Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunipa uhai, nguvu, afya njema na akili timamu ili niweze kuchangia hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge.
Naomba nichukue fursa hii kwa heshima kubwa, kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa na Watanzania kuongoza nchi yetu katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba, 2015. Kwa kipindi kifupi alichokaa madarakani Watanzania kwa ujumla wetu tumefarijika na uongozi wake mahiri ambao unaonesha nia ya dhati ya kuiwezesha nchi yetu kupiga hatua kubwa kimaendeleo na kufikia kiwango cha uchumi wa kati. Na mimi naungana na Watanzania wenzangu kuendelea kumuombea afya njema ili aweze kuendelea kututumikia kwa mapenzi makubwa kama alivyoanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, ninampongeza Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Ninampongeza pia Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, kwa kuteuliwa kwake kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile napenda kukupongeza wewe, Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wengine wa Bunge kwa kuchaguliwa kuliongoza Bunge letu Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchaguliwa kwao kuwawakilisha wananchi katika Bunge hili. Nina imani kwamba sote tutatekeleza kazi zetu za kuwatumikia wananchi kufuatana na kauli mbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Hapa Kazi Tu ili tufikie malengo yetu ya kujikwamua kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwashukuru kwa namna ya pekee wapigakura wangu wa Wilaya ya Namtumbo kwa namna walivyojituma katika kuhakikisha ninaipata fursa hii ya kuwatumikia katika nafasi ya Ubunge, pamoja na kwamba muda mwingi sipo nao kutokana na majukumu ya Kitaifa, wanajua ninawawakilisha kwa kiwango kikubwa katika kutatua changamoto zao. Ninawaahidi, mambo yote niliyoyaahidi na yaliyoahidiwa ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi nitayasimamia yatekelezwe kwa kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia. Changamoto zote za kilimo, hususan kilimo cha tumbaku na mazao mchanganyiko pamoja na masoko ya uhakika, maji, umeme, mitandao ya simu, barabara, maeneo ya kilimo na mipaka ya kiutawala, zinazowakabili wakazi wa Wilaya ya Namtumbo nitazishughulikia kikamilifu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati kabisa ninapenda kumshukuru Mheshimwa Rais kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, kumsaidia Mheshimiwa Profesa Makame Mnyaa Mbarawa katika nafasi yake. Napenda kuwaahidi Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na Watanzania wote kuwa sitawaangusha.
Aidha, ninaomba niishukuru familia yangu, mke na watoto wangu kwa kuniunga mkono, kunivumilia na kunitia nguvu katika kutekeleza dhamira yangu ya kuwatumikia Wana Namtumbo na Watanzania wote katika nafasi hii ya Naibu Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusema kwamba, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa ndugu zangu Wabunge wote tuunge mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, pamoja na kwamba inawezekana barabara ama ahadi yako nyingine haipo katika mpango wa utekelezaji kwa mwaka huu. Ni wazi ahadi zipo nyingi na sisi tutajitahidi kuzitekeleza kikamilifu kwa awamu, kwani tunaye jemedari, Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Kazi anayoifanya mnaiona na dhamira yake ya kututumikia Watanzania, hususan wananchi wa vipato vya chini haina mashaka kwa yeyote mwenye mapenzi mema na Taifa letu. Hivyo, kwa heshima na taadhima nawaomba mtuunge mkono na kwa kweli, tupeni moyo wa kuwatumikia. Nawashukuru Wabunge wote kwa namna mlivyochangia, mawazo na mapendekezo yenu yote kwetu ni maelekezo.
