Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi ya kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa zawadi ya kukutana siku ya leo. Nichukue nafasi hii kukupongeza wewe kwa heshima kubwa uliyolijengea Taifa hili, Bunge hili na Afrika kwa kuchaguliwa kwako kuwa Spika wa Umoja wa Mabunge yote Duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natamani kama ningepata nafasi ya kusimama kwenye Jukwaa la Mji wa Mbeya kuwaambia watu wa Mbeya kwamba mmeipa Tanzania zawadi njema kabisa, mmeipa Afrika zawadi, mmeipa dunia zawadi ya kiongozi kijana, makini na msomi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado nitasema hivi ndani ya Bunge, nitasema popote nitakapokwenda kwa sababu maandiko matakatifu yananiambia Yesu Kristo alisema; “Atakayenionea haya mbele za watu na mimi nitamuonea haya mbele za Baba yangu.”

Mheshimiwa Spika, unazo sifa mdogo wangu na bosi wangu, endelea Mungu atakubariki, huu ni mwanzo tu wa mchango wako katika ulimwengu tunaoukanyaga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu pia nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu, Dkt. Biteko kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kwa nafasi ya kuwa Naibu Waziri Mkuu. Kwa namna ya pekee naungana na Wabunge wenzangu wote kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi njema anayolifanyia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna mashaka juu ya dhamira njema aliyokuwanayo Mheshimiwa Rais kwa nchi, hii amejitoa kwa hali na mali, ametafuta fedha kwa kukusanya kodi ya wananchi, ametafuta fedha za wafadhili za misaada na mikopo ili kuhakikisha kwamba ustawi wa nchi unapatikana. Nataka niseme wazi, sina mashaka kwamba mafanikio haya ya Mama Samia yana mkono wa Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri waliopo, Makatibu Wakuu pamoja na Makamu wa Rais anayemsadia, lakini yana mkono pia wa Bunge hili lilosimamia fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye mchango wangu na naanza kuwakumbusha vijana na Taifa hili juu ya maneno ya aina ya viongozi wanaopaswa kukabidhiwa dhamana za kutumikia umma katika Serikali na taasisi zingine zilizoko chini ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa 81 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ukurasa wa 103 na ukurusa wa 104 inasema hivi naomba ninukuu: “Kwa hiyo hata katika hali ya demokrasia na ujamaa wakati wote ni muhimu kwa chama na umma kuwa na hakika na anayekabidhiwa madaraka haya ya Serikali maana yakiangukia katika mikono ya wapinga mapinduzi, madaraka hayo yanaweza kutumika dhidi ya maslahi ya umma wenyewe, hivyo chama kuongoza maana yake ni kuhakikisha pia kuwa madaraka muhimu ya Serikali na ya Mashirika ya Umma wanakabidhiwa watu ambao pamoja na uwezo wa kitaaluma…” naomba sana nikazie hapa; “pamoja na uwezo wa kitaaluma ni wenye msimamo wa kizalendo, waaminifu kwa chama na wakulima na wafanyakazi wa Tanzania.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna mashaka kwamba Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Ndugu yetu Kichere inathibitisha pasipo shaka juu ya matumizi mabaya na upotevu wa fedha za umma kwa muda mrefu sana. Sasa kosa liko wapi? Kosa lipo katika upangaji wa safu ya watendaji na viongozi katika Serikali hii yetu. Naomba kusema hakuna namna unaweza kutenganisha uongozi na maadili, kwa sababu maadili ni sifa ya uongozi, lakini siku hizi mkiangalia leo, mkipitia Ripoti ya CAG ya 2021/2022 na mkaenda 2020/2021 na mkaenda 2019/2020 hakuna shaka kwamba waliohusika katika miaka yote hiyo bado ni watumishi walioko katika Ofisi za Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, rai yangu nakusudia kuleta marekebisho hapa ya kuliomba Bunge hili liliridhie na kukuomba wewe uridhie tuunde Kamati Teule ya kuchunguza, kwa sababu tumekuwa tunapokea Ripoti ya CAG, inakuja Bungeni, tunafanya maazimio, sasa baada ya maazimio tunaishia wapi? Lazima tuangalie namna bora ya kufuatilia utekelezaji wa Maazimio ya Bunge na hatua zilizochukuliwa dhidi ya wale ambao wamefanya makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna pekee ni kwa kuunda Kamati Teule ya Bunge itakayokwenda kuangalia ukaguzi wa miaka mitatu, waliotusababishia dosari hizo, wamechukuliwa hatua gani, bado wapo maofisini au