Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na mimi kwa kupata fiursa hii ya kuchangia Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa mafanikio makubwa ambayo tumeyapata sisi Tanzania. Ukiangalia huu Mpango ni sehemu ya Mpango wetu wa Taifa wa miaka mitano. Vile vile, huu ni Mpango wa nne. Dhima ya Mpango wetu ilikuwa ni kujenga uchumi shindani, viwanda na maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, nimeuangalia huu Mpango wetu, kwa kweli nawashukuru sana hawa Waheshimiwa Mawazii wawili na hizi Wizara mbili pamoja na Tume ya Mipango; wamefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipouangalia huu Mpango, ukiuangalia umesheheni taarifa nyingi ambazo zinaonesha ni kiasi gani Tanzania tuko vizuri kiushindani Afrika lakini hata nje ya mipaka yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye utulivu wa shilingi yetu kwa kweli tuko vizuri sana. Nilikuwa nalinganisha utulivu wa shilingi kuanzia mwaka 2015 mpaka mwaka 2023. Nimekuja kupata taarifa kwamba shilingi ya kwetu ukilinganisha na Naira ya Nigeria, shilingi ya kwetu imepanda thamani kwa zaidi ya asilimia 350. Ukiilinganisha na Kenya, shilingi ya kwetu imepanda thamani kwa zaidi ya asilimia 122. Vile vile, yote hayo ukiangalia na Afrika Kusini, shilingi ya kwetu bado imepanda thamani. Hii maana yake ni kwamba utulivu wa uchumi wetu ni kutokana na hawa wenzetu na Mheshimiwa Rais ambao kwa kweli kazi yao ilikuwa ni nzuri mno. Kwa hiyo, utulivu tunaouona na hizi taarifa tunazoziona zinadhirisha kwamba, pamoja na changamoto tulizonazo duniani Tanzania tuko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuendelee kuwa vizuri ni nini cha kuangalia? Mimi kwenye mpango huu nilijikita kwenye vihatarishi. Tusipojipanga ku-manage hivi vihatarishi (risk management), haya mafanikio yote tunayoyaona na hii mipango yetu hatuwezi kwenda. Katika Mpango wameweka vihatarishi ambavyo nilipoangalia kwenye Ripoti ya Kamati ya Bajeti, wameweza kuvijumuisha katika sehemu tatu. Kwanza ni strategic risk au risk za kimkakati, ya pili ni operational risk au risk za kiutekelezaji. Sasa nilipoangalia hizi mbili zote na ukiangalia mpango, huwezi kuona kiasi gani tutaweza kuzi-manage hizi risk; kwa sababu dunia ya leo imebadilika sana. Management ya leo ni tofauti na huko tulikotoka. Management ya leo ukiangalia majadiliano ya wiki iliyopita kwa zile Kamati tatu, ukiangalia matatizo makubwa inawezekana hatukuweza ku-manage hizo risk zetu ambazo zilikuwepo. Kwa hiyo, katika mipango hii kama hatutajipanga vizuri, inawezekana haya mafanikio yote tuliyoyapata tusiweze kwenda nayo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu; kwa sababu kwenye vihatarishi vya kimkakati (strategic risk) hapa ndiyo unaangalia sasa kwenye ile dhima ya ushindani Tanzania tutashindana vipi na wenzetu? Kwa sababu kwenye uchumi wa leo wa dunia, hizi nchi zimebaki kama vijiji, kwa hiyo Tanzania hatuwezi kuwa kama kisiwa. Kwa hiyo, sasa ni namna gani tunapopanga mipango yetu, kama huu mpango kwa hatua alizochukua Mheshimiwa Rais za kuhakikisha kuwa tunaboresha ufanyaji kazi wa Bandari zetu ambalo ni jambo jema sana, ambalo linaweza kuwa sehemu ya kutukomboa sisi kwenye changamoto zote hizi tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimeizungumzia hiyo, naangalia ya kwamba, je, tumeboresha pale, mizigo itafika vipi kwa wateja wetu hasa wa nchi za nje? Hapo inabidi mkakati uwe ni kuhakikisha kuwa reli yetu ya SGR kipande cha Dar es salaam mpaka Makutupola, kikamilishwe haraka na kianze kufanya kazi. Hiyo