Tutayafanyia kazi kwa kuanzia na kusimamia kutekeleza miradi ambayo Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano amewasilisha kwa mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze katika kujibu hoja na nitajibu baadhi tu ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia. Hoja ni nyingi, kwa hoja ambazo tutashindwa kuzitolea majibu leo kutokana na muda tutazijibu kwa maandishi. Kama nilivyosema, hoja ni nyingi na, nitaanza na hawa ambao hatujazijibu rasmi kwenye vitabu ambavyo baadaye tutawagawia. Nitaanza na wale waliochangia mwishoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa Bandari ya Nyamisati naomba nikuhakikishie, zimetengwa shilingi bilioni 1.5 kushughulikia bandari hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa barabara ya Bumbuli - Korogwe, Soni - Bumbuli, fedha zimewekwa sifuri kwa sababu study imekamilika. Sasa tunatafuta fedha ndani na nje ili mwaka ujao wa fedha, 2017/2018 tuanze kujenga, lakini Waziri wangu atalifafanua zaidi hilo na kama kutakuwa na mabadiliko atayaeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetenga jumla ya shilingi bilioni 3.5 kwa ajili ya malipo ya fidia katika eneo la Muhalala, pale ambapo panajengwa One Stop Inspection Station. Naomba tukubaliane, hiyo hela imetengwa na tutawalipa fidia ili kile kituo kianze kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara nyingi ambazo zimeongelewa hapa, ziko ambazo kwa sasa tumezitengea bajeti ya matengenezo peke yake. Naomba kuwahakikishia, huu ni mwaka wa kwanza, ahadi iliyoko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ahadi ambazo viongozi wetu wamezitoa kuanzia Serikali ya Awamu ya Tatu, ya Nne na ya Tano, ninawahakikishia zote tutazikusanya na tutatafuta namna tuziwekee priority tuanze ipi na hatimaye tutamalizia na ipi kwa sababu nadhani sio rahisi kwa mwaka huu wa kwanza kuingiza barabara zote zilizoahidiwa na viongozi wetu wakuu na tulizoahidi katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Naomba mtuamini, tutahakikisha ahadi zote ambazo zilitolewa na viongozi wetu wakuu pamoja na chama kupitia, kitabu cha Ilani tutazitekeleza; ndiyo kazi tuliyopewa katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kibondo - Kasulu - Manyovu imeongelewa kwa kirefu sana na Wabunge wengi sana wa upande wa Magharabi. Labda kitu ambacho wengi wamekihoji ni kwamba, fedha zilizooneshwa na AfDB hazijaonekana katika kitabu cha bajeti. Hizo fedha zinazotumika kwa sasa kwa ajili ya feasibility study na detailed design zimeshatolewa, ziko dola 1,286,685 ambazo ziko katika bajeti ya East African Community na Sekretarieti ya East African Community ndiyo inayosimamia ujenzi wa barabara hiyo. Ninawahakikishia barabara hiyo kipande kilichobaki ni kirefu, ndiyo, lakini tutahakikisha kinajengwa kwa kadiri ambavyo wahisani na wengine wametusaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende Kusini. Barabara ya Mtwara - Masasi - Nachingwea - Ruangwa hadi Nanganga. Mimi naomba mtuamini, tumepanga bajeti, ni kweli ni kidogo, lakini tuanzie na hicho ambacho tumekipanga. Na kwa upande wa Nachingwea - Ruangwa hadi Nanganga tutaanzia na feasibility study na detailed design. Ile nyingine ambayo feasibility study na detailed design imekamilika, ile inayoanzia Masasi - Nachingwea - Nanganga, tutaanza kuijenga, lakini kwa kiwango hicho ambacho tumekitenga. Ni kidogo lakini mimi naomba tukubaliane kwamba mwaka huu wa kwanza tuanze na tuone tutaendeleaje; na mimi nina uhakika tutaendelea vizuri kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudi kwenye barabara ya Soni - Bumbuli; pamoja na kwamba imewekwa sifuri na tumeweka hela hizi za matengenezo, nawahakikishia mwaka ule mwingine 2017/2018 tutaiangalia kwa macho zaidi kama mlivyosema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijibu machache. Kimsingi vitabu hivi tutawapa kwa hiyo, majibu kwa wote walioongea humu ndani Bungeni ambao wamefikia zaidi ya 84 na waliotuletea kwa maandishi wamefika 105. Wote majibu yenu tutayaingiza katika kitabu hiki na tutawagawia kabla wiki ijayo haijaisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wachache ambao nitafungua tu popote pale, kwa sababu ni mengi sana, sitaweza kumaliza, kwa mfano Mheshimiwa Shaban Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, pamoja na Mheshimiwa Rashid Shangazi Mbunge wa Mlalo; hoja yao walitaka Serikali ianze kujenga Bandari ya Tanga sambamba na ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Uganda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali kupitia TPA imetenga jumla ya shilingi bilioni 14.461 kwa ajili ya kuboresha Bandari ya Tanga na katika mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya Shilingi bilioni 19.798 zimetengwa. Aidha, Bandari ya Tanga ili iweze kufanya kazi kwa ufanisi TPA kwa kushirikiana na wataalam waelekezi inarejea upembuzi yakinifu uliofanywa mwaka 2012 kwa kuzingatia shehena iliyobainishwa kupitia katika bandari hiyo. Mtakumbuka huko nyuma tulisema ile bandari ilionekana haina faida na wengi walikataa kuwekeza, lakini baadaye tulipoingiza reli ya kutoka Musoma hadi Tanga bandari ile sasa inaonekana ina faida na hivyo uwekezaji ni wa dhahiri.
MWENYEKITI: Ahsante!