Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Bajeti hii Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, bajeti hii ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Shilingi Trilioni 41.48 kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023 inaleta matumaini makubwa sana, italeta mapinduzi kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa maono haya makubwa ya kuwaletea Watanzania bajeti inayoleta matumaini makubwa. Nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri wetu wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri na timu nzima kwa kazi nzuri wanayofanya pamoja na taasisi zilizo chini ya Wizara hii kwa kusimamia sana sera za kifedha na za kiuchumi, pamoja na changamoto ya mfumuko mkubwa wa bei hapa duniani, kwa kweli kwa nchi yetu mfumuko wa bei upo katika wigo wa Afrika Mashariki, kwa hiyo wanafanya kazi kubwa wenzetu hawa tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii ukiangalia imejielekeza sana kwenye sera za uzalishaji. Kwa mfano, Wizara ya Kilimo tumetenga bajeti kuanzia Bilioni 294 mwaka 2021/2022 hadi Bilioni 954 kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 ni hatua kubwa sana tuwapongeze sana wenzetu upande wa Serikali. Wizara ya Uvuvi na Mifugo bajeti imetoka Bilioni 168 kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 hadi Bilioni 268 ongezeko la Bilioni 100 ni hatua kubwa sana na hii sekta muhimu sana katika nchi yetu. Hatua mbalimbali za kikodi zilizopendekezwa pia zinaonekana kabisa kupanua wigo wa walipa kodi na kupunguza mzigo kwa walipa kodi wachache hapa nchini. Ili kufikia makusanyo haya tunayotarajia Bilioni 41.48 naomba nishauri katika maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni mifumo ya ukusanyaji mapato iliyoko chini ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), eneo la pili nielekeza kwenye coordination ndani ya Serikali katika utekelezaji wa miradi mbalimbali. Dunia ya leo ni dunia ya TEHAMA na Tanzania siyo kisiwa lazima tukubaliane uhalisia kwamba sasa mawasiliano na biashara zote ziko kwenye TEHAMA. TEHEMA imerahisisha maeneo mbalimbali kwenye ulipaji na ukadiliaji wa kodi ni lazima tuelekeze kwa kutumia mifumo, ili kutokupoteza makusanyo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TRA ina mifumo ya high tax ambayo iko ndani ya kodi za ndani, kuna mfumo wa TANCIS ambao upo Idara ya Forodha na Ushuru wa Bidhaa, lakini kuna e-filing ambayo inatumika kwenye kodi la ongezeko la thamani (VAT). Changamoto iliyopo kwenye mifumo hii yote ni kwamba haisomani, ndani ya taasisi moja muhimu ya kukusanya mapato ya nchi mifumo haisomani, kwa hiyo niombe sana Wizara ya Fedha na Mipango kuiwezesha Mamlaka ya Mapato Tanzania ili mifumo yote iweze kusomana kusiwe na mwanya wa kupoteza mapato ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo ni muhimu sana ikasomana ili endane na wakati, lakini manufaa ya mifumo bora inayosomana ni kama ifuatayo: -

Moja ni kupunguza muingiliano baina ya Maafisa wa Kodi, na Wafanyabiashara na hivyo kupunguza mianya ya rushwa katika nchi yetu. Faida ya pili ni kupunguza mapingamizi ya kodi yanayotokana na ukadiliaji tukiwa na mifumo bora hata assessment zinatoka kwa ubora kwa hiyo utapunguza mapingamizi ya kodi kwenye Bodi za Rufaa pamoja na Mahakama za Rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni kurahisisha ulipaji wa kodi, kwa hiyo tukiwa na mifumo bora inayosomana itarahisisha ulipaji wa kodi na kupunguza usumbufu wa Watanzania na Wafanyabiashara, wetu kwa hiyo kuna haja kubwa sana ya mifumo hii kuwezeshwa ili makusanyo yetu yakusanywe kwa manufaa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunganishe hili na Idara ya Forodha na Ushuru, Idara ya Forodha na Ushuru wa Bidhaa inachangia zaidi asilimia 40 ya mapato yote ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), lakini changamoto kubwa iliyoko kwenye idara hii sasa ni kukosekana kwa Cargo Scanners. Kamati ya Bajeti ilifanya na ziara katika mpaka wa Namanga tumekuta hakuna Cargo Scanners lakini ukienda Tunduma, Holili, Sirari kwenye eneo hili tumepoteza mapato makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukipata hii bila kuwa na Cargo Scanners ni vigumu kutambua bidhaa gani zinaingia nchini kwa hivyo kutokupata makadirio sahihi ya kodi katika maeneo haya. Kwa hiyo niombe sana upande wa Serikali wawekeze kununua Cargo Scanners kwa mikakati mikubwa ili tuweze kuboresha makusanyo ya kodi katika Taifa letu. Tunalenga kupata hiyo bilioni 41 bila kuwa na mifumo sahihi itakuwa ni ngumu sana kufikia malengo haya. Kwa hiyo niombe sana wizara iweze kufanya nguvu kubwa ili tuweze kukusanya makusanyo makubwa katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni uratibu wa bajeti za Wizara, tunapanga mipango mizuri sana na bajeti nzuri sana, lakini bila kuwa na Wizara zetu kusomana itakuwa ni vigumu sana katika kuteleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika Taifa yetu. Kwa mfano, Wizara ya Kilimo kwa mfano inapoandaa miradi mbalimbali ya umwagiliaji na kadhalika je inahusisha Wizara ya Ujenzi ambayo itahusika na ujenzi wa barabara kufikia maeneo haya ya uzalishaji, je, inahusisha Wizara ya Nishati, inayohusika na miundombinu ya umeme? Kwa hiyo, tunapoandaa mipango na bajeti yetu ni muhimu sana kukawa na coordination baina ya Wizara zetu ili kuweza kuweka tija na kuweza kutekeleza miradi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili bila coordination ama tunachelewa au tunakwamisha kutekeleza miradi mbalimbali ya wananchi wetu kwa hiyo niombe sana wenzetu upande wa Serikali kuwe na coordination ili tuweze kutekeleza bajeti zetu kwa pamoja. Tunapokosa coordination baina ya Wizara idara na Taasisi inachelewesha miradi lakini tungekuwa tunawasiliana tungepunguza gharama na pia tungerahisisha utekekelezaji wa miradi mbalimbali na kuwa na tija katika Taifa letu, kuna umuhimu mkubwa sana wa coordination ndani ya Serikali ili mambo haya yaweze kufanyika kwa wakati na kwa manufaa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nashukuru sana kwa fursa, naunga mkono hoja. (Makofi)