Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kupata fursa hii ya kuchangia na kutoa maoni yangu kwenye bajeti hii ya Serikali. Nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Tanzania na Serikali nzima kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani yetu imetekelezwa vizuri mno na kwa asilimia nzuri mno, na nina imani katika kipindi hiki kinachoishia mpaka Juni kwa kweli tutakuwa tumefanya yale ambayo hayakutegemewa kutokana na changamoto za kidunia zilizokuwepo. Wengi hatukutegemea kuwa bajeti hii itatekelezwa kwa kiwango hiki hasa kutokana na vita ambayo imetukumba dunia sasa hivi, pia na ugonjwa wa UVIKO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana vilevile kwa Serikali na Mheshimiwa Rais kwa kuja na hii bajeti. Hii bajeti ni ya kimapinduzi, hii bajeti tunaweza kusema ni ya kimapinduzi au kwa lugha nyingine wanasema transformation budget, imetuonesha mwelekeo mzuri mno na ukiangalia dhima ya mpango wetu ni kujenga uchumi shindani na viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ina maana kubwa mno kwa vile uchumi shindani hatushindanishi mazao yetu au mashirika yetu hapa, lakini tunashindana globally, tunashindana dunia nzima. Kwa hiyo, uchumi wetu tunapouangalia kibajeti, tuangalie sisi je, ni sehemu gani ya dunia ambayo tumeimega na nchi yetu inahakikisha kuwa inakuwa na ushindani ambao ni mzuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hii bajeti, kwa kweli kwa kiasi kikubwa imekidhi. Ukuaji wa GDP imeonesha kuwa katika kipindi cha COVID nchi yetu ilifanya vizuri, lakini hata hiki kipindi tunachokwenda, ukuaji wa asilimia 5.3 ni wajuu kuliko nchi zote za Kusini mwa Jangwa la Afrika. Hiyo rekodi ni kubwa sana ukilinganisha na wastani wa 4% tu ambapo nchi nyingine zote ni 4%, sisi tuna asilimia 5.3. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia vile vile, tunaendelea kuhakikisha uchumi wetu unaendelea kuwa imara. Mfumuko wa bei ambao ni kati ya 3% mpaka 5% na sasa hivi ni chini ya 4%, hiyo ni rekodi nzuri sana. Kwa sababu katika hiki kipindi ambacho mfumuko wa bei duniani ni mkubwa, hata nchi zilizoendelea zimeshindwa kuhimili kuweza ku-contain hiyo inflation yao, lakini unashangaa Serikali yetu chini ya Mheshimiwa Rais, ni maajabu gani wanayoyafanya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia utulivu wa Shilingi, nilikuwa najaribu kuangalia kwa mazoea tulizoea kuona exchange rate ya dola ilikuwa inalingana na bei ya petrol kwenye kituo cha mafuta, lakini leo hii mafuta ni zaidi ya 3,000, lakini exchange rate ni Shilingi 2,300/=. Ina maana Benki Kuu na Serikali kwa jumla wanafanya vizuri mno. Kwa hiyo, hata ile imported inflation nayo bado haijatuathiri kwa kiasi kikubwa. Kwa hiyo, nakushukuru sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, Mheshimiwa Waziri umefanya kazi nzuri sana na timu yako, na nimefurahi zaidi nilipoona bajeti yako imeweka kipaumbele cha kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kinaajiri asilimia 65 ya Watanzania, lakini kilimo kinachangia asilimia 25 tu ya uchumi. Kwa kweli huo uwiano siyo mzuri, haiwezekani Watanzania zaidi ya asilimia 65 wachangie tu asilimia 25 ya uchumi. Hiyo siyo dalili nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza Serikali iangalie, pamoja na bajeti ya kilimo kuongezeka kutoka Shilingi bilioni 294 mpaka karibu Shilingi bilioni 954, ongezeko hilo ni kubwa mno; ni mara tatu. Kwa hiyo, tunategemea mchango wa kilimo uende mara tatu; na ukienda mara tatu nchi hii itakuwa imefika mahali pazuri mno. Mchango wa kilimo ulikuwa mdogo kwa sababu ya ufanisi, lakini tunashukuru kwa mpango aliokuja nao Waziri wa Kilimo, unatuonyesha kuwa unaweza kututoa hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kwa sababu, bila kuhakikisha kuwa kilimo kinatutoa hapa tulipo, nchi yetu itakuwa ni maajabu tukipata hayo maendeleo tunayoyafikiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za kigeni tunazitegemea kutokana na mazao ya kilimo, madini na utalii, lakini zaidi zaidi tunategemea kwenye kilimo. Kwa hiyo, tunaomba nguvu kubwa iende kwenye kilimo. Tunashukuru kwa ruzuku ya mbolea, lakini hii ruzuku ya mbolea iliyooneshwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa 80, kile kiasi alichokitaja mwanzoni na hata alichokitaja Waziri wa Kilimo hakijaonekana. Amezungumzia tu ya kwamba katika kilimo kutakuwa na ruzuku ya pembejeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunakuomba ruzuku ya pembejeo ya mbolea ilenge kupunguza bei ya mbolea zote wanazotumia wakulima kwa mazao ya biashara na vilevile mazao ya chakula. Hiyo itatupeleka mahali pazuri zaidi, kwa sababu sasa hivi commodity prices zinakwenda vizuri sana. na kwasababu commodity prices zinakwenda vizuri, tukizalisha tunahitaji masoko, na masoko yanahitajika ya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba commodity exchange market iimarishwe. Hii itasaidia uhakikika wa masoko ya mazao yetu, lakini unapoimarisha hii, uimarishe pia warehouse receipt finance. Ni muhimu kwa vile zinaenda pamoja. Pamoja na hiyo, tunaomba usajili wa ma-warehouse yote na sheria ibadilike ili kulinda hizi warehouses na hii biashara yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba sana, kuna huu mfumo mpya wa ujenzi wa barabara wa EPC and finance. Huu mfumo inabidi uwe coordinated vizuri kwa sababu inawezekana Wizara ya Ujenzi ikaenda na huu mfumo ikategemea labda ni free lunch, yaani ni kitu ambacho tutapewa bure, Hapana. Huu ni mkopo. Kwa hiyo, tuangalie hii mikopo tutailipa namna gani? Kwa hiyo, zile securities, zile mortgages ambazo tutazifanya, tuwe waangalifu kwa kuangalia nchi za wenzetu walifanya nini mpaka wakaangukia kubaya kwa ajili ya hii mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imetajwa barabara ya Tanzam kipande cha Igawa - Mbeya mpaka Tunduma. Hiki kipande ni muhimu sana kwa ajili ya biashara ya bandari. Naomba sana, inawezekana huu mfumo haujawa tayari, lakini katika hii barabara kuna kipande cha Uyole - Songwe bypass wananchi hawajalipwa fidia mpaka leo. Hebu walipeni fidia wale wananchi tunaposubiri hii mipango. Naomba ujenzi wa hii barabara upewe kipaumbele, na barabara zote za Isionje - Kikondo - Makete nayo ipewe kipaumbele kwani ilishaanza, na ni muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mbalizi - Makongorosi ipewe kipaumbele; na barabara ya Mbalizi - Shigamba ipewe kipaumbele. Vilevile kumalizia ujenzi wa uwanja wa ndege wa Songwe uliopo Mbeya upewe kipaumbele. Hii itaenda pamoja kuhakikisha kuwa mazao yetu yanafika kwenye masoko ya kidunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)