Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuwa miongoni mwa wachangiaji. Awali ya yote nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada kubwa sana anayoifanya kuwatumikia Watanzania na kupeleka huduma mbalimbali ambazo kila eneo zimewafikia Watanzania. Hata hivyo, yapo ya msingi ambayo kayafanya, amewaongezea mishahara watumishi wa Serikali, ni jambo kubwa sana na bado kwenye sekta ya elimu ametoa elimu bure mpaka kidato cha sita. Kwenye bajeti hii aliyoleta Mheshimiwa Waziri, hili ni jambo la faraja kwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na ushauri kwa Serikali hasa kupitia Wizara ya Fedha kwenye maeneo ya mapendekezo waliyoyaleta juu ya kuhamisha vifungu vya kisheria ambavyo kwenye sekta ya mawasiliano wanainyang’anya Mamlaka ya Mawasiliano TCRA wanapeleka kwenye TBS ambayo hawatakuwa na uwezo wa kufanya kazi hiyo inayokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi na ni vizuri Serikalini wanapokuwa wanaleta mapendekezo wawashirikishe wadau wote kuliko wakijifungia tu wanaleta ya kwao ambayo hayatafanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hilo tu kwenye eneo la sekta ya ujenzi na LATRA wameleta mapendekezo ya kuhamisha baadhi ya mambo ambayo wanapeleka TBS, jambo ambalo si zuri na ni vizuri wakawashirikisha. Hata kwenye Wizara ya Kilimo nako kuna mapendekezo ambayo wameyaleta, wanahamisha shughuli zilizokuwa zinafanywa na mamlaka ya pamba, wanapeleka kwenye TBS. TBS kazi yake ni kutunza ubora na kuhakiki ubora ule ambao umefanywa kwenye eneo la viwanda. Hili naomba Waziri mwenye dhamana aliangalie na a-review kabisa hivi haya mapendekezo ambayo ameyaleta ambayo ukweli kimsingi ukiyafuatilia hayawezi kufanya kazi kama walivyokusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kusisitiza kwenye eneo hilo hilo, ni kumkumbusha Mheshimiwa Waziri TBS kupitia Bunge hili hili tuliwapa mamlaka ya kuhakiki mitambo ya magari na Serikali ikagharamia mtambo karibu wa shilingi bilioni 10 ambao uliletwa na umeshindwa kufanya kazi kwa sababu ya kung’ang’ania shughuli ambazo hawajazifanyia uhakiki ule unaokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite kwenye sekta ya kilimo, kwenye sekta ya kilimo ni sekta ambayo ndiyo inayoweza kukuza uchumi na tuangalie nyakati zinavyokwenda. Sasa hivi dunia nzima ina njaa na tutakuwa na njaa kubwa na sisi kama nchi yetu ni nchi ambayo ina maeneo ambayo tungeyapanga vizuri Serikali ikajikita, tungetatua baadhi ya maeneo na kuwafanya Watanzania wenzetu wakawa na kipato kikubwa sana na nchi ikawa na fedha ambazo zingesaidia kufanya shughuli zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna tatizo la ukosefu wa ngano tunajua Ukraine, Rusia kuna vita, Wazungu hawatakuja kuwasaidia Waafrika, ngano yote itabaki kule kule iweze kufanya shughuli za kuwasaidia wenzao. Niombe sasa Serikali ijikite katika kipindi hiki cha mwaka huu wa fedha wahakikishe kwenye maeneo ambayo yana uzalishaji mkubwa na unaofanana na hali ya hewa kama Mkoa wa Njombe, Mkoa wa Mbeya, Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Arusha na hata kwetu Katavi kwenye eneo la Tarafa ya Mwese ni maeneo ambayo yanaweza yakazalisha ngano. Sasa wafanye utafiti wahakikishe wanawawezesha Watanzania kwenye maeneo haya wazalishe ngano ambayo itauzwa hapa hapa nchini na kupunguza fedha zile ambazo tunatafuta za kigeni kwenda kununua ngano nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni la muhimu sambamba na kukuza