wameondolewa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukifanya hivi tutakuwa tumekusaidia wewe, tumeisaidia nchi kuhakikisha kwamba Bunge linatimiza wajibu wa Bunge makini ambalo litaacha rekodi ya kuhakikisha kwamba fedha za walipa kodi zinafika maeneo yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, haivumiliki, haivumiliki kwamba wanafanya maamuzi kama haya KADCO, Bunge lifanye maamuzi, Baraza la Mawaziri linafanya maamuzi, halafu tumelipa na fedha za kununua hisa, bado wanashindwa kukabidhi shughuli za KADCO kwa TAA, kuikabidhi kwa Serikali, tulimlipa nani fedha hizo? Tulifanya uamuzi huo, wewe unayekaidi wewe ni nani wa kukaidi maamuzi ya Bunge na maamuzi ya Baraza la Mawaziri? Naungana wa Wabunge kusema kuna haja ya kuchunguza na kujua ukweli juu ya jambo hilo kwamba nani anajificha hapo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niseme wazi tatizo tulilonalo na ukinzani ambao tunao na wenzetu waliopo kwenye front bench ni vizuri Mawaziri wakajua, viongozi makini hawawezi kuishia kwenye dilemma. Wote, tumekula kiapo kwamba rushwa ni adui wa haki, sitapokea wala kutoa rushwa, cheo ni dhamana, nisitumie cheo changu wala cha mtu mwingine kwa faida yangu. Ziko kwenye ahadi ya mwanachama wa chama chetu na hii ndiyo inatujengea uhalali kwamba chama hiki kimeendelea kuwa mtetezi wa kuaminika wa maslahi ya wakulima na wafanyakazi pamoja na madaraka yao ya uwajibikaji wa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwalimu Nyerere alizungumzia shida ya dilemma ya viongozi wasiokuwa madhubuti kwenye kitabu cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania anasema hivi: “Kifo cha maji kushoto, kulia kifo cha moto, kukubali, kukataa kila moja ni balaa, kote huko hatarini, hujui ufanye nini?” Ninyi mko kwenye dilemma na mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viongozi wako kwenye hatari ya kufanya maamuzi, wanakumbuka ahadi yao ya CCM? Wanakumbuka maamuzi ya Bunge? Wanakumbuka wajibu na hasira ya Rais, dhidi ya Ripoti ya CAG? Kinachonitatanisha kwa nini hawafanani na uso wa Mama Samia siku anapokea Ripoti ya CAG? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ningekuwa Waziri, ningelikuwa Waziri miezi sita hii, hakuna ambaye angebaki aliyetuhumiwa kwenye ufisadi, kwenye Wizara yangu. Hata hivyo, nataka niwaambie wako watu wamefanya ufisadi kuanzia kwenye IPTL na leo wako Serikalini, pamoja na Maazimio ya Bunge, wako watu na nataka kusema ni leo tu nanyamaza, kesho kutwa katika mjadala mwingine nitataja nani wako nyuma ya IPTL, nitataja nani wako nyuma ya ufisadi wa Standard Gauge Railway ambayo manunuzi ya lot one imetugharimu hasara ya zaidi ya trilioni 1.45. Hizo fedha tungegawawi Majimboni, tungegawiwa Majimboni, Zanzibar…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, dakika moja malizia.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, tungegawiwa Majimboni maana yake hata Zanzibar kwa mgao wa kanuni ile ile, wangepata zaidi ya bilioni karibu mia tatu, mia tatu na sisi tungepata katika Majimbo yetu zinazotosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakusudia kuleta marekebisho haya, nimeshayaweka mezani ili tufike mahali tutafute dawa na nitaomba Bunge hili liniunge mkono ili tuweze kuunda Kamati Teule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama nitakuwa sijavunja Kanuni chini ya Kanuni ya 139 ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la mwaka 2023, baada ya CAG kuchunguza habari hizi na kuzileta, nataka kutoa hoja na naomba niungwe mkono kama Kanuni zinaruhusu kwa sababu nimeshaweka kwenye meza, nimempa Katibu wa Bunge kuundwa kwa Kamati Teule ya kuchunguza ufisadi huu na kuweza kutusaidia Bunge hili tuweze kutoka, hii itatenda haki kwa sababu Mawaziri watakuwa hawajaonewa kwa sababu watapata haki ya kujieleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja ya kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge itakayoshughulikia mambo haya. Naomba mniunge mkono kabla sijavunja Kanuni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, siko nayo hii hoja hapa mbele, siko nayo na yeye amewaambia kwamba amekabidhi. Kwa hiyo, pengine wanatazama utaratibu mzuri wa kuitumia, siko nayo hapa mbele. Kwa hivyo siwezi kusema kama imeungwa mkono ama kwa namna gani. (Kicheko)