Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Awali ya yote niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na niwaambie kwamba michango yao tumeipokea baadhi nitaisemea hapa, lakini nitawaomba waridhie mingine tutaitoa kwa maandishi na kwa hotuba tutakapokuwa tunawasilisha Bajeti Kuu ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri wangu Mheshimiwa Chande kwa ufafanuzi wa hoja ambazo amezitoa na kwa ushirikiano ambao amekuwa akinipatia katika kutekeleza majukumu yangu.

Mheshimiwa Spika, la tatu, niwapongeze Kamati ya Bunge wakiongozwa na Mwenyekiti pamoja na Makamu wake, Kamati nzima pamoja na wataalam wa Wizara ya Fedha na Mipango na Taasisi zake kwa kweli kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakinipatia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaelezea hoja zilizotolewa na Wabunge naomba mambo haya nitakayosema yaingie kwenye kumbukumbu. Jambo la kwanza naomba Bunge lako tukufu litambue ukubwa wa kazi aliyonayo Mheshimiwa Rais ya kuwezesha miradi ya maendeleo iweze kufanyika katika nchi yetu. Hili jambo baadhi ya watu ambao hawajaangalia takwimu za nchi yetu zinasemaje wanaweza wasijue kazi aliyonayo Mheshimiwa Rais japo wanaona mambo yanakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika nchi yetu karibu kila kitu ni cha lazima, karibu kila kipengele cha matumizi ni kipengele usichoweza kukiahirisha, kipengele hicho ndicho kinachofanyakazi iwe ngumu sana kwa sababu karibu kila expenditure item, kila kipengele cha matumizi unachokigusa ni kipengele usichoweza kukiahirisha. Kwa mfano tumetoa kwenye taarifa yetu kwamba makusanyo yetu ya ndani yalikuwa shilingi trilioni 19.99 ukienda kwenye mchanganuo wa haraka Deni la Taifa kwa mwaka linachukua karibu shilingi trilioni 6.9 ni kama shilingi trilioni saba hivi, mishahara ukiweka na tunakoelekea itachukua zaidi ya shilingi trilioni sita na sehemu ukiweka na mahitaji mengine ambayo ni ya lazima.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye miradi mikubwa reli peke yake tuna zaidi ya shilingi trilioni 1.45 kwa miradi ambayo kwa lot ambazo zilikuwa zinaendelea. Ukienda kwenye barabara tuna zaidi ya shilingi bilioni 579 ambazo hizi zinapitia kwenye TANROADS, ukienda kwenye TARURA barabara za vijijini ambazo fedha hizo ziko kwenye mifuko hugusi gusi tu ni zaidi ya shilingi bilioni 414 kwa mwaka, ukienda kwenye elimu ya juu peke yake ni zaidi ya shilingi bilioni 423.5, ukienda kwenye REA ni zaidi ya shilingi bilioni 367, ukienda kwenye maji ni zaidi ya shilingi bilioni 346, ukienda kwenye elimu bila malipo ni zaidi ya shilingi bilioni 202. Hapa unaongelea kwenye mahitaji yale usiyoweza kuyaahirisha ni shilingi trilioni 16.5 kati ya shilingi trilioni 19 hayo ni yale mahitaji usiyoweza kuyaahirisha, yale ambayo fedha zake zimehifadhiwa mahsusi kwa matumizi yale.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake afya peke yake inachukua zaidi ya shilingi trilioni 2.5, elimu inachukua zaidi ya shilingi trilioni 5.6, maji yanachukua zaidi ya shilingi bilioni mia nane na nusu na social production inachukua zaidi ya shilingi trilioni 1.8. Unaweza ukaona ni space kiasi gani inayosalia kwenye matumizi ya shughuli zingine, ni kiasi gani kinachosalia kwenye shughuli zingine haya ni matumizi mengine ambayo hauwezi ukarudi nyuma pawe na UVIKO, pawe na vita Ukraine, pawe na ukame, haya ni matumizi ambayo huwezi ukayaahirisha.

Mheshimiwa Spika, kazi hii yote ndiyo inayomfanya Mheshimiwa Rais asilale, ndiyo maana utaona leo yuko huku, leo yuko huku na wengine wanadhani haya mambo yanaweza yakaenda hata pasipokuwa na mwanga, hata pasipokuwa na jua limewaka. Mimi nawaulizeni swali dogo tu ni Waziri gani wa Fedha wa nchi za kiafrika anaweza akafanya appointment ndani ya wiki moja akaonana na Rais wa Benki ya Dunia? Ni Waziri gani wa nchi za Kiafrika anaweza akafanya appointment ndani ya siku tatu akaonana na Rais wa IMF? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya ni mambo ambayo yanafanyika kwa uzito wake na Mheshimiwa Rais anaona ayaongezee nguvu na ndiyo maana unaona alipoenda kwenye nchi za Ulaya alionana na taasisi zote zile za muhimu kwa shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alipoenda Marekani alionana na taasisi zote hizi za muhimu kwa wiki moja ameonana na Rais wa Benki ya Dunia, Rais wa IMF na ameonana na Makamu wa Rais wa nchi kubwa kama ya Marekani na mimi namshukuru sana alinifanya niwe Mnyiramba wa kwanza kuingia Ikulu ya Marekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya ni sehemu tu ya kazi kubwa ambazo zinalazimika Rais aingie mstari wa mbele ili kazi hizi ziweze kwenda. Hivyo hivyo na alivyokuwa Falme za Kiarabu kule alionana na viongozi wakuu wote wale na maeneo mengine yapo ambayo yanakuja ambako yatatusaidia katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kwa hiyo, nimshukuru sana na nimpongeze na niwaombe watanzania waielewe kazi hiyo ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alisemea Mheshimiwa Mbunda pamoja na Wabunge wengine waliochangia kuhusu jambo la ukaguzi wa ndani, tumepokea hoja hiyo tutaitolea ufafanuzi tutakapokuja kwenye Bajeti Kuu.

