Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Dr. Charles Stephen Kimei

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vunjo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nianze kwa kuwapongeza Mawaziri wote wawili kwa mawasilisho mazuri na Mapendekezo mazuri ya Mpango pamoja na Mwongozo wa Bajeti kwa mwaka unaokuja. Najua kwamba hii siyo Mpango, ni mapendekezo. Kwa hiyo nitajikita zaidi kwenye yale yanayoyendana na yale yaliyowasilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kuweza hatimaye kurejesha Tume ya Mipango na Wizara ya Mipango na Uwekezaji. Naamini hivi ni vyombo viwili ambavyo vilikosekana na pengine ndiyo sababu tumeshindwa kwa muda mrefu kuweza kufuatilia utekelezaji wa dira yetu, kuweza kufuatilia na kutathimini mipango ambayo tumejiwekea. Hatimaye sasa tumeipata na ninaamini huko tunakoenda tutaweza kusimamia vizuri zaidi kutathmini na kujua ni kitu gani ambacho kimekosekana kwenye mikakati yetu ili kuendelea kuboresha kila wakati yale ambayo tutakuwa tunayatekeleza kwenye mipango yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba institution building ni kitu kizito sana kwenye nadharia ya uchumi. Ni kitu ambacho kinawezesha. Ukiwa na taasisi zinazostahiki, taasisi za kijamii, taasisi za kiserikali, taasisi za sekta binafsi zikiwa zimejipanga vizuri katika kusimamia maendeleo na kushauri maendeleo, basi hapo tutaona tunapata maendeleo yale ambayo tunayategemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba Wakoloni waliamua kuvunja zile taasisi zetu za kiasilia ili tusipate mahali pa kujishika. Ndiyo sababu tunapata shida sana kurejesha hizi taasisi ambazo tunaamini kwamba zingekusaidia kutekeleza. Kwa mfano, kwenye kilimo bila ushirika, actually huwezi kufanya mambo mengi kwenye uchumi ambao umetawaliwa na wakulima wadogo wadogo. Kwa hiyo, ni mambo ya kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimbilie kwenye moja niliyonayo kwenye mwongozo wa bajeti; katika mpango huu wa miaka mitano, tulikuwa tumejiwekea lengo kwamba matumizi ya maendeleo yawe kati ya asilimia thelathini na arobaini ya bajeti yetu, na kusema kweli Bunge hili kazi yake kubwa ni kuhakikisha kwamba bajeti ya maendeleo inaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa bajeti ya maendeleo imebakia pale pale trilioni 15 na kiuwiano inazidi kupungua kwa sababu ilikuwa asilimia 34 ikaenda ikafika sasa ni asilimia 32. Hili jambo bado naamini kwamba tusilikubali sana, tujaribu kumbana Waziri wa Fedha ili atekeleze vile anavyosema kwamba atajaribu kubana matumizi yasiyo ya lazima na fedha hiyo inayokuwa served iende kwenye maendeleo badala ya kupunguza maendeleo. Kwa hiyo, mimi naomba kwamba wakati tunapopeleka hii tuhakikishe kwamba tunaweka ukomo, kwa mfano bajeti ya kawaida isiwe zaidi ya inflation rate, something like that, tungeweka ukomo wa namna ile ili isikue sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini ukimpa mtu fedha atatumia tu, utakuta kwamba unakaribisha Waziri aje kwenye Kamati anakuja na watu hamsini. Watu hamsini wanahitajika? Wakija watatu tu au wawili wanatosha, ukweli ni kwamba tunawapa fedha nyingi mno za matumizi ya kawaida, ndio sababu wanaweza, kama ni kuhamishia task force zikaenda Arusha na nini lakini wanatumia hii fedha ya kawaida bila kujali sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu cha pili, kwenye hilo ni kwamba hatujafanya public expenditure review kwa miaka mingi kidogo, naamini turejeshe kufanya public expenditure review ili tuweze kufanya strategic resources allocation na tuone kwamba fedha zinaenda mahali pake nani wapi ambapo tunaweza tuka-serve ili kuweza kuchangia zaidi kwenye maendeleo ya majimbo yetu na wananchi wetu wakafurahi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nafikiri hilo ni la msingi na nafikiri kwamba Mheshimiwa Waziri anapokuja na mpango kamili atakuwa na fedha nyingi zaidi ya hiyo fedha ili angalau twende asilimia 34 kama tulivyokuwa hapo awali ili ibaki kwenye maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ya mpango hayajabadilika sana na yale ya miaka hii mitatu ya nyuma na ninajua ni kwa sababu gani? Kwa sababu pengine ni mpango ule ule wa miaka mitano ndio tunautekeleza, kwa hiyo, kuna miradi inaingiliana na kadhalika lakini pia Tume ya Mipango ilikuwa ni mpya bado haijajikita sana kufanya tafiti zinazohitajika ili waweze kuleta mpango ambao una ubunifu wa kwao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho kinasikitisha ni kwamba bado hatujaona mwanga unaotupeleka kukuza kasi yetu ya ukuaji wa pato letu kufikia asilimia nane. Asilimia nane ndio ilikuwa kwenye