itawezesha kupunguza msongamano hasa wa mizigo na hasa hata msongamano wa magari. Kwa hiyo, presha tuliyonayo ya magari sasa hivi itapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine. Ili tuhakikishe kuwa sehemu yetu ya biashara ya bandari inafanya vizuri ukilinganisha na wezetu, inabidi Serikali ichukue hatua ngumu ya kuiboresha TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kandege, amezungumza asubuhi, nimemsikiliza kwa makini sana. Mizigo yetu ya nje inapitia ukanda au mkondo huu wa Reli ya TAZARA au Barabara ya TANZAM. Kwa hiyo, tusipoiboresha TAZARA inawezekana ushindani wetu usiwe mzuri kwa sababu wenzetu tayari wamekwishaanzisha Lobito Corridor ambayo ni kwa ajili ya kushindana na bandari ya Dar es salaam. Vile vile, kuna Naccala Corridor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingawaje watu wanachukua kwa wepesi lakini mkakati uliopo ni kuua biashara yetu. Sasa, ningeiomba Serikali ifanye mkakati wa kuichukulia hii kama kihatarishi cha biashara yetu na kupoteza biashara za nje. hivyo iboreshe TAZARA. Pia, mimi ningependelea zaidi siyo kuboresha tu, hizi reli zetu mbili ziendeshwe na watu binafsi. Na uzuri wake katika mpango, Mawaziri wameonesha ni namna gani washirikishe sekta binafsi katika biashara za reli, bandari, na viwanja vya ndege; na huo ndiyo uwe mwendelezo. Kwa sababu Serikali isijiingize kufanya biashara sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na tatizo la Sheria ya TAZARA. Kwa hiyo Serikali ichukue hatua katika kuhakikisha kuwa lile tatizo linatatuliwa mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo limeoneshwa kwenye Mpango (Vipaumbele) ni madini. Resources hizi tulizonazo hazitakuwa na maana tukichelewa kuzitumia. Uzuri wake Serikali imeonesha kwa kiasi kikubwa kuwa itaweka nguvu kubwa kwenye madini hasa haya madini ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mgano mdogo sana. Kwa Mbeya, Songwe tuna madini hayo ya kimkakati ambayo Serikali imechelewa mno kuamua ni namna gani tuyapeleke sokoni na ni namna gani tuingie sokoni. Kwa Mbeya tuna madini yanaitwa Niobium. Nimeongea mara nyingi sana inawezekana hata jina lilibadilika nikaitwa bwana Mheshimiwa M-niobium.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo madini ingechukuliwa 2016 mzigo wa vyuma kwa ajili ya Reli yetu ya SGR ambao tunalalamika sasa hivi na majengo yetu, isingekuwepo. Kwa sababu wale wawekezaji wako tayari kujenga kiwanda cha kwanza Afrika na cha nne duniani ambacho kitaleta ajira nyingi lakini na FDI nyingi ambazo ndiyo Serikali yetu inahitaji leo kutokana na changamoto za forex. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiendelea kuchelewa tunajichelewesha wenyewe. Hayo Madini yatagunduliwa sehemu zingine na hao watu wanatafuta sehemu zingine ambazo wanaweza kufanya biashara zao vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la barabara na reli ni muhimu sana na twende kwenye barabara ambazo zina-impact kubwa kwenye uchumi. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ujenzi wa kuboresha barabara ya TANZAM na barabara ya Dar es Salaam – Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya TANZAM inahitajika siyo leo ilikuwa inahitajika juzi. Kwa hiyo naiomba Serikali ifanye haraka kukamilisha hiyo mipango iliyopo ili faida yetu ya hawa watu ambao wanaendesha Bandari iweze kuleta matunda ikiwemo vilevile na ujenzi wa Bandari Kavu ambazo zitaleta pressure zitaongeza ushindani kwa hawa wenzetu ambao wanataka kupoka soko letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)