Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami nianze kuchangia hoja hii kwa kuanza kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba na timu nzima ya Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini nigusie tu kwamba tunayo barabara yetu inayotoka Hydom kuja Katesh. Ile barabara inategemewa sana na wana Hanang na Watanzania. Pia ile barabara ukifika Katesh inaunganisha na Nangwa - Gisambala - Nkondoa ni barabara muhimu sana kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, Hanang ukiacha kuwa wanalima sana mazao mbalimbali ikiwepo ngano na ndiyo kitovu cha uzalishaji wa ngano kwa Taifa hili, lakini pia tuna kiwanda cha cement ambacho kiko kwenye utaratibu wa kuanza, na pia tuna kiwanda cha chumvi ambacho kiko kwenye utaratibu wa kuanza. Kwa hiyo, barabara hizi zikitengenezwa zitatusaidia sana kusafirisha bidhaa hizo muhimu kwa Taifa letu na itakuwa ni hub ya kuilisha Dodoma ambako ndiyo Makao Makuu ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, vilevile tuna barabara ambayo inatoka Kibarashi inakuja mpaka Kijungu – Kibaya – Kijoro; barabara hii inakuja mpaka Dalay – Mbicha. Kwenye mpango wa Taifa ambao tumeupitisha hapa Bungeni na bahati nzuri ninao hapa, barabara hii inapita Kondoa, baada ya Kondoa inaenda Singida. Ila kwenye mpango ambao Mheshimiwa Waziri ameuleta sasa, barabara hii amei-divert, badala ya kupita Kondoa, yeye anataka ipite Chambalo, ipite Chemba baada ya hapo iende kwa Mtoro halafu Singida.

Mheshimiwa Spika, barabara hii inategemewa na watu wengi, barabara hii tumeinadi kwenye ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Wana-Hanang nimewaambia, wana Kondoa vijijini wameambiwa wana-Kondoa Mjini wameambiwa, maeneo mbalimbali watu wameambiwa kwamba hii barabara inakuja kutengenezwa.

Mheshimiwa Spika, barabara hii iko kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, iko kwenye ukurasa wa 73. Sasa kama iko kwenye Ilani, pia iko kwenye mpango wetu wa miaka mitano 2021/2022 - 2025/2026. Nini kilichotokea hapa katikati hii barabara ikabadilika? Mheshimiwa Waziri mimi niseme wazi, hii barabara inategemewa na watu wengi, na watu wameweka matumaini huko. Hayo mabadiliko mnayoyafanya sasa, watu hatuyatambui, ni mapya, hatuyaelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwa niaba ya wana-Hanang, wana-Manyara wana-Kondoa tunaomba utupe ufafanuzi, nini kilichotokea? Kwa sababu haipo kwenye mpango, haipo kwenye Ilani, kama itabaki hivi ilivyo ndugu yangu Mheshimiwa Waziri wewe ni mtani wangu, kwa hapa hatuko pamoja. Hapa hatuko pamoja, naomba hili niliweke wazi kabisa. Hili lirekebishwe. Naamini ni makosa madogo ya kiuchapaji, siyo ya kimpango. Makosa haya ya kiuchapaji yarekebishwe ili yale matumaini ambayo Watanzania wameyaweka hapo yaendelee kubaki kama yalivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusemea hili suala la barabara, na mara zote napenda kuongea masuala ya barabara, nimefananisha barabara na mishipa ya damu ya mwili wa binadamu, kwa sababu barabara ndizo zinazoboresha uchumi wa maisha ya wananchi. Lazima hapo tupaangalie vizuri.

Mheshimiwa Spika, nichangie kidogo kwenye eneo la ukuaji wa uchumi wa Taifa. Nimejaribu kupitia kwenye hotuba ya Waziri. Ukiangalia, ametupa taarifa, mwaka 2019 chumi za nchi za kusini mwa Afrika zilikua kwa asilimia 3.1, lakini wakati wa Corona mwaka 2000 uchumi ukashuka sana ukuaji wake mpaka -1.7. Baada ya Corona kuondoka mwaka 2021, ukuaji huo ukaboreka ukaenda kwenye 4.5.

Mheshimiwa Spika, kwenye nchi zetu za Afrika Mashariki, ukijaribu kuangalia ukuaji kabla ya Corona mwaka 2019 nchi nyingi sisi tulikuwa 7.0, lakini nyingine zilikuwa 4.8, 9.5, 3.1, 1.8, 0.9. Baada ya Corona kututandika na mambo yakaenda ndivyo sivyo, sisi Tanzania kwa kuwa tulichukua hatua mahususi za kutokufunga shughuli za uzalishaji, za kuhakikisha kila fursa tunayoipata tunaitumia ili kuhakikisha kwamba uchumi wetu haudorori. Tulikua kwa asilimia 4.8, lakini nchi nyingine zote za ukanda wa Afrika Mashariki iliyojitahidi sana ilikuwa kwa 0.6, lakini kuna nyingine zilifanya vibaya kabisa, zilikua kwa -6.6.

