Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii nami nitoe mchango wangu kwenye hoja iliyoko mezani. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama jioni hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili naomba niwapongeze, nikianzia na Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri wa Fedha na waandamizi wake wanaofuatana katika kazi hii, kwa kazi nzuri waliyoionesha kwa ajili ya Watanzania. Ama kweli Mama ameonesha kwamba yeye ni Mama, ana uwezo wa kushinda na njaa lakini akampa mtoto wake tonge la mwisho ili aweze kushiba, ili Watanzania waweze kufurahi wote. Hili ndilo alilolionesha katika Bajeti hii ya Mwaka wa Fedha 2022/2023. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza naomba niongelee suala la kilimo. Naishukuru sana Serikali, namshukuru Waziri wetu kwa kurekebisha na kurudisha Export Levy kwa zao la korosho. Naomba kama ilivyokuwa miaka ya nyuma, uzalishaji wetu ulikuwa mkubwa, ulikuwa unaongezeka mwaka hadi mwaka kutokana na mapato ya Export Levy kuhudumia zao la korosho, mpaka tulifika hatua tuyolifikia tani 323,000. Baada ya kuondoa Export Levy ambayo ilianzishwa na wadau, basi zao hili limeshuka mpaka leo hatujafika uzalishaji wa tani 250,000. Naamini kwa kurejesha huku, zao litaendelea kupaa kwenda juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nina mashaka na nina ushauri katika hili, kutokana na uzoefu niliyokuwa nao. Kwenye jambo hili mmestiki sana kwenye Sulphur, lakini Export Levy ina mambo mengi ambayo yanayofanya korosho iweze kukua katika uzalishaji. Moja ya jambo ambalo likuwa linashughulikiwa na Export Levy ni pamoja na kuzalisha miche bora na kusambaza kwa wakulima. Hiyo ni pamoja na kutoa fedha kwa ajili ya usimamizi kwenye Halmashauri zetu. Sasa hivi Halmashauri zinahangaika kusimamia zao la korosho kwa sababu hawana fungu maalum linalofanya waweze kusimamia zao hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na suala la usimamizi, tulikuwa tunajenga maghala. Pale kwetu Tunduru tulianza kujenga ghala, ilitolewa Shilingi bilioni moja, lakini tangu 2015 mpaka leo ghala lile lipo tu kwenye foundation. Naomba fedha hizi zirejee kutengeneza ghala lile likamilke ili katika mfumo wa stakabadhi ghalani tutumie maghala yenye ubora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo Tunduru tu, Mkuranga pamoja na kule Tanga haya Maghala yalianzishwa na yalifikia hatua yaliyofikia. Tunaomba sana kwa kuwa Export Levy hii inarudi tena, basi itumike kuhakikisha yale maghala yanajengwa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kujengwa vizuri, tunaomba sana Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo ihakikishe kalenda ya uzalishaji wa korosho inafuatwa, siyo unatoa fedha mwezi wa Sita ya kununulia Sulphur wakati Sulphur inatakiwa mpaka kufika mwezi wa Tatu na wa Nne iwe imeshafika ili wakulima waweze kuwahi. Kwa hiyo, tusianze tena kuizungusha hii fedha kwa sababu tayari imeshapitishwa kisheria, basi naomba sana jambo hili lizingatiwe ili kuhakikisha kwamba hili zao linaenda mbali kwa sababu linawaleta faida kubwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda nichangie kwenye hilo, ni suala la kilimo cha umwagiliaji. Naishukuru Serikali kwa kuongeza na kutenga fedha kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Ni wazo langu kubwa na kwa kuishauri Serikali, basi tuweke specific area angalau tuangalie maeneo machache ambayo tutatia nguvu kubwa tuweze kuzalisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimebahatika kwenda kuangalia shamba la miwa pale Kagera Sugar, tumeona namna ya mwekezaji yule amejitolea kwa nguvu zake na kuhakikisha kwamba anazalisha na anaweka msimamo wa kumwagilia ili aweze kuzalisha tani 300,000 za sukari. Naomba kwa mtindo ule, wenzetu wa Serikali wakajifunze, tuanzishe