafuta vyanzo mbadala vya fedha kugharamia ujenzi huo, kwa vile kutakuwa na fursa kubwa za usafirishaji. Pamoja na ujenzi wa SGR, napendekeza kuendelea na kuboresha reli ya TAZARA na uboreshaji wa bandari zetu ikiwemo ujenzi wa bandari kavu ikiwemo ya Inyala, Mbeya ambayo ina fursa kubwa katika kipindi hiki ili kupunguza gharama za kusafirisha pembejeo na mazao. Serikali ichukue hatua za haraka kuinusuru reli ya TAZARA hata ikibidi kurekebisha mikataba ya umiliki na uongozi ili mradi iendeshwe kwa tija.

Mheshimiwa Spika, kuna kuchukua hatua za makusudi kwa kutumia zaidi TAZARA kusafirisha mizigo ambayo imeelemea hata uwezo wa barabara zetu. Usafirishaji wa mizigo kwa kutumia TAZARA ilenge kupunguza gharama za pembejeo kwa wakulima na wakati huo kupunguza gharama za kusafirisha mazao ya wakulima.

Napendekeza Serikali iwekeze angalau shilingi bilioni 100 kwa mwaka kwa kipindi cha miaka mitatu kwa ajili ya kuboresha mindombinu ya reli na karakana. Uwekezaji huu utawezesha TAZARA kujiendesha kwa faida na kuipunguzia Serikali mzigo wa kulipa zaidi ya shilingi bilioni 15 kwa mwaka ikiwa ni mishahara ya wafanyakazi wa TAZARA. Uwekezaji huu unahitaji haraka wakati Serikali za Tanzania na Zambia zinaendelea na jitihada za kurekebisha mikataba ikiwemo wa uendeshaji wa TAZARA. Pamoja na kuboresha TAZARA, napendekeza kukamilisha taratibu za ujenzi wa bandari kavu ya Inyala, Mbeya ambapo Mamlaka ya Bandari kwa kipindi kirefu wamewahakishia wananchi kulipa fidia ya eneo lao wanalolichukua.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za mapato kutokana na janga la Covid-19, kuna fursa nyingi za muda mfupi za kuongeza mapato kupitia hatua za kiutawala kiwemo ya kuondokana na matumizi na malipo ambayo hayana tija kwa Serikali na hata walipakodi. Kutokana na mahitaji makubwa ya uwekezaji kwenye miradi ya kimkakati, uchumi wetu utaendelea kuwa na mahitaji makubwa ya mikopo ya pesa za kigeni na wakati huo huo kulipa mikopo iliyoiva.

Pia Serikali iweke mkakati wa kuhakikisha mapato ya fedha za kigeni yanaongezeka kupitia mazao ya kilimo, madini na utalii. Kuongezeka kwa mapato ya fedha za kigeni yatasaidia kuimarisha Deni la Taifa kuwa himilivu na pia kuendeleza utulivu wa shilingi yetu dhidi ya sarafu kuu za kigeni na hata kuhakikisha utulivu wa mfumuko wa bei. Serikali ihakikishe kipaumbele cha kuwekeza kwenye kilimo ikiwemo pembejeo na umwagiliaji kwa lengo la kuongeza tija na pia kuongeza mapato ya fedha za kigeni na kulinda mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Spika, kutokana na upotevu mkubwa wa fedha za Serikali ikiwemo miradi ya Serikali Kuu na Halmashauri, napendekeza Serikali kuimarisha Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani ili kuongeza ufanisi na uhuru wa Wakaguzi wa Ndani. Serikali ihakikishe Mkaguzi wa Ndani wakati wote anakuwa huru kutoka kwa Afisa Masuuli. Wakaguzi wa Ndani wa Halmashauri wasimamiwe na Mkaguzi Mkuu wa Mkoa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa. Serikali iimarishe uhuru wa Mkaguzi Mkuu wa Ndani (Internal Auditor General) na hata kupandisha hadhi ya Ofisi kuwa na Fungu la Bajeti linalojitegemea.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.