Mheshimiwa Spika, baada ya Corona mwaka 2021 nchi nyingi zili-bounce back. Iliyoshindwa sana ilikuja kwenye 0.1 kwenye ukuaji wa uchumi, lakini hiyo kabla ilikuwa na -6.6. Maana yake ni kwamba baada ya Corona yenyewe ule ukuaji wa uchumi wake umeongezeka kwa asilimia 6.7. Sisi tume-bounce back kwa 4.9, ongezeko la asilimia 0.1.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema, ukiangalia sisi baada ya Corona ile gain haijawa kubwa. Wataalam wetu wa uchumi, Mheshimiwa Waziri ukiwaongoza, hapo tunapaswa kufanya kazi ya ziada. Tuangalie ni sehemu gani tunapaswa kuboresha ili tu bounce back kama wenzetu. Kuna nchi ambayo ilikuwa -3.4, lakini baada ya Corona iko 10.9. Maana yake ongezeko lake ni asilimia 14.3. Sisi tunapaswa kujitathmini hapa, sehemu gani tumekosea na nini tukifanye?

Mheshimiwa Spika, nimejaribu kuangalia kwenye suala la ukuaji wa uchumi mwaka 2021, sekta ambayo imeongoza ni sekta ya ujenzi asilimia 13.1. Ni imani yangu kwamba eneo hilo lilifanya vizuri kwa sababu fedha ziliongezwa kwenye eneo la TARURA, shughuli nyingi za uchumi zilifanyika kwenye ujenzi wa miundombinu. Ukiangalia shughuli ambayo Watanzania wengi wanategemea, kilimo imekua kwa asilimia 9.6, lakini ufugaji asilimia 7.1. Ukiangalia ndiyo Watanzania wengi walikoajiriwa.

Mheshimiwa Spika, kwa wastani wa kitaifa, wakulima na wafugaji ni asilimia 65 plus. Kwa sisi wa vijijini ni zaidi ya asilimia 95. Eneo hili tumeongeza bajeti, ni jambo jema, lazima tuangalie namna ya kuhakikisha kwamba inaleta tija ambayo tunaitarajia.

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia maeneo ambayo yamefanya vibaya sana, kuna suala la sayansi, utaalam na ya ufundi. Mheshimiwa Waziri wa Elimu alitueleza kwa kina wakati ana-present bajeti yake na akasema yeye ataweka incentive kwa wale ambao watafanya tafiti zitakazoleta tija na hatimaye atatoa fedha. Naomba kwenye eneo hili, Waziri wa Elimu awezeshwe ili tafiti ziweze kufanyika na hatimaye ugunduzi uweze kufanyika, nchi yetu kwenye eneo hilo tuanze kujitegemea tujitengenezee vitu vyetu na eneo hilo liweze kukua kwa sababu ukuaji wake kwa sasa ni asilimia 0.9. Ila ukiangalia shughuli kubwa ambayo inaajiri Watanzania ni hilo eneo la kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti hii tumependekeza uingizaji wa ngano kutoka nje ya nchi tunapunguza kodi. Kwenye ngano tunapunguza kutoka asilimia 35 kuja asilimia 10. Tufanye maamuzi magumu kama tulivyofanya maamuzi magumu wakati wa Corona, wenzetu wakifunga mipaka sisi tunafanya shughuli, uchumi unaimarika. Tuachane na kupunguza kodi kwenye eneo la shughuli zinazohusiana na kilimo kwa sababu watu wetu wana uwezo wa kulima.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wengi wako vijiweni, wakiamka asubuhi utawaona wanacheza karata, wako kwenye michezo ya bonanza; ile kamari ambayo kila siku mtu anakuwa na shilingi, lakini kila siku inaondoka na bonanza. Twende tukawahamasishe watu waende shambani wakalime, fursa ndiyo hiyo. Badala ya kusema tunapunguza kodi ili tupate mazao zaidi kutoka nje ya nchi, tuna ardhi ya kutosha ya kilimo, hatuna sababu yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata kwenye upande wa kilimo cha miwa, miwa mingi inaharibika lakini kwa nini tupunguze kodi kwenye sukari? Tuangalie eneo hilo. Hayo ni maeneo ya msingi sana kwa Watanzania wetu tukawahamasishe wakalime zaidi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nitaunga mkono hoja baada ya kuwa nimepata ufafanuzi wa barabara niliyoisema, ile ambayo haijakaa sawa sawa.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)