mazao ya mafuta. Tunayo mikoa ambayo tunazalisha mafuta ya michikichi kwa upande wa Mkoa wa Kigoma na Mikoa ya jirani kama vile Katavi, Tabora hadi Kagera wana uwezo wa kuzalisha michikichi, Wizara ihakikishe inawawezesha hawa wakulima wazalishe ili kuwe na uwezekano wa kuweza kuzalisha mafuta ndani ya nchi yetu. Kwenye zao la alizeti karibu kila mkoa alizeti inastawi mahali pote, wahakikishe wanaandaa mbegu, wanawapa mbegu bora ili wazalishe mazao hayo ambayo yatapunguza kupoteza fedha za kigeni ambazo tunazitumia kwa ajili ya matumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tunaishauri Serikali ni kwenye sekta ya maliasili. Kwenye eneo la maliasili hatujafanya vizuri pamoja na jitihada ambazo zinafanywa na Serikali kuhakikisha tunatangaza utalii kwa nguvu zote na Mheshimiwa Rais amefanya hili vizuri sana, lakini kuna eneo ambalo hawajalifanyia kazi kama Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Nchi za Magharibi au zilizoendelea kwa ujumla zina uchafuzi wa mazingira kupitia viwanda. Sasa maeneo haya sisi kama Taifa hatujatumia fursa aliyopo, viwanda vyote duniani ambavyo vinazalisha na kuchafua mazingira vinatakiwa kulipa gharama za kutunza mazingira. Wenzetu Nchi jirani ya Kenya wanapata fedha karibu dola bilioni mbili kwa mwaka kupitia uvunaji wa hewa ya ukaa ambayo wanaifanya na sisi ambao tupo kwenye maeneo mengi ya misitu hatujanufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri amefanya kazi kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais inayoshughulikia mazingira, analijua ninalolizungumzia. Tanzania wilaya chache tu ndizo ambazo zinavuna hewa ya ukaa. Wilaya ya Tanganyika nilikotoka mimi nina ushuhuda, vijiji karibu 10 vinanufaika, wanapata karibu kila kijiji kwa kipato cha mwaka huu tu wamepata bilioni tatu vijiji na tunategemea wanaweza wakapata karibu bilioni 10. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama tukitoa sheria ambazo tumeziweka zinazoziba mazingira ya kuweza kukusanya fedha hizi kwenye National Park kama Wakenya wanavyofanya, kwenye misitu ambayo ni tengefu, naomba hili walifanyie kazi. Naamini Mheshimiwa Naibu Waziri analifahamu, tukieleza nguvu kwenye hii sekta ya misitu, Tanzania tuna uwezo wa kupata fedha zaidi ya bilioni 400 kwenye misitu tunayoimiliki. Naomba hili walifanyie kazi sambamba na kuchungulia ni mahali gani ambako tunafanya nao biashara, kwa sasa tunafanya na watu wa kati, middle man ambao wapo katikati, hatujawafikia wale ambao wanatoa hizo fedha. Naomba hili Wizara ilifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie eneo la sekta ya miundombinu. Tunapojenga miundombinu hasa barabara nashukuru Wizara ya Ujenzi imekuja na mpango wa kushirikisha sekta binafsi ili waweze kujenga barabara ambazo wata-design, watajenga na watakuwa financier wao, ni jambo lililo zuri. Sasa tuangalie ni barabara zipi tunazoenda kuzijenga, tujenge barabara ambazo zitakuwa na uchumi na zitakazorudisha return ya fedha tulizowekeza. Mfano, tunayo barabara ya kutoka Ifakara kwenda Madete hadi Njombe – Ludewa ambako kuna machimbo ya mkaa na sasa hivi kupitia vurugu ya dunia, mkaa unahitajika karibu kila sehemu. Naomba hili walifanyie kazi, tujenge barabara ambazo zina faida. Barabara nyingine ni ile ambayo inatoka Wilaya ya Mpanda, Mkoa wa Katavi kwenda eneo la Karema ambako Serikali imejenga bandari. Hii barabara waijenge haraka ili washike soko la Kongo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)