Kuhusu Ofisi za Mamlaka ya Mapato tumepokea hilo nilishapokea na baadhi ya Wabunge wengine ambao wameongelea katika Bunge hili wakiwa wanaongea wengine kupitia maswali pamoja na hawa ambao ameongelea tumelipokea na hilo tutabainisha na mipaka mingine tutatembelea na tutachukua uamuzi baada ya tathmini ili tuweze kuwarahisishia wananchi utaratibu wa kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, tumepokea suala la chuma chakavu na Naibu Waziri ameliongelea vizuri. Tumepokea hoja pia aliyoisemea ndugu yangu Tarimba mwananchi bingwa mtarajiwa ambaye amelielezea sana katika eneo hili la kutumia mifumo ni njia ambayo itatupa ufanisi na Mheshimiwa Rais amelisisitiza sana hili na sisi ndani ya Wizara tunaendelea kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ameongelea Mwenyekiti wangu wa Kamati Mheshimiwa Sillo mazingira ya kufanyia biashara hii ni kazi kubwa tunaendelea nayo namna ya kutekeleza blue print yetu ambayo imebainisha maeneo mengi sana ambayo yatatupa mazingira mazuri ya kufanyia biashara zikiwemo biashara kubwa pamoja na biashara ndogo ndogo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo mengine ambayo ameongelea yanayohusiana na mikataba ya double taxation. Mafunzo tumepokea na hilo ni jambo ambalo tunatoa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mama yangu Leah pamoja na Wabunge wengine wameongelea fedha za miradi na kwa kweli kazi kubwa sana imefanyika kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea karibu mikoa yote ya nchi yetu imepata zaidi ya asilimia 100 ya fedha za maendeleo walizokuwa wanatarajia kuzipata katika mwaka huu wa fedha na ndiyo maana mnaona miradi ya maendeleo inaenda kwa kasi ambayo inastahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimemsikia ndugu yangu Mtemvu, nimemsikia rafiki yangu Maganga Ofisi ya TRA nitatembelea, tutaenda kuifungua na Maganga wewe ni kichwa ulitoa wazo la kununua mitambo ya kutengenezea barabara wazo lako tulilitekeleza katika Wizara ya Maji na tutaangalia na katika maeneo mengine na kuhusu masuala ya riba tunaendelea kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachotumia kwenye riba ni utaratibu kwamba soko letu tunatumia nguvu ya soko katika kuamua masuala haya ya kiuchumi. Majirani zetu waliwahi kujaribu kutumia nguvu ya dola kuweka ukomo kwamba asubuhi tu tunaamka tunasema leo riba itakuwa asilimia tano, ilileta madhara kiuchumi kwa sababu hivi viashiria vya kiuchumi mpana huwa vinategemeana, unaweza ukakiathiri kimoja ikaleta tatizo kwenye viashiria vingine. Kwa hiyo, tutaendelea kutumia nguvu ya soko lakini pia na ya kisera kuweza kuhakikisha kwamba tunafika katika hatua hiyo hili linakwenda likitekelezeka na tunaamini itaenda kufanyika na kukamilika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Jerry nimesikia haya masuala ya Bodi tutayajibu katika hotuba kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu nani atatumika kwenye sensa, sasa hivi vijana hata ukiondoa walimu tuna vijana ambao ni wasomi ambao na wenyewe ni walimu kimsingi wengine ni walimu, wengine ni walimu wa akiba, kwa hiyo, tuliona kwa sababu zoezi hili linahitaji watu wengi sana, walimu watatumika kufundisha, watatumika kusimamia, lakini na hawa vijana ambao wengi wao wameshasoma, ni wasomi wazuri na wenyewe watafanya hiyo kazi huku wakishirikiana na walimu ili tuweze kuleta ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kubwa tulilolifanya tumefanya hawa vijana watoke katika maeneo yale yale ambayo watayasimamia ili kupunguza gharama kwa sababu kwa sasa hivi hakuna kata isiyo na wasomi. Kwa hiyo, tuliona watumike kule kule waliko ili waweze kufanya kazi hiyo kwa ufanisi.

Mheshimiwa Cecilia pamoja na mama mkwe wangu pale Mama Kaboyoka nimepokea jambo hilo tutalisemea kwenye hotuba kubwa, lakini hili la maduka ni jambo ambalo tunaendelea kulifanyia kazi, hatujamaliza idadi yote, lakini tunaendelea kulifanyia kazi na Mheshimiwa Cecilia mtani wangu, ukihitaji takwimu pia nitakupatia, lakini hatujafika mwisho kwa sababu tunafanya kwa umakini, lakini nikuhakikishie ni zoezi ambalo linaendelea kufanyiwa kazi na wewe ukitafiti zaidi utapata taarifa kama hizi ninazokwambia na baadhi ya watu wameshapata utekelezaji wa jambo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu wale walioomba leseni mpya pamoja na yale masharti hilo ni jambo kubwa la kisera nitaomba uridhie ili tulitolee tamko baada ya kuwa tumeshakamilisha hotuba yetu kubwa tunayoiandaa ili tuweze kutoa tamko ambalo litahusika na watu wengine wote waweze kufuata muongozo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hiyo kama nilivyosema mambo mengine tutayajibu kwenye hotuba kubwa ya bajeti, nakushukuru na nakupongeza kwa kuendesha kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa baada ya kusema maneno hayo naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naafiki.