Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kunipa nafasi na mimi njiweze kuchangia kwenye mapendekezo haya ya mpango ya mwaka 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais wetu Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake chanya ya kuweza kurudisha Tume ya Mipango lakini pia kwa kuunda Wizara maalum ya Mipango na Uwekezaji kwa ajili ya kushughulikia masuala mahsusi ya mipango ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri sasa kwa kuwepo kwa Tume hii ya Mipango pamoja na Wizara hii maalum kutatua changamoto zote ambazo zilikuwepo hapo awali, changamoto ambazo tuliona kila Wizara ya kisekta inapanga mipango kivyake vyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili liliweza kusababisha gharama kubwa ya utekelezaji wa miradi ya maendelep lakini pia ufanisi hafifu wa utekelezaji wa miradi. Kwa mfano, Wizara ya Maji inachimba mabwawa kwa ajili ya matumizi ya binadamu, lakini Wizara ya Kilimo inachimba mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji, vilevile Wizara ya Mifugo na Uvuvi inachimba mabwawa kwa ajili ya ufugaji wa Samaki na kunyweshea mifugo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi yote hii tungeweza kuitekeleza kwa Wizara moja tu ya Maji na hivyo kuweza kutumiwa na Wizara zingine za kisekta. Bwawa hilo moja ambalo lingeweza kutengenezwa na Wizara ya Maji lingeweza kutatua tatizo la umwagiliaji, uvuvi na kilimo na hivyo basi tungeweza kuokoa gharama kubwa ambazo tungetumia kutekeleza miradi mingi kwenye kila sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa ushirikiano kunasababisha miradi kutekelezwa kwa gharama kubwa lakini pia Serikali inatawanya fedha kwenye maeneo mbalimbali na hivyo kutokuwa na ufanisi wa miradi ambayo tunaitekeleza na miradi inakuwa haina tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Kamati ilivyoshauri, kwa miradi inayofanana basi Wizara hizi za Kisekta ziweze kushirikiana na Wizara ya Fedha ili fedha hizi ziweze kutoka kwenye fungu moja ili kutekeleza mradi mmoja wenye tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Waziri alivyosema hapo awali, pamoja na mambo mengine ambayo mapendekezo haya ya mpango yamezingatia, pia mapendekezo haya yamezingatia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya Uchaguzi wa 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuzingatia hili tunategemea tuone kwenye mpango, mikakati ya Serikali iliyonayo katika kutekeleza malengo haya kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano tu, kwenye sekta ya utalii hadi kufikia mwaka 2025 tunategemea idadi ya watalii iweze kuongezeka kufikia watalii milioni tano. Namwomba Mheshimiwa Waziri, kwenye mpango unaokuja, atuainishie hapa tutawezaje kufikia watalii milioni tano kutoka idadi ya sasa iliyopo ya watalii milioni moja na laki nne.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto zote tulizonazo kwenye sekta hii ya utalii, changamoto ya miundombinu, changamoto ya idadi ndogo ya vyumba vya kulaza wageni wetu, changamoto ya ukosefu wa maduka ya kubadilishia fedha, changamoto tuliyonayo ya ada na tozo mbalimbali ambazo ni kubwa sana kwa watalii wetu. Namwomba Mheshimiwa Waziri, wakati anahitimisha atuambie mpango unaokuja utawezaje ku-address changamoto hizi ili tuweze kufikia malengo yaliyopo katika Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu hapa ni mfano tu nimeutoa, kwa hiyo katika malengo yote ambayo tunayo kwenye ilani ya Chama Cha Mapinduzi basi tuhakikishe kwamba mpango wetu unaweza ku-address jinsi gani tunaweza kufikia malengo haya hadi ikifika 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia Malengo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda ni lazima kama Taifa tuweze kuongeza tija kwenye zile sekta za uzalishaji kama sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi lakini sekta ya madini pamoja na misitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kuongeza uzalishaji tutakuwa na uhakika wa kulisha viwanda vyetu, pia kwenye hili, ni lazima kama Taifa tuje na mikakati ya kuweza kuhakikisha tunaongeza thamani ya mauzo, ambayo tunauza nje ya nchi. Tukiweza kufanikisha haya tutaweza kukuza uchumi wa Taifa letu kwa sababu tutauza bidhaa zetu za nje kwa bei ya juu lakini vilevile tutaweza kuongeza fedha za kigeni ambayo ni changaomoto kubwa hivi sasa kwenye sekta ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, ili kufikia malengo ya mpango wa kujenga uchumi shindani ni lazima tushirikishe sekta binafsi kwa vyovyote vile. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, hapa kwenye hotuba yake naona amekazia ushiriki wa sekta binafsi lakini ombi langu nililonalo kwa Serikali hivi leo ni kwamba, Serikali iweze kutatua changamoto zilizopo sasa hivi ambazo zinakwamisha utekelezaji wa miradi kwa njia ya ubia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za ushiriki wa sekta binafsi kwenye miradi yetu bado ni nyingi sana. Bado kuna urasimu mkubwa lakini kuna tozo na ada mbalimbali tuweze kuziangalia kwa ukaribu, lakini mazingira ya uwekezaji kwa ujumla kushirikisha sekta binafsi bado ni magumu. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hapa aweze ku-address mambo yote haya ambayo yanakwamisha utekelezaji wa miradi kwa njia ya ubia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mipango yetu ni lazima tuzingatie utekelezaji wa miradi wenye tija na ufanisi. Kwenye hili naomba niongelee mradi wa BBT wenye lengo la kujenga kesho iliyo bora. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuja na maono haya kuanzisha miradi kama hii ambayo itatatua changamoto za ajira kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ya BBT inatekelezwa kwa fedha za Mkopo za ECF kutoka IMF…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia 2023 Wizara ya Kilimo imeshatumia zaidi ya bilioni mia moja kwenye mambo haya ya BBT, lakini Wizara ya Mifugo na Uvuvi wameshatumiam zaidi ya bilioni 28 kwenye utekelezaji wa miradi hii.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Zaytun, kengele ya pili hiyo.

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumalizia kwa kusema kwamba kupanga ni kuchagua lakini sio kuchagua tu ila kuchagua mambo yaliyo bora zaidi na yenye tija. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, wakati anahitimisha asituletee orodha ya mirdi isiyotekelezeka lakini atuletee miradi michache yenye tija na inayotekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)