Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi ya kuweza kuchangia katika mpango wa mwaka 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuipongeza Serikali kupitia Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya haswa ya kuendelea kuisimamia miradi mikubwa katika nchi hii ambayo inaendelea kutoa fursa kubwa na kuendelea kutanua fursa kwa asilimia zaidi ya sabini kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nje ya kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania niwapongeze sana Mawaziri, Waziri wa Fedha, Waziri wa Mipango kwa mpango huu wa mwaka 2024/2025. Naomba sasa niende kwenye mchango wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mipango hii iweze kwenda na ili mipango hii tuweze kuhakikisha inaweza kufanikiwa, kwanza kabisa lazima tujiwekeze katika miundombinu ya umeme katika nchi hii. Bwawa la Mwalimu Nyerere linakwenda kuifungua nchi, lakini Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuhakikisha inaendelea kuleta miradi mikubwa katika nchi hii ambayo yote inahitaji umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere peke yake hauwezi kuja kutosheleza bado tunahitaji tuendelee kuweka fedha nyingi za kuhakikisha tunaendelea kutengeneza njia nyingine za kuweza kuvumbua umeme ili uweze kuwa suluhisho la matatizo na changamoto kwa Wananchi wa Tanzania na hususan vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia namna ambavyo umeme unakuza pato, kukatika kwa umeme ni hasara kubwa katika nchi. Kwa sababu, wapo watu wa welding ambao ni vijana wanategemea, wapo watu wa ice cream wanafunga huko wanategemea. Kwa hiyo, umeme unagusa watu wadogo na watu wakubwa. Unagusa viwanda vidogo na viwanda vikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima katika mpango tuendelee kuhakikisha watu wa nishati na haswa kwenye umeme wanatengewa fedha na umeme mwingine unaendelea kuibuliwa ili kutatua kero ya umeme katika nchi yetu na kuweza kuhakikisha hakuna siku inayosababishwa na kukatika kwa umeme mapato ya nchi yanapungua katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili nijielekeze kwenye JKT. Hapa niongelee masuala ya kilimo, kwanza ninaishukuru sana Serikali kama kijana wa Kitanzania, kwa kupitia JKT kuwatengeneza vijana wetu katika uzalendo lakini kuwatengeza vijana wetu katika kupata ujuzi wa stadi za maisha za kuja kuweza kujipatia kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatumia gharama kubwa sana na vijana hawa wanakaa kwa miaka mitatu kambini. Wana ujuzi mkubwa mno ambao sisi wenyewe Serikali tumewaweka katika uzalendo lakini katika ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Kilimo kwa ule mpango wa BBT. Mpango wa BBT, JKT wengi kupitia mazao ya mnyororo wa thamani, kilimo cha JKT wangeweza kuwatumia vijana wale wanapomaliza baada ya miaka mitatu leo tungetemea JKT sio sehemu tu ya kulima bali tuone sasa JKT inaenda kuwa na viwanda vidogo vidogo ili kutoa ajira kwa vijana wale ambao tayari kwa miaka mitatu tumewapa study na skills za maisha ambazo wanaweza kabisa kusaidia nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kama asilimia 40 tu ya vijana wanaotoka JKT ndiyo wanaoweza kuajiriwa kwenye vyombo vingine vya ulinzi na usalama lakini karibu asilimia 60 inarudi nyumbani na tayari tumewapa skills za maisha. Sasa ni lazima tuondokane na mazoea ama kukariri ama kutumia tu kanuni zile kwamba, ni kwa mujibu wa sheria na wakimaliza waende nyumbani lakini tuna uwezo wa kuwatumia kama ambavyo BBT imeweza kutoa ajira zaidi ya watu 800. Tayari tuna rasilimali na nguvukazi hii ambayo tayari ina nidhamu, ina weledi na inajua inafanya nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, BBT imefanya vizuri sana lakini