Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo ipo mezani kwetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kuwapongeza wenyeviti wa Kamati zetu hizi tatu za PAC, LAAC na PIC kwa taarifa zao nzuri ambazo wamewasilisha, lakini pia niwapongeze Wajumbe kwa uchambuzi ambao wameufanya kuhusu Ripoti ya CAG. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kwa kutupa taarifa ambazo ni za bayana ya nini kinachoendelea katika Wizara zetu, Serikali za Mitaa na Idara ambazo zinajitegemea, ni ripoti ambayo haina mashaka na uzalendo wa CAG tunaufahamu, kwa hiyo hongera sana Ofisi ya CAG.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda mimi nitajikita sana kwenye Taarifa ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na niendelee kuipongeza taarifa hii kwamba ni taarifa ambayo imeandaliwa vizuri. Imeonesha madhaifu mengi kwenye makusanyo ya mapato ya ndani, imeonesha udhaifu katika udhibiti wa ndani, imeonesha udhaifu katika mfumo wa usimamizi, lakini imeonesha udhaifu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani ambacho kingekuwa imara kingekuwa kinawasaidia Mamlaka za Serikali za Mitaa, lakini pia imeonesha udhaifu wa Sekretarieti za Mikoa katika kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, taarifa hii iko vizuri na sipendi kwenda kwenye takwimu kwa sababu ukisoma taarifa yao kila kurasa wametoa maelezo na takwimu za fedha ambazo zimepotea na hasara ambayo Serikali imeipata.

Mheshimiwa Spika, ningejielekeza kwenye nini tukifanye na hasa kwenye ku…, kwa sababu ukiiangalia hii taarifa kuna mambo kama matatu hivi; kwanza kuna suala la sheria zinazoongoza Mamlaka za Serikali za Mitaa, kuna miongozo yetu, lakini kuna muundo. Mimi nitajikita hapo ili pengine tuweze kurekebisha kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwenye sheria zetu ambazo zinaongoza Mamlaka za Serikali za Mitaa zimetungwa muda mrefu sana, ni muda sasa wa kufanya mapitio au tujiulize je, zinafaa kuendelea hadi sasa? Kuna mjumbe mmoja pale kaka yangu Mheshimiwa Mwambe amesema kwamba sisi ni sehemu ya Madiwani na tunahusika na ubadhirifu unaotokea. Ndugu zangu kwa mifumo iliyopo sasa hivi na miongozo iliyopo sasa hivi hata Madiwani wenyewe hawafahamu kinachoendelea kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi nani anamsaidia Diwani kuifahamu Taarifa ya CAG, nani anamsaidia Diwani kujua final account za halmashauri? Menejimenti inaamua nini ipeleke kwenye Baraza na nini isipeleke, lakini je, hivi kweli inawezekana taarifa za sekta kama kumi hivi Madiwani wakutane siku moja tu kwenye Baraza wazungumzie elimu, wazungumzie afya, wazungumzie maji na wazungumzie nini. Hii mifumo kwa kweli sasa hivi haituwezeshi.

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile ukisoma ile Sheria ya Tawala za Mikoa, Katibu Tawala wa Mkoa siyo mamlaka ya nidhamu kwa watumishi wa halmashauri, yeye ni mamlaka ya nidhamu kwa watumishi wa RS. RAS akienda kwenye Halmashauri pale hata kama atapiga kelele Wakuu wa Idara wataulizana kwani huyu mmemjazia mafuta aondoke zake, kwa sababu hawezi kufanya chochote. Atapiga kelele zake atafanya hivi, anaondoka zake. Mamlaka ya nidhamu ya RAS ni kwa watumishi wa RS tu, lakini wale wa Mamlaka za Serikali za Mitaa siyo wa kwake.
Mheshimiwa Spika, vilevile kuna suala hili la ugatuaji, tuna Sera yetu ya Ugatuaji ya mwaka 1998; je, hiyo ni valid mpaka sasa hivi? Kuna malalamiko yapo kwamba TAMISEMI sasa kumekuwa congested.

Mheshimiwa Spika, kuna malalamiko yapo sasa hivi kwamba kwa mfano Katibu Mkuu Uvuvi akitaka kuandika barua kupeleka kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ni mpaka ipitie kwa Katibu Mkuu, TAMISEMI. Ina maana kwamba tuna Chief Secretary mwingine sasa mdogo, kwamba hatuwezi kupeleka taarifa huko mpaka zipitie TAMISEMI, lakini je, kuna coordination gani kati ya TAMISEMI na hizi Wizara za kisekta?

Mheshimiwa Spika, naomba kwa sababu Mheshimiwa Rais amekuja na 4R hii R ya reform lazima tufanye reform kubwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. Tufanye reform kwenye Regional Secretariat, RC, RAS wawe na nguvu kwenye usimamizi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. Ikibaki hivi hivi tutaendelea kama business as usual na ndiyo maana Mawaziri mnapata shida sana, viongozi wetu wa Kitaifa wanapata shida sana, wanapofika mikoani wanashughulikia isuue ambazo zingefanywa na ma-DC na ma-RC. Naomba tufanye mabadiliko ya hizi sheria. Hizi sheria siyo bible siyo msahafu, tuzibadilishe sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile naomba sasa kwenye mabadiliko haya tuangalie nafasi za Wakurugenzi wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa, isiwe mtu akiteuliwa basi ndiyo huyo Mkurugenzi, Wakurugenzi hawa tuwape mikataba sasa na kuwe na KPI za kuwapima, akimaliza muda wake kama ha-perform basi aondoke, lakini Mkurugenzi akishateuliwa anaona ameula, Akiharibu Kiteto anakuja Nanyamba, akitoka Nanyamba anakwenda Nanyumbu anabadilisha badilisha tu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo lazima ifike mahali sasa tena mimi Mheshimiwa Mchengerwa nakutegemea sana. Wewe ulipoingia TAMISEMI tuna matumaini makubwa sana. Ni mtu wa kuthubutu, hebu kafukunyue hivi vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mamlaka za Serikali za Mitaa sheria nyingine zimetungwa wakati wa Baba wa Taifa tuzibadilishe sasa hivi. Mchengerwa unaweza na timu yako, kafanye mabadiliko ili tuwe na strong RS. Mkuu wa Mkoa, Katibu Tawala, akifika kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa haonekani kuwa ni mtu ambaye anaweza kuchukua hatua, lakini anafika pale anapiga maneno kwamba hizo ni kawaida zao. Ni kama mnavyowaambia Mawaziri mmeapa mkienda kwenye Wizara, watumishi wanasema kwamba huyu ni Waziri wa nane mimi huyu, mwenzake alikuja hapa na ukali huu huu, lakini alitulia. Kwa hiyo, twendeni tukafanye hayo mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tuangalie nafasi za wenye viti na mayor wa Halmashauri. Hivi kwa mtindo wa sasa hawa kweli wana uwezo wa kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa? Nani anamsaidia Mwenyekiti wa Halmashauri kuifahamu vizuri Halmashauri yake kwa sababu Mkurugenzi anamficha taarifa muhimu Mwenyekiti wa Halmashauri ili asimsumbue kwenye vikao, anapata wapi zile taarifa? Anapata wapi usaidizi na anakwenda siku mbili tu kwa wiki? Tena siku nyingine anaambiwa leo hakuna gari tutakutumia posho yako huko huko ulipo anasema sawa, basi hafiki Halmashauri. Kwa hiyo, naomba tufanye mabadiliko kama hayo.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, vilevile…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja nakushukuru sana.