Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa fursa hii ya kuchangia kwenye mpango na Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka 2022/2023. Awali ya yote nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan na Serikali yake kwa kuja na bajeti nzuri ya kimkakati, na mikakati iliyopo ndani ya bajeti hiyo inaendana na nyakati tulizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiisoma bajeti Kuu ya Serikali, ukatazama namna ambavyo Serikali inaenda kupunguza kodi, namna ambavyo Serikali inaenda kuwekeza kwenye miradi ya kimkakati, utaona moja kwa moja kwamba taswira na umbile la bajeti hii ni taswira ya kwenda kufanya economic recovering kufuatia kuanguka kwa uchumi wa Kitaifa na Kimataifa kulikosababishwa na mambo makubwa mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza likiwa, kuanguka na kudorora kwa uchumi kulikosababishwa na mlipo wa ugonjwa wa Covid-19 mwaka 2019 ambapo madhara yake tunayapata mpaka leo. Jambo la pili, mdororo wa uchumi na changamoto tunazopitia leo hii zinafanana na zile za mwaka 1979 na 1980 ambao ulisababishwa na mapinduzi ya kule Iran ya wale Ma-shaah wa Iran ambapo mafuta kutoka Iran hayakuweza kuingia kwenye Soko la Kimataifa kirahisi na hivyo gharama za mafuta kwa maana ya force refuels zika-double.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sasa hivi pia kumetokea mgogoro baina ya nchi ya Ukraine na Urusi ambapo hususan Urusi ni nchi ya pili kwa uzalishaji mkubwa wa mafuta na ni nchi ya kwanza kwa uzalishaji wa gesi. Kwa maana hiyo, kudorora kule kwa uchumi tunakokupata sasa hivi na kupanda kwa bei za mafuta kumesababishwa na mgogoro huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya changamoto za kiuchumi zilizotokea mwaka 1980 ama ukitazama changamoto za kiuchumi zilizotokea mwaka 1930 na miaka iliyofuatia kufuatia the great depression, utaona sera za kiuchumi ambazo Serikali za nchi mbalimbali zilichukua zilikuwa ni za supply side economics, kwa maana ya sera ambazo proponents wake ni wachumi kama akina John Bernard King ambao walikuwa wanazungumzia kwanza kuhusu Serikali kuongoza uchumi kwa maana ya kufanya Government intervention na kuachana na sera za kwamba Serikali haitoshikilia chochote kwenye uchumi, itauacha uchumi wenyewe ujiendeshe na mwisho wa siku kimbunga kikipita basi bahari itatulia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sera hizi ninaziona moja kwa moja kwenye bajeti hii ya mwaka 2022, na pia naziona sera hizi kwenye mchakato mzima wa kuendesha uchumi wa Taifa letu katika kipindi cha mwaka mmoja cha uongozi wa Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, ambapo mambo yanayofanyika ni pamoja na kwanza kupunguza viwango vya kodi. Tumeona kodi zimepunguzwa maeneo mengi, na la pili ambalo tunaliona ni kuendelea kutekeleza miradi ya kimkakati kwa maana ya kwamba Serikali inaachia fedha ilizonazo, inazipeleka kwenye jamii kwa kutekeleza miradi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, tunaona Serikali ikichukua mikopo kutoka sehemu mbalimbali na hata sasa hivi ukisoma hotuba ya Bajeti ya Waziri wa Fedha na mipango, unaona tayari wako katika negotiation ya mkopo wa zaidi ya Shilingi trilioni moja kutoka Benki ya Dunia. Wapo katika negotiation ya mkopo wa zaidi ya Shilingi trilioni mbili kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), lakini na pia unaona zile fedha za shilingi trilioni 1.3 za UVIKO ambazo zote zinakuja kuingia katika uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kuishauri Serikali iendelee katika trajectory hiyo hiyo, wasisikilize kelele za watu wanaosema tunakopa sana kwa sababu hao hawawatakii mema wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwanini nalisema hili, anasema, John Bernard King kwamba katika zama kama hizi ambapo