Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

WAZIRI WA FEDFHA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia. Awali ya yote na mimi nipongeze Taarifa za Kamati na nimpongeze CAG kwa kazi kubwa ambayo ameifanya.

Mheshimiwa Spika, ninapoanza, niwaombe Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania tukubaliane yalikoanzia mafanikio haya makubwa ya leo yameanzia mpaka yamefika hapa, maana naona tulianza pamoja lakini kwenye kuvuna naona kama tunatawanyika.

Mheshimiwa Spika, taarifa hii na hata Watanzania watakuwa mashahidi, imewasilishwa kwa namna tofauti kuanzia kwa CAG na imejadiliwa na Bunge kwa namna ya tofauti.

Mheshimiwa Spika, wengine ambao tumekuwemo humu tumeanzia mbali, tulikuwa wote humu. Kuna mambo ambayo tulikuwa tunayalalamikia na Bunge limesema kwa miaka yote. Wabunge wamelalamika miaka yote na wananchi wamelalamika miaka yote na Serikali ilikuwa inaona lakini ilikuwa haijatoa majawabu ya matatizo yale yanayojitokeza.

Mheshimiwa Spika, mambo yale yalikuwa yapi? Nianze na la kwanza; na Mbunge mmoja alisema pale na wewe ukaunga mkono; kwa sheria tulizokuwa nazo na kwa aina ya ukaguzi tuliokuwa tunaufanya ilikuwa inawezekana kuanzia bajeti inavyopita, mradi unapobuniwa, taratibu za manunuzi zinavyofanyika; taratibu zote zinafanywa lakini mradi unakuwa hauna thamani ya fedha iliyotumika. Hivyo tukasema huku ni kuiba kwa mujibu wa sheria. Lilikuwa linafanyika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa miaka yote CAG alikuwa anakagua compliance, utaratibu wa kiuhasibu tu ndio aliokuwa anakagua CAG kwa miaka yote.

Mheshimiwa Spika, Wajumbe wa Kamati watakumbuka, nilipoteuliwa Waziri wa Fedha jambo la kwanza ambalo Mheshimiwa Rais alilonituma; na bajeti ikiwa imeshafungwa; Bajeti ya CAG inapitishwa na Kamati ya Bajeti, ilikuwa imeshafungwa, imepitishwa ya kutekeleza compliance. Mheshimiwa Rais akasema hapana, hatuwezi tukaendelea na utaratibu wa kukagua compliance, yaani kukagua na kubariki watu wanaoiba kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Rais, akasema nenda kaiombe Kamati, ifungue bajeti ambayo ilishapitisha tumuongezee CAG fedha anazotaka ili aanze kukagua real time, akague value for money. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilienda kuongea na Mwenyekiti wa Kamati nikamwambia hii bajeti mlishaipitisha lakini tunaomba tumwongezee CAG fedha. Nikaongea na CAG akaniambia fedha anazotaka.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, sahani…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Subiri kidogo Mheshimiwa Tabasamu. Mheshimiwa Waziri nikuombe, unapozungumza, ukigeuka nyuma maneno yale hayaingii kwenye Taarifa Rasmi za Bunge. Kwa hiyo jitahidi hapo hapo kwenye kisemeo ili tuyapate hayo maelezo kwenye Taarifa Rasmi za Bunge maana ukigeuka nyuma hatuyapati. (Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, naomba wasinisemeshesemeshe maana nilishashika kasi hapa, waniache niseme ili tuelewane.

Mheshimiwa Spika, ninachosema ni nini; niliongea na CAG,

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA: ...nikamwambia Mheshimiwa Rais anataka aongeze fedha ukague value for money, thamani ya fedha, real time audit, ukague kwa wakati.

SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, kuna taarifa.

WAZIRI WA FEDHA: Nikaongea na Kamati wakaongeza zaidi ya bilioni tano.

SPIKA: Mheshimiwa Nchemba, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam.

TAARIFA

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri anasema kwamba akaongeza pesa katika bajeti ya CAG. Bunge hili ni Bunge linaloendeshwa kwa tamaduni za Jumuiya ya Madola. Je, Jumuiya ya Madola tunatoa asilimia ngapi kuipa bajeti Ofisi ya CAG, aeleze umma wa Watanzania maana anapewa ela ndogo kiasi hicho wakati anatakiwa apewe asilimia kumi ya bajeti ili tukague miradi yote ya Serikali nchi nzima.

SPIKA: Haya, ahsante sana, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba.

WAZIRI WA FEDHA: Yeah, wang’wise huyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo baada ya hapo tukakubaliana na Kamati tuongeze fedha ya kwa ajili ya kuanza kukagua real time. Wengine labda wanaweza wakasema wang’wise ni jambo baya, Wang’wise ni kaka yangu, yaani nimesema huyu ni kaka yangu, sijampa jina hata la tuzengano ni kaka yangu, wang’wise ng’wanuyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tukaongeza bilioni tano kwa ajili ya kumwezesha CAG, aanze kufanya real time audit, na hiki, Mheshimiwa Rais ndiye aliyesema sitaki kuona watu wanaendelea kukagua compliance ambayo inawafanya watu waibe kwa utaratibu; hapo ndipo tulipoanzia. Kwa hiyo, bajeti ya mwaka ule uliotangulia ilikuwa takribani bilioni 78 tukaipeleka mpaka sasa imeshafika 97 kwa ajili ya CAG, na ndipo mwaka 2020/2021 akaanza na akakagua, alianza na technical audit nne. Mwaka uliofuata akapeleka nane na mwaka uliofuata 11.