dira na karibu tungeifikia lakini ndio tukaja tukayumbushwa na Uviko lakini bado kinachosikitisha ni kwamba mipango inayokuja haijaweza kusema ni lini tutaanza kuona uchumi unarejea asilimia saba mpaka nane. Naamini bado kuna mikakati kama hii ya sekta ya kilimo na sekta nyingine inaweza ikasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi niseme kwamba, tunafahamu kwamba Waziri wa Mipango amesema vizuri sana kwamba, kupanga ni kuchagua na amesema kwamba tutakamilisha kwanza ile miradi ambayo inaendelea kabla hatujaingiza miradi mipya mingine kwenye bajeti yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni sawa kabisa na kwa sababu inaendana na ukweli kwamba resources zetu ziko limited na ukweli kwamba, hususan kwenye sekta hii ya nje hatujawa na mikakati ambayo inaweza ikawa na uhakika wa kuongeza fedha za kigeni. Fedha za kigeni zimekuwa ni utata na sasa hivi kitakachokuwa consumed katika kutekeleza malengo yetu ni fedha ya kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa issue inayojitokeza ni kwamba tunasema kilimo na sekta nyingine lakini na Kamati ilisema, imeona kwamba maeneo rahisi zaidi ni kwenye eneo hili la utalii na eneo la logistics, usafirishaji hasa kutoka kwenye Bandari ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Bandari ya Dar es Salaam tuna bahati, Mungu ametupa bahati tumepata DP World imekuja wakati wake, kwa hiyo, naamini kwamba inaweza ikafungua ile logistics ya hub yenyewe tukaanza kuona kwamba hii infrastructure iliyojengwa, barabara na SGR inatumika kwa uhalisia kupeleka mizigo kwa nchi jirani na kuanza kuongeza sana pesa zetu za kigeni, kutumia DP World. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kwamba hili ni jambo ambalo tutaiomba Serikali ilifanyie kazi na ijaribu kumuomba Mheshimiwa Rais wetu na tumuombee ili aweze kuhamasisha hawa jamaa zetu ili waweze kuingiza ule uwekezaji ambao walikuwa wameahidi, wauingize haraka kwenye hii bandari yetu na tuweze kuona tunabadilisha kabisa suala zima la foreign exchange hapa kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimeliona ni kwamba, matumizi ya takwimu za sensa hayajakaa sawa kwenye mipango na kwenye miongozo. Nilifikiri kwamba Serikali na Wizara hizi zingeangalia zile statistics za sensa ili waone kwamba ni kitu gani wanaweza kutumia kupata mapato zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna idadi za nyumba na tunajua nyumba zimeandikishwa, makazi yanajulikana, kwa hiyo kuna uwezekano wa kukusanya zaidi kwenye kodi ya majengo. Tungeweza kuona kwamba ni vitu gani tunatarajia kule, hata huku kwenye DP World hajaweza kuona kwamba mapato tutakayopata yataongezeka au yatakuaje kwa sababu kusema ukweli projected revenue ni kubwa sana ukilinganisha na uhalisia wa 2022/2023 ni thirty-nine trillion halafu mwaka huu 2023/2024 tumeweka forty-four utaona kwamba niongezeko kubwa sana kwa hapo kama ukitumia uhalisia wa mapato tuliyopata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukienda forty-seven trillion ukitumia uhalisia huu tunaona utakuta kwamba hatutafikia. Forty-seven trillion ni fedha nyingi sana pengine unless mnasema DP World wataanza kutuingizia fedha kwenye akaunti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba kwa vile usanifu wa miradi umekuwa ni hafifu na Wizara ime-recognize kwamba ubora ule wa usanifu wa miradi hatuna, yaani ubora ule wa usanifu na usiposanifu vizuri huwezi kupata hata financing cost ya miradi ile. Kwa hiyo, ndio sababu miradi inachelewa kwa sababu haikusanifiwa kwa ubora, na unaenda sokoni ukiwa na mradi ambao umesanifiwa nusunusu, haijatathminiwa na watu wawili au watatu, halafu unaenda unapata bei kubwa unashindwa kutekeleza mkakati na unaanza kupata matatizo njiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nafikiri hilo ni jambo la kuangalia na ningeomba sana wizara isiingize kwenye mpango miradi ambayo haijasanifiwa. Ifanyiwe upembuzi yakinifu mapema na isanifiwe mapema ili wakati tunaingiza kwenye mpango wetu wa mwakani basi iwe inajulikana kwamba inapoenda kutekelezwa maandiko yake yamekaa vizuri na tunaweza kuyauza kwa PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu niseme, nafurahi kwamba kwenye mpango huu, mkazo unawekwa kwenye sekta binafsi kushirikishwa na hii inaenda sambamba kabisa na ile sheria ya PPP tuliyoipitisha ambayo sasa hivi iko vizuri na ninaamini sasa hivi tutapata wawekezaji wengi ambao wataweza kuja kuwekeza kwa mpango huu wa PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tena nirejee kuwashukuru Mawaziri, pia nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi hii anayoifanya.