mashamba ya mpunga, mashamba ngano na mashamba ya mahindi, kwani yatatusaidia kuhakikishwa kuondokana na tatizo la chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana kwa umwagiliaji ule kama tutaenda kwenye mazao yote, basi tunaweza ku-export mazao mengi nchi za nje kwa ajili ya kupata umwagiliaji wa aina tofauti. Kwa kweli, tabia nchi imetuathiri, uzalishaji wa kutegemea mvua imekuwa ni changamoto kubwa sana. Tuweke mkazo, tuweke nguvu kwenye uzalishaji wa kilimo cha umwagiliaji ili kuhakikisha kwamba tunaondokana na shida ya njaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, wakulima wetu huko vijijini hasa Wilaya ya Tunduru hasa Jimbo la Tunduru Kusini wanaathirika sana na tembo. Kile kile walichokilima vyote vinaondoka. Sasa nadhani hawa tembo wana ramani, wana time table ya kilimo hiki cha kawaida. Kama tutaanzisha kilimo kidogo hiki cha umwagiliaji, kipindi cha kuanzia mwezi Julai, mpaka Oktoba mpaka kufika Desemba, hakuna tembo, humwoni kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, basi tusisitize suala la kulima kilimo cha umwagiliaji kwa wakulima wetu wadogo wadogo hasa kule Misaje, maeneo ya Mkotamo, Madaba, kote huko kuna mito na mahali ambapo tunaweza kulima kwa umwagiliaji angalau tukakwepa hawa tembo wanaokuwa na tabia ya kuweza kwenda kuvamia mazao ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye suala hili la Export Levy naomba tujenge maghala kwenye vijiji vyetu. Tunapokwenda na Mfumo wa Stakabadhi Ghalani naomba mtembelee muone hali ya vijiji hivyo jinsi ilivyokuwa. Naomba fedha zitengwe kwa ajili ya kujenga maghala kwenye vijiji vyetu yasaidie kwenye Mfumo wa Stakabadhi Ghalani.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kumshukuru Rais wetu, ni suala la kutoa elimu bure kwenye Kidato cha Tano na cha Sita. Pamoja na changamoto ambayo sisi Wabunge, hasa mimi katika Jimbo langu ilikuwa na kila mwaka nalipa takribani Shilingi milioni mbili mpaka tatu kwa ajili ya kulipia ada Kidato cha Tano na cha Sita. Kwa hili Serikali kweli wametusaidia, nami angalau nitapumua kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ila changamoto tuiangalie, kuna wazazi washalipa full, Five na Six, fedha iko benki kwenye shule za sekondari. Sasa tuweke utaratibu, kwa sababu mwaka wa fedha huo haujafika na mtu alilipa advance, basi mtoe maelekezo, wale ambao tayari walishakuwa wamelipa basi tuone namna ya kuweza kuwafidia, kwa sababu mwaka wa fedha wao ulikuwa bado haujafika, Kidato cha Tano ndiyo kwanza kimefunguliwa. Malalamiko hayo yapo kwenye maeneo mengi tuhakikishe wale wazazi wanarudishiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie kwenye hili tumeacha sehemu moja ambayo tulitakiwa tuiangalie. Kila Tarafa tuweke High School. Jambo la kujenga madarasa 12,000 ya sekondari limeongeza idadi ya wanafunzi kwenye shule za sekondari kuanzia Kidato cha Kwanza mpaka cha Nne, lakini bado hatujaangalia wakimaliza Kidato cha Nne hawa wanaenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iangalie uwezekano wa kila Tarafa kuweka High School ili kuwapunguzia wazazi mwendo mrefu wa kuwapeleka watoto kutoka Tunduru kwenda Tabora, mwingine kwenda Bukoba, ambapo nauli yao ni mara tatu au mara nne ya ile ada ambayo tumeiondoa. Naomba sana kwenye jambo hili tuliangalie kwa hali ya juu na kwa huruma kwa sababu walio wengi waliosoma kwenye shule hizi za Sekondari za Kata ni wakulima ambao uwezo wao ni mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tujitahidi sana miaka ijayo tuangalie namna ya kuweza kuweka at least kila Tarafa iwe na High School ili watoto wetu waendelee kusoma mazingira yale yale yatakayosaidia wazazi wetu kwa ajili ya kuondoa gharama za maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi hii. Naunga mkono hoja. (Makofi)