Mheshimiwa Spika, jambo hilo limewezekana tu baada ya kuanza kukagua value for money halafu real time. Yaani mradi ukiwa unaendelea; na ndipo CAG anapofanya kazi yake ya udhibiti; anaendelea kukagua. Amefanya hivyo kwenye miradi mikubwa.

Mheshimiwa Spika, jamani Afrika yetu tunaijua, ni mara chache sana nchi za kiafrika zinakuwa na Rais anayeweza kumwambia CAG usipepese macho kwenye taarifa. Mbona tunataka kusahau mapema? Ni marachache sana Afrika Rais anamtuma CAG akakague miradi mikubwa ya kimkakati tena ikiwa inaendelea. Amekagua miradi ya barabara, amekagua miradi ya kilimo na miradi yenyewe sio ya kitoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye barabara ameenda kukagua Daraja la Busisi likiwa linaendelea, kwenye umeme amekagua bwawa likiwa linaendelea. Ameenda kukagua reli ikiwa inaendelea. Irrigation schemes zinaendelewa kujengwa na CAG yuko site kukagua na haya ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais na ameweka fedha mahususi kukagua value for money sio vitabu...

SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Anatropia.

WAZIRI WA FEDFHA: ... kama kweli wote tuna nia njema, Je, kuna mtu anaweza kuwa na nia njema zaidi ya aliyetoa fedha ziende kukagua….

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Haya, Mheshimiwa Nchemba, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Anatropia.

TAARIFA

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nashukuru, nimpe taarifa Mheshimiwa Waziri, kaka yangu anayeongea. Itakuwa ni moja kati ya makosa makubwa kudhani kwamba Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kupewa fedha kiasi gani na kukagua ije kwa hisani. Kwanza anakagua kwa mujibu wa sheria na kuna kaguzi za aina tofauti tofauti. Ni wajibu wetu na wajibu wa Serikali kuhakikisha inamwezesha na si tu audit…
SPIKA: Haya, ngoja.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: ...tunayoifanya, tufanye forensic audit ili tuweze kuwakamata na hizo ndio ripoti zinazoweza kwenda mahakamani.

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, unapokea taarifa hiyo?

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, mimi sina hata haja ya kubishana na taarifa yake. Ninachomsisitizia ndicho na yeye anachosema. Tunachosema ni kwamba cha kwanza kilichotangulia ni political will.

Hivi mbona Watanzania tunasahau mapema sana, hivi Prof. Assad alishindwa kukagua, halafu aliondokaje? [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Spika, kwa nchi za Kiafrika, political will ni jambo la msingi sana kufanya ukaguzi kwa uwazi, kwani jambo hili ni la kawaida?

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, ngoja, umeanza maneno political will yaliyoendelea hapo mbele, hebu yafute, halafu…

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, ili nisipoteze muda nayaondoa. Nasema nilichotaka kukwambia ni kwamba, Rais ameonesha political will na akaongeza fedha wala sio kwa hisani, ameongeza fedha kama ambavyo katiba inasema lakini kilichotangulia ni political will yake, kwa sababu hajabadili katiba ili kuongeza hizo fedha. Ameonesha tu political will na jinsi utayari wake wa kutaka majizi kuonekana ndio hicho ninachokisisitiza.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, dakika moja malizia.

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kwenye upande wa Mkaguzi wa ndani; Mkaguzi wa Ndani amepewa vote yake na Bunge lilipitisha hapa, ameitengenezea muundo mpya ambao Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanasema hapa, kwa hiyo na yenyewe ni kwa ajili ya kudhibiti fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi naomba tusitawanyike twendeni tumuunge mkono Mheshimiwa Rais, ameshaonesha nia ya kushughulikia vitu hivi tena kwa njia ya kikatiba na Waheshimiwa Wabunge, nilimsikiliza ndugu yangu Mheshimiwa Mpina…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, kengele ya pili imeshagonga.

WAZIRI WA FEDHA: ... sisi wote tunapo kuja hapa ni Wabunge, tena mimi ni Mbunge wa jimbo anayekubalika Jimboni kwake...

SPIKA: Mheshimiwa ahsante sana.

WAZIRI WA FEDHA: ...kwa hiyo unapoongelea jambo…

SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu Nchemba…

WAZIRI WA FEDHA: ...kitu ambacho hujathibitisha na hakipo kwenye taarifa ni vyema tukaheshimiana…

SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu Nchemba…

WAZIRI WA FEDHA: ...maana mimi ninapotangazwa Jimbo zima huwa linashangilia, sio kama wewe tunajua unavyoshinda… (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Mwigulu Nchemba…

WAZIRI WA FEDHA: …lazima tu…