kila mkoa una vijana katika nchi hii, mradi huu ukiweza kuongezewa nguvu na ukaenda kila mkoa ili kuweza kurahisiha mradi huu kwa kule mikoani utawasaidia vijana wengi katika nchi yetu ya Tanzania na haswa nikiuchukulia mfano Mkoa wangu wa Manyara, hauhitaji kusubiri uweke miundombinu ya maji bali mvua zenyewe za msimu zinakuja mara kwa mara na kwa wakati na tuna uwezo wa kufanya uzalishaji mkubwa na ukawa na manufaa katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la chumvi. Tumekuwa na chumvi nyingi sana katika nchi yetui ya Tanzania na haswa nikitolea mfano Mkoa wa Lindi. Ipo chumvi kule ya kutosha ambapo Waziri wa Viwanda, tungeweza kui-process kuweka viwanda vidogo vidogo ingeweza kusaidia Watanzania wasinunue chumvi inayoandikwa imetoka nchi fulani wakati ndani ya nchi yetu tuna chumvi ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano wa wilaya ninayotoka, Wilaya ya Hanang. Kwa mwaka mmoja inazalisha zaidi ya tani 35,000 za chumvi; hiyo ni kwa kutumia local kabisa huko chini (njia za kawaida kabisa za kienyeji) lakini tunatarajia Waziri wa Mipango uone namna gani aidha tunapata wawekezaji wakubwa. Pia, kuna wawekezaji mle ndani wadogo wadogo wakawezeshwa ili kuweza sasa kwa sababu tukipata vyombo vya kisasa, maana yake kwa mwaka tuna chumvi zaidi ya tani 70,000. Tutaendaje kununua chumvi kutoka nchi nyingine wakati ndani ya nchi yetu tuna uwezo kabisa wa kutengeneza viwanda vidogo vidogo, na kuwatafuta wawekezaji. Lakini nje tu ya kuwa na chumvi ya Tanzania bali ni kutoa ajira kwa vijana, kina mama na wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuendelee kuliona hili kwa mapana yake, kwa ukubwa wake. Zile rasilimali ambazo tunazo tukaweza kuzitengenezea viwanda vidogo vidogo na kutafuta wawekezaji na tukaweza kufanya vizuri zaidi na kuingiza mapato katika nchi yetu. Fedha za Kitanzania lakini pia za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ya Tanzania imebarikiwa sana. Hapa naomba niongelee upande wa mashamba na ninaomba nijikite sehemu ambayo ninaifahamu vizuri, sehemu ambayo ninayotoka. Kule Hanang kuna shamba la Basutu. Shamba la Basutu kwa sasa hivi mwekezaji ana takribani ekari 40,000 ambazo zimeanza uzalishaji lakini katika ekari 40,000 ni ekari 22,000 ambazo ameweza kuzilima na ekari 18,000 zimebaki kama msitu. Nini ambacho ninataka kukiomba? Serikali ya Wilaya kwa maana ya halmashauri inategemea shamba ambalo ni ekari 9,000 ambalo halmashauri inalimiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa fedha zile za halmashauri zinaingiza mapato kwenye halmashauri na mchakato wa fedha hizo ndiyo unaotumika katika mgao wa asilimia nne kwa wanawake, nne kwa kinamama na mbili kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali katika mpango wenu shamba lile la ekari 9,000 libaki kwenye halmashauri ili halmashauri iendelee kuingiza kipato kwa sababu mpaka sasa hivi inatumia karibu shilingi bilioni moja kujiingizia kipato. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali kwamba, kwa upande wa wawekezaji tumwangalie kwanza mwekezaji wa kwanza ekari 40,000 kazilima ekari 22,000 na ekari 18,000 zimebaki hazina kazi sasa tuchukue tena ekari 9,000 tuwape tena wawekezaji? Hebu niombe kwanza study nzuri ifanywe kwa huyu mwekezaji wa kwanza tuone anatuingizia tija gani katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kengele imegongwa lakini niendelee kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kupitia Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anatupambania vijana. Ukiangalia kwenye elimu, miundombinu mikubwa ambayo inaendelea kutengenezwa kwenye nchi hii vijana ndiyo nguvu kazi ambayo inatumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)