Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu kwenye hii Bajeti Kuu na nianze mchango wangu kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kuipongeza Serikali kwa bajeti nzuri. Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara ya Fedha, bajeti hii imeenda kujibu vilio vingi vya Watanzania na niseme naipongeza sana.

Mheshimiwa Spika, kitendo cha Serikali kuondosha ada ya kidato cha tano na cha sita kimeenda kujibu vilio vya wananchi wengi. Mimi mwenyewe binafsi yuko kijana mmoja, mjukuu wa mama mmoja maarufu kule tulikokulia, marehemu Kibibi ilikuwa nimlipie ada wiki hii, kwamba kauli hii na mimi mwenyewe hela yangu imepona, naipongeza sana Serikali. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, misamaha ya kodi kwenye kilimo, mifugo na uvuvi inaenda kuwatengenezea Watanzania maeneo mengi zaidi ya kujishughulisha kwenye shughuli zao na sasa tunaenda kupata matokeo chanya kwenye Sekta ya Kilimo, kwenye Sekta ya Mifugo na Sekta ya Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza nitakalolisemea ni eneo la kodi na mimi nimpongeze kidhati Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kauli yake aliyoitoa pale Bukoba kwenye ziara yake ya Mkoa wa Kagera. Kauli ile imepokelewa vizuri sana na wafanyabiashara wa nchi hii. Kumekuwa na dhana na tumekuwa tukisema hapa kwamba Serikali kwa kukusanya kodi anajikuta ni mbia asiyechangia mtaji kwenye biashara ya Mtanzania. Kwa hiyo tumekuwa tukiishauri sana Serikali ukusanyaji wao wa kodi, taratibu zao za makusanyo ziwe rafiki na elimu itolewe kwa wafanyabiashara na wasitengeneze dhana ya kugombana na wafanyabishara na kufunga biashara zao. Kauli ile ya Mheshimiwa Rais yuko rafiki yangu mmoja ambaye najua kabisa hata mimi hakunipigia kura mwaka 2020 alinitumia speech ile na akaniandikia Mama Samia Suluhu Hassan amepata kura yangu 2025.

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali, niwaombe sana TRA waende wakatekeleze maagizo yale. Tuliongea hapa, wako wafanyabiashara wadogo hawa presumptive tax regime ambapo naona sasa hapa tena wamewekewa asilimia 3.5 ya turn over. Asilimia 3.5 ya turn over siyo hela ndogo, lakini hawa ndiyo wenye mitaji ya Sh.1,000,0000 au Sh.500,000, unapomwambia aende akanunue mashine ya Sh.500,000 ni ngumu kuweza kutekelezeka. Sasa kama Serikali ni mbia wa kodi ni lini Serikali itaona ni wajibu wake kumpa mtu mashine ya EFD bure ili mashine ile sasa iweze kuweka rekodi za kodi Serikali iweze kupata kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako marekebisho mengi ya kodi ambayo Serikali imeelekeza yafanyike. Nitachangia kwa uchache na nadhani nitachangia vizuri kwenye Finance Bill. Unapoweka withdrawing tax ya asilimia mbili kwenye small scale miners, maana yake unaongeza pale ilipokuwa loyalty na ile inspection charge ya asilimia sita na moja sasa unaenda kwenye asilimia tisa.

