Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia jioni ya leo. Kabla sijaendelea na mchango ambao nimeukusudia unaohusu Jimbo langu, nina jambo la ushauri kwa Serikali ambapo kwenye Hotuba ya Waziri sijaliona, lakini nafikiri ni muda sahihi nami kutoa mawazo yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo jambo moja la Mwenge wa Uhuru. Mwenge wa Uhuru ni jambo jema sana kwenye nchi yetu. Mwenge wa Uhuru unakimbizwa kwa niaba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na Mwenge wa Uhuru unakagua miradi mikubwa yenye gharama kubwa ya fedha za Serikali. Naipongeza Serikali kwa kuendelea kuwekeza nguvu na kuhakikisha Mwenge wa Uhuru unakimbizwa nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kwenye eneo hili nina wazo. Wakimbiza Mwenge wanapokwenda kufungua miradi ile, wanaifungua kwa niaba ya Mheshimiwa Rais. Nafikiri kwa ukubwa na wingi wa miradi inayofunguliwa nchi nzima kwa mwaka mmoja kwa Mbio za Mwenge wa Uhuru ingependeza sana tukapitia upya utaratibu wa kuyaandika mawe yale ya miradi yanayozinduliwa. Ingefurahisha sana! Kwangu binafsi kama kila mradi unaozinduliwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru, kwa maana ile ile ya kupongeza jitihada anazozitekeleza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tungeandika majina yake katika miradi yote ili iwe kumbukumbu kwa kila Kijiji kutokana na nguvu kubwa anazozitoa kuhakikisha kwamba miradi ile inaonekana na Watanzania wote kwamba ni utekelezaji wake yeye mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu nikiangalia hata kwenye Risala ya Utii ambayo anasomewa Mkimbiza Mwenge, inatamkwa, “Mheshimiwa Rais…” Kwa hiyo, ni busara kabisa kwamba na mawe ya msingi pia yanayozinduliwa yakawekwa kwa jina la Mheshimiwa Rais. Hii ni katika kumpongeza na kumpa morali na nguvu na kuendelea kuzitoa pongezi zetu kwake na Serikali yake kwa namna ambavyo anaelekeza fedha nyingi kwenye miradi mikubwa ambayo inatatua matatizo ya wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hili, nirudi kujielekeza kwenye kupitia hotuba hii iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri, nikijielekeza sana mambo ambayo yanagusa Jimbo langu. Nimeisoma Hotuba vizuri, nimemsikiliza wakati anaiwasilisha, kwa kweli nimpongeze, ana kiwango kikubwa sana cha kuwasilisha jambo na kueleweka kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo jambo hasa katika masuala mazima ya Ujenzi na Uchukuzi. Kuna eneo kwenye hotuba ile imezungumza ujenzi wa barabara ya kilomita 158 ya mwendokasi inayotokea Dar es Salaam – Mlandizi – Chalinze hadi Morogoro. Barabara hii ni mpya, inakwenda kujengwa kwa ajili ya kurahisisha usafirishaji kwa watu kuingia kwenye barabara hii ya kulipia na kuwa ni barabara ya mwendokasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nategemea tukiwa tunafikiria kuanzisha miradi mipya mikubwa hasa kwenye sekta hii ya barabara, tungejaribu kuangalia miradi mikubwa ya barabara ambazo zipo kwenye mipango kwa muda mrefu ambazo hazijatekelezwa. Tunapokuwa tunaenda kuanzisha mradi huu, maana yake tunautafutia na chanzo cha pesa cha kwenda kuutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niikumbushe Serikali, upo mradi wa barabara ambayo kila nikisimama naisema, na ninaisema kwa sababu naiona iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tangu mwaka 2005; barabara ya kutoka Makofia – Mlandizi, Mlandizi – Mzenga, Mzenga – Mwanarumango mpaka Vikumburu. Ni barabara yenye urefu wa kilomita 153. Kwa hiyo, inafanana kabisa na barabara ambayo inafikiriwa kwenda kuanzwa kutekelezwa kwa sasa hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ninayoitaja ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tangu 2005, na kila Ilani inatajwa. Cha kusikitisha, kwenye hotuba ya Wizara husika, barabara hii imetajwa; kwenye hotuba ya Wizara husika ya mwaka 2021 barabara hii ilitengewa na fedha; kwenye hotuba kubwa ya Serikali iliyowasilishwa juzi, barabara hii haipo, inazungumzwa barabara mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii imeshafanyiwa upembuzi yakinifu. Kwa kipande cha kilomita 35 kinachotokea Makofia mpaka Mlandizi