unataka kuchochea ukuaji wa uchumi kufuatia mdororo, ni lazima Serikali iingilie, ni lazima Serikali ichukue hatua za muda mfupi, hatua za dharura za kuwakomboa wananchi wa kipato cha chini dhidi ya ukali wa maisha unaosababishwa na mdororo wa kiuchumi. Hatua zenyewe ni pamoja na kuhakikisha tunaongeza ajira kwa kuongeza uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila Rais wetu na Serikali yake kutoka nje, kuboresha mahusiano ya Kimataifa, kurudi ndani kuboresha mifumo na misingi ya utawala bora, hatuwezi kukopesheka, hatuwezi kuvutia wawekezaji kutoka nje kuja kuwekeza katika uchumi wetu, na hatimaye kuzalisha ajira, kuzungusha fedha katika mzunguko wa uchumi wetu, na mwisho wa siku tutaanguka vibaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kuwaambia Serikali kama ambavyo alifanya Ronald Regan miaka ya mwanzo ya 1980 na sera zake zikajulikana maarufu sana kama Reganomix na ambazo mimi pia nimezifuatilia kwa ukaribu na nimeandika katika kitabu changu cha Kigwanomix, napenda pia kuendelea kuwaomba watu wa Serikali wakae katika mtiririko huo huo wa kutanua uchumi wetu kwa kufanya uwekezaji lakini pia kuboresha mahusino ya Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi hatua zote ambazo zinachukuliwa na Mheshimiwa Rais nimeziweka katika makundi 10. Ukizitazama kwa undani wake unaweza ukaziita Samianomix kama ambavyo kule Marekani mwaka 1980 waliziita sera za Rais wa wakati huo Bwana Ronald Regan, Reganomix. Kwa hiyo, nami napenda kuzitaja hatua ambazo zinachukuliwa ni pamoja kupunguza viwango vya kodi, kufuta baadhi ya mipango isiyo na tija kama hii ambayo ameisema Waziri wa Fedha wakati anasoma bajeti yake; kupunguza magari, lakini pia gharama za kusimamia magari ya watumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ya tatu, kupunguza matumizi ya Serikali kama ambavyo tunaona Waziri wa Fedha alipohutubia, kupunguza riba kwenye benki zetu kama ambavyo tunaona kwenye benki katika kipindi cha Mheshimiwa Mama Samia, baadhi ya benki zimeshusha viwango vya riba mpaka asilimia tisa. Pia kuendelea kukopa mitaji kutoka nje ili kuleta katika uchumi wetu; sita, kuboresha utawala bora na uhusiano wa Kimataifa kama ambavyo tunaona, Rais ana-reach out kwenye Mataifa mbalimbali, kama ambavyo tunaona Rais ameweza kuitangaza Tanzania vizuri sana kupitia Royal Tour.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa napenda nitoe mapendekezo kwamba Waziri wa Maliasili na Utalii akatazame mkakati ambao tulianza kuufanya kipindi mimi nikiwa pale Wizarani wa kutangaza vivutio vya Utalii kwenye michezo hususan Soka la Ulaya. Hii ni katika mikakati ambayo itaungana na Royal Tour katika kuvutia wawekezaji na wageni kuja kutembelea Tanzania. Ni mkakati ambao utaendana na Samianomix.

Mheshimwia Naibu Spika, la saba ni kutekeleza miradi ya kimkakati kwa kutumia fedha za nje badala ya kutumia fedha za ndani. Kwa hiyo, ni katika ile ambayo ameisema Waziri wa Fedha hapa EPC+F.

Mheshimiwa Naibu Spika, namba nane ni kuendelea kuwekeza kwenye sekta ambazo zinagusa watu wengi ikiwemo sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi kama ambavyo bajeti inasema; tisa, ni kuboresha huduma za jamii kama ambavyo tumekuwa tukifanya; na kumi, kuwekeza zaidi kwenye miradi ya kimkakati kwa mfano miradi ya gesi, aliongea vizuri sana Mheshimiwa Prof. Muhongo, sina haja ya kurudia. Siyo tu kwenye gesi wameanza na LNG plant, waende kwenye miradi ya mbolea ambayo inatokana na gesi, waende kwenye miradi ya madawa ambayo inatokana na gesi, na tukifika hapo, tutakuwa tumeweza kuchomoka katika mtanziko tulioingia kutokana na changamoto nilizozisema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda umeniishia, ningeweza kuongea mengi zaidi. Nashukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)