Mheshimiwa Spika, as we speak right now dhahabu nyingi inayochimbwa na wale wachimbaji wadogo wale wa kushika na mercury inatoroshwa nchini. Unapoongeza kodi Serikali hamuendi kuongeza mapato mnakwenda kuongeza utoroshaji wa dhahabu na ziko nchi zinanufaika na utoroshaji huo. Mwaka jana hapa iliwekwa withholding tax kama hii kama kwa wakulima, Bunge la mwezi wa Agosti liliiondosha. Sasa niwaombe sana Serikali tusingoje tufanye jambo tupate kilio, tuje tena kubadilisha sheria wakati jambo tunaliona halitatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda ni mchache lakini ukichukua turn over za corporates kubwa Tanzania Breweries Limited, Vodacom Tanzania, TIGO ukaangalia na corporates tax wanayolipa ni chini ya hiyo asilimia 3.5. Mwaka huu wa fedha Vodacom ime-declare loss, TIGO wame-declare loss, kwa hiyo hawajalipa corporate tax, unapotaka hawa presumptive tax measure walipe 3.5 percent ya gross huendi kuwatendea haki na nadhani utekelezaji wake utakuwa ni mgumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda niseme tu Serikali niiombe na niishauri iongeze nguvu kwenye communication. Tulikwenda kule Amani Muheza kwa Mheshimiwa MwanaFA tulikuta wale wasafirishaji wa vipepeo wanaathirika na lile katazo la Serikali la kusafirisha wanyama hai nje as if wanyama simba wanafanana na vipepeo. Juzi Serikali ikatoa kauli hapa kauli, nilivyoielewa ni kusaidia wale wa vipepeo na wale wanaoshika mijusi na wanyama wengine wadogo wadogo, lakini kwa sababu haikuwa communicated vizuri ikatengeneza taharuki, Waziri naye alivyopata taharuki akajaa upepo, akafuta lile agizo. Kwa hiyo, wale waliokuwa wanasherehekea maskini wa Mungu wale Conservators wa misitu wa kule Amani ambao wanasaidia kutunza misitu kwa ajili ya vipepeo na wao wamerudi tena kwenye back to square one 2018. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hili la TIN Number, kwa tabia za TRA za ukusanyaji wake wa kodi ukimwambia mwananchi naye apewe TIN Number lazima ataruka kimanga, anajua tunarudi kule kule wanakofanyiwa wafanyabiashara, sasa tutafanyiwa Watanzania wote. Naomba Serikali ifanye communication, ielimishe wananchi na ndio maana Mheshimiwa Twaha amesema ziko nchi zinaita Insurance Number, ziko nchi zinaita Social Security Number, kikubwa Mtanzania leo tunavyozungumza hapa alipo mwenyewe ni mlipakodi. Anaponunua pembejeo ile transaction inatakiwa ilipiwe kodi, anapolipa nauli kwenye daladala, anapopanga chumba, anaponunua chakula zote zile ni transaction za kibiashara ambazo huyu mwananchi angekuwa na namba yake zingeingia kwenye taarifa zake. Tunapoongelea universal worthy insurance ndio atajikuta ametumia kiasi gani kwa mwaka apate bima ya maisha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa wanaiweka TIN Number limebutuka huko la kwao hilo, kazi yao kwenda kuelimisha wananchi kwamba namba hii ya NIDA ikitumika kuweka miamala yako inakusaidia wewe mwenyewe, kama tunagawa pembejeo za ruzuku tunajua wewe ni mnunuaji mzuri na matumizi yako na kilimo chako upate pembejeo. Sasa naamini Serikali italifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kifupi, niombe mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, niombe na niipongeze Serikali imemwongezea fedha Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) kukagua matumizi ya Serikali. Imepokea ushauri wa Kamati ya Bunge, imeongeza meno kwa Internal Auditors kusimamia matumizi. Sasa niiombe iendelee kupokea ushauri wa kuweka mifumo ya TEHAMA. Mifumo ya TEHAMA ndio itasaidia kupunguza matumizi ya Serikali na mifumo hii ya uangalizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nia yangu ni nini? Let the Government be the Government, let corporate be corporate and let the Parliament