Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niruhusu nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya. Kwa uhakika yeye na wenzake Wizarani wamethibitisha kuwa nia inapokuwepo na mengine yote yanawezekana. Hongera kwa mipango mizuri, Chalinze tunakutakia kila la kheri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mazuri ambayo yanaendelea kutokea Chalinze, barabara inayounganisha Mkoa wa Pwani na Morogoro, inayotoka Mbwewe hadi Mziha hadi Turiani hadi Dumila imeachwa haitengenezwi. Na sasa ni takribani miaka nane toka nyumba ziwekewe alama ya “X” na hakuna lolote ambalo limeendelea. Nafikiri kwa tafsiri ya barabara ya TANROADS, barabara hii inatosha vigezo na hivyo, ni muda muafaka kuiangalia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais aliahidi kuhusu ujenzi wa kituo kikubwa cha malori na mabasi. Mwananchi mmoja wa Chalinze alisema, kama mko tayari Wizara, yeye yuko tayari kutoa eneo; ninachotambua ni kuwa hili ni jambo la kimkakati na nina imani ninyi wasaidizi wake mlitakiwa kulishughulikia. Je, jambo hili mmefikia wapi? Maana muda unakwenda na sioni hatua zikiendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni takribani miaka saba toka ujenzi wa makazi ya Makao Makuu ya Wilaya ya Chalinze yaanze. Nyumba mbili zimejengwa na kwa bahati nzuri aliyefungua nyumba hizo ni Mheshimiwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne na Rais wa sasa akiwa ni Waziri wa Ardhi; sasa hali imeendelea kubaki kama kipindi kile. Je, Wakala wa Nyumba za Serikali analo eneo la heka 50 kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya watumishi watakaokuja kufanya kazi? Je, ni mkakati gani mlionao kuhakikisha kuwa Mamlaka ya Makao ya Wilaya ya Chalinze yanajengwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mvua zinazonyesha maeneo ya Pwani hasa Bagamoyo, yameathirika sana, hususan barabara inayojengwa toka Msata kwenda Makofia, Bagamoyo, ardhi hii imesababisha kufungwa kwa barabara. Mheshimiwa Waziri tuhakikishie kuwa barabara itakapokamilika kesho au siku zijazo, hakutatokea majanga kama yanayotokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, toka utungaji wa Sheria ya Makosa ya Kimtandao wasomi, wanasheria na wanaharakati katika kada mbalimbali wamechambua na kuonyesha mapungufu ya Sheria hiyo. Mfano, ni juu ya ukweli wa data za mteja, Sheria hii Ibara ya 32 hadi 35 zinamlazimisha mtoa huduma kutoa data za mteja wake kwa Mkuu wa Kituo cha Polisi bila kibali cha mahakama. Hii kwa mujibu wa taratibu za haki, kibali cha kutoa taarifa hutolewa na mahakama, hii ni kinyume na taratibu hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 3(a) ya Sheria ya Makosa ya Kimtandao inampa Waziri mamlaka ya kuamua kipi ni kosa na kipi si kosa. Anapewa mamlaka ya kusimamisha na kusitisha huduma na hata pia kuondoa taarifa juu ya kitendo husika, mfano, kuondoa mijadala ambayo yeye ana maslahi nayo au ambayo anaona inagusa ofisi yake. Katika Sheria za Utoaji Haki, haki za kufanya maamuzi ni kazi ya mahakama na Hakimu ndiye mtamkaji, kumpa Waziri nafasi hii ni kufinya utaratibu wa utoaji haki. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie ana mpango gani juu ya sheria hii kandamizi kwa haki za binadamu, ukiachilia mbali matumizi mabaya yanayoendelea ambayo wewe Mheshimiwa Waziri umepewa nguvu na Ibara ya 39 ya Sheria ya Makosa ya Kimtandao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri ambayo mmekwishaifanya katika upangaji mzuri wa mawasiliano, changamoto ya upatikanaji wa mawasiliano imekuwa ni jambo la kawaida hata baadhi ya wananchi kuamini kuwa, wao hawapaswi kuwa na simu. Hapa nawazungumzia wananchi wa Kibindu, Miono, Mkange, Msata, Chalinze na maeneo mbalimbali ya Mji wa Kiwangwa na Kata ya Talawanda. Wakati wa Serikali ya Awamu ya Nne Mheshimiwa Waziri aliniahidi kuongea na watu wa Halotel/Viettel ili kumaliza taabu ya mahitaji ya mawasiliano kwa wananchi hawa waliopiga kura nyingi kuichagua Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuwa imani yao ni kubwa sana watapata suluhu ya tatizo lako. Naomba kuwasilisha.