Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu nitazungumzia mambo matatu. Jambo la kwanza falsafa ya uongozi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka mmoja cha uongozi wake Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameonyesha kuwa ni kiongozi msikivu, mpole, mtulivu na anayetumia hekima kubwa sana katika kufanya maamuzi yenye maslahi makubwa kwa Taifa letu. Nitatoa mfano wa mambo manne; moja, Mheshimiwa Suluhu Hassan amefufua na kuimarisha mahusiano ya Tanzania na nchi za nje na kukuza hadhi na heshima ya Taifa letu katika medani ya kimataifa. Pili, Serikali anayoiongoza ina mpango wa kuanzisha Chuo kipya cha Teknolojia, Habari na Mawasiliano hapa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi sasa dunia imo katika awamu ya nne ya mapinduzi ya teknolojia, mapinduzi ambayo yanashuhudia matumizi makubwa ya sayansi ya kompyuta na hasahasa matumizi ya kompyuta zinazofikiri kama binadamu, roboti, mitambo inayojiendesha yenyewe bila kumtegemea binadamu. Bila shaka maendeleo haya yanahitaji vijana wenye ujuzi, maarifa, utaalam katika masuala ya sayansi ya habari na teknolojia ya habari na mawasiliano kwa ujumla na bila shaka wazo la Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuanzisha Chuo cha Teknolojia ya Habari limekuja katika wakati muafaka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amefufua Mradi wa Ujenzi wa Bandari ya Kisasa ya Bagamoyo na nne, Rais Samia amefufua Mradi wa Kusindika Gesi Asilia huko Mtwara.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, nchi yetu inawekeza fedha nyingi kila mwaka kwa ajili ya ujenzi wa barabara lakini kwa bahati mbaya sana barabara hizi zinaharibika katika kipindi kifupi sana. Kwa hiyo, nchi yetu inalazimika kutenga fedha nyingine kwa ajili ya kuzifanyia marekebisho na matengenezo barabara hizo. Kwa kawaida barabara inahitaji kufanyiwa matengenezo makubwa katika kipindi cha miaka kumi mpaka ishirini, lakini kwa upande wetu hali ni tofauti sana katika kipindi kisichozidi miaka mitatu barabara zetu nyingi zinaharibika na hatimaye tunalazimika kutenga fedha nyingi kwa ajili ya kuzifanyia matengenezo. Nchi yetu ni maskini na haiwezi kumudu gharama za namna hii. Ili kuepuka matengenezo ya mara kwa mara ya barabara, hivyo, napendekeza mambo mawili yafuatayo: -

(i) Serikali iteue wahandisi waadilifu na wenye weledi wanaoweza kuwasimamia wakandarasi wa barabara ili barabara zijengwe kwa kiwango na ubora unaotakiwa. (Makofi)

(ii) Naunga mkono hoja ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti; Serikali iimarishe Kitengo cha Ukaguzi wa Barabara ili kubaini uharibifu mapema na hatimaye kufanya matengenezo yanayohitajika kwa wakati. Jambo hili litatusaidia sana katika kudhibiti matumizi makubwa ya fedha katika matengenezo ya barabara zetu kama Waingereza wasemavyo a stitch in time saves nine, kwa Kiswahili usipoziba ufa utajenga ukuta. (Makofi)

(iii) Mwaka 1987 marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alipokuwa akihutubia Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa alisema maneno yafuatayo: -

“Iwapo nchi yetu inataka kupiga hatua kubwa za maendeleo na za haraka, hatuna budi tuzitumie rasilimali zetu kikamilifu.”

Mheshimiwa Spika, kwa mawazo yangu bado hatujauzingatia ushauri huu wa Mwalimu ipasavyo hasa katika sekta ya gesi asilia. Mwenyezi Mungu ametubariki na kutujalia gesi ipatayo trilioni 57 za ujazo, lakini kwa bahati mbaya sana tumeweza kutumia kiasi hiki cha gesi kwa kiasi kidogo sana. Iwapo tunataka kukabiliana kikamilifu na kupanda kwa bei za mafuta zinazotokea kila wakati tunapaswa kuimarisha uchumi wa gesi. Kwa hiyo, napendekeza Serikali ifanye mambo yafuatayo: -

(i) Serikali iongeze matumizi ya bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam. Kwa bahati mbaya hivi sasa Serikali imetumia bomba hili kwa asilimia 10 tu. Habari hizi si njema hata kidogo, tunapaswa kuongeza matumizi ya bomba hili. (Makofi)

(ii) Serikali ihakikishe mipango na matumizi ya nishati ya gesi katika matumizi hasa katika kuendesha magari ya Serikali na mizigo ili kupunguza gharama ya usafiri na usafirishaji.

(iii) Serikali iharakishe mipango ya kutekeleza mradi wa kusindika gesi asilia kule Lindi.

Mheshimiwa Spika, hapana shaka tukichukua hatua hizi nilizozieleza tutaweza kupunguza uagizaji wa mafuta kutoka nje kwa kiasi kikubwa na naamini hali hii itatusaidia sana kupunguza makali ya maisha kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)