be Parliament. Huwezi ukaendesha Serikali kama shirika la kibiashara this is not a profit-making organization, yaani leo Kamishna wa Ardhi akopeshwe Prado akitaka kwenda kukagua mgogoro wa ardhi anajiendesha mwenyewe, haitakaa itokee. Tusipende kutengeneza vitu ambavyo vitatengeneza mkwamo kwenye utendaji wa Serikali. Serikali ijiendeshe, matumizi yabanwe, controls ziwepo, mifumo iwepo, lakini uendeshaji wa Serikali ni ngumu kulinganisha na sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kifupi kwenye custom duty, matairi ya bodaboda yameongezwa toka asilimia 10 mpaka asilimia 25. Kule juu wakulima tumewaangalia, wafugaji tumewaangalia, wavuvi tumewaangalia, hebu tuwatambue na hawa bodaboda na wenyewe kama Watanzania na tupunguze kodi kwenye matairi ya bodaboda kwa sababu uendeshaji wa bodaboda sio anasa bali na yenyewe ni ajira kama eneo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko eneo Serikali ina-propose kupunguza mikopo ya halmashauri ya asilimia 10, ambayo ni mikopo inayokopesha makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, eti ibaki asilimia tano. Tunawathamini sana Wamachinga na sisi ni wapiga kura wetu kule mijini, Serikali itafute mahali kwingine fedha ya kujenga miundombinu lakini sio kwa Wamachinga. Mikopo hii asilimia 10 ibaki, hapo ilipo yenyewe haitoshi, kama mnavyogawa pembejeo bure kwa wakulima na sisi wa mjini mikopo hii inasaidia wapiga kura wetu. Hili naomba kushauri na hatutokubali lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona hotel levy ilikuwa asilimia 20 imekuja asilimia 10 inakwenda asilimia tano. Hotel levy ilikuwa ni suluhu ya wale wanaokimbia VAT asilimia 18, wanakuja kwenye hotel levy na ndio maana ika-balance kwenye asilimia 20, haya ni mapato ya Local Government, naomba tuyaangalie.

Mheshimiwa Spika, vile vile niombe jambo moja property tax ilichukuliwa ikapelekwa TRA haikukusanywa na taarifa ziletwe hapa, haikuwahi kukusanywa effective kama mamlaka za Serikali za Mitaa zinavyokusanya. Mwaka jana wakachukua wakapeleka kwenye LUKU, nyumba ya Masaki inalipa Sh.1,000 kwa mwezi Sh. 12,000 kwa mwaka. Niombe kwenye bajeti hii kodi ya majengo irudishwe kwenye halmashauri, ikirudishwa kwenye halmashauri itengenezwe retention scheme asilimia tano ibaki kwenye mtaa, asilimia tano ibaki kwenye kata, isaidie uendeshaji, isaidie mafunzo, ujenzi wa ofisi, posho za Wenyeviti wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji na za Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusitengenezeane fitina ya kisiasa kwa jambo ambalo linawezekana kwa kudhani mishahara ya Madiwani inatakiwa kutoka Serikali Kuu; na kama Serikali haina uwezo basi isijibu suala hilo wakati maeneo mengine wanafanya. Fedha hazikusanywi, hawa viongozi wanatakiwa kuwa ni chachu ya ukusanyaji wa mapato ukisoma Local Government Authority Act na Kanuni za Kudumu za Halmashauri, Madiwani wanapaswa kuwa ni watu wa kuchochea maendeleo na kusimamia shughuli za kijamii kwenye maeneo yao. Waturejeshee kodi ya majengo, watuwekee malengo, mifumo ya kukusanya ipo watuwekee retention scheme. Kuna kata zitanunua magari, zitajenga ofisi za magorofa, zitalipana posho, kuna Kata na Mitaa wananchi wataacha kutozwa Sh.1,000 za barua kwa fedha itakayobaki kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda la mwisho na sio kwa umuhimu hizi kodi ndogo ndogo mara kwa king’amuzi, mtu kashachoka kashatumika siku nzima, karudi nyumbani anataka kuangalia mpira wake wa Yanga anaambiwa king’amuzi tena kilipiwe na tozo. Niombe sana tutengeneze mifumo ya kodi ambayo ni rafiki inayoweza kukusanyika kirahisi ambayo itasaidia Watanzania wapende kodi na wapende Taifa lao.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)