kinahitaji fidia isiyopungua Shilingi 9,986,550,000/=, mpaka leo, na upembuzi yakinifu huu umefanyika mwisho kabisa wamemalizia kazi mwezi Kumi mwaka 2018. Watanzania hawa ambao wanaisubiri fidia hii, nyumba zao zinabomoka, wamekaa kwenye nyumba ambazo wanashindwa kuzifanyia ukarabati, hawaelewi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana wengine walipoisikia hotuba wanajaribu kuniuliza, Mheshimiwa Mbunge, hebu tuulizie kwa Waziri, kama wanaanzisha wazo la kutengeneza barabara mpya ya kilomita 158 zinazopita kwenye Jimbo hili hili la Kibaha, iweje sisi ambao tulishafanyiwa upembuzi yakinifu iwe hatuna chochote tunachokipa? Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri, kama wamesahau kuizungumza, namwomba sana, kwa faraja ya watu wa Jimbo la Bagamoyo, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na Kisarawe, ni vyema Serikali ikaja na tamko kwenye eneo hili ili watu hawa wajue nini kinafuata baada ya muda mrefu kupita?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye hotuba ambayo Waziri amesoma, sisi kwenye utekelezaji wa Serikali tuna mambo mawili makubwa tunaenda nayo. Kwanza kuna dhima ambayo inaonekama kwenye mipango ya Serikali; kwenye Mpango wa Miaka Mitano wa kuanzia 2021/2022 mpaka 2025/2026.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023 tunayo dhima ya bajeti hiyo. Hizi dhima mbili ukiziangalia, zote zina lengo la kukuza uchumi, kuondolea wananchi umasikini na kuwaongezea watu maisha bora katika maeneo wanayoishi. Wizara imeweka wazi kabisa, imebainisha vipaumbele ambavyo wanakwenda kuvifanyia kazi; kilimo, mifugo, uvuvi, nishati, uwekezaji na biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kuzungumza kwenye eneo hili, lazima tunapokwenda kufikiria kuwaongezea watu uchumi wao, lazima tuanze kutafakari pale ambapo watu hawa wapo, pale ambapo watu hawa walikuwepo na wapi tunataka tuwapeleke kwa sasa? Ukiiangalia bajeti ya Serikali, inajielekeza kwenye kufikiria kuchimba mabwawa makubwa, kutafuta mbolea na kutafuta mbegu bora. Ni lazima tujiulize, wakulima hawa tunaowafikiria kuwapelekea mambo haya, changamoto zao za kawaida za asili ambazo zinawakabili, ni kiasi gani Serikali imezielekezea nguvu kwenye kuzitatua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano wa changamoto moja nyepesi kabisa. Kwenye hotuba hapa, Waziri ametambua, naomba ninukuu kidogo mistari michache sana. Amesema, “kwa ardhi, maji na watu tulionao ni jambo la aibu kwa Tanzania kulia shida ya ngano, shida ya mafuta ya kula kwa sababu ya vita ya Ukraine na Urusi.” Sasa kama tunatambua haya, lakini hawa wananchi ambao wanalima kienyeji, kwa kilimo cha zamani kabisa, cha jembe la mkono, tunawafikiaje? Tunawezaje kwenda kuanza nao pale? Ili uweze kumfikisha mtu mbali, kaanze naye pale alipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijaona mpango mkakati wa Serikali kuwashughulikia wakulima wadogo wenye jembe la mkono. Wanamtoaje kwenye jembe la mkono kumpeleka kwenye jembe ambalo anaweza akazalisha ili afikie malengo makubwa ambayo Serikali inayafikiria? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia, wamezungumzia masuala mazima ya kuchimba mabwawa; leo hii tunavyo vyanzo vya maji, nao wamevitambua. Kuna Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa, mito mikubwa kama Malagarasi, Ruvuma, Rufiji, Mara, Pangani, Ruvu na kadhalika. Mito hii ipo. Kabla hawajaanza kufikiria kuchimba mabwawa makubwa, wana mkakati gani wa kuyatumia maji haya ambayo tayari yapo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza kutafuta fedha za kuchimba mabwawa, wakati huo huo vyanzo hivi vya maji ambavyo vinasimamiwa na Bodi za Maji wameweka taratibu ngumu za wananchi kuyatumia. Sasa tunajichanganya wenyewe. Huku unatafuta kuchimba bwawa la maji, huku una mto umeutambua, una ziwa unalolitambua, lakini maziwa yale na mito ile wananchi ambao wamepakana nayo kando kando kama Mto wa Ruvu watu wanashindwa hata kumwagilia kwa masharti magumu yaliyopo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ndiyo maeneo ambayo tunafikiri eti ndiyo tunamsaidia mwananchi.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)