Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2024/2025. Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa nafasi ya kuwepo katika Bunge hili kwa siku ya leo, lakini pia nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutekeleza mipango miwili ambayo imepita na kuna mambo mengi sana ambayo yamefanyika katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ameendelea kutekeleza miradi ya kimkakati, nikitolea mfano wa SGR lakini Bwawa la Umeme la Mwalimu Nyerere, lakini pia ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya barabara, mambo ya elimu, ujenzi wa miundombinu kwenye shule za msingi, elimu bila malipo, ujenzi wa zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, hospitali za mikoa lakini na Hospitali za Kanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kuwapongeza sana Mawaziri wawili, Waziri wetu wa Mipango na Uwekezaji, lakini pia Waziri wa Fedha kwa kuandaa Mpango mzuri wa mwaka 2024/2025 lakini pia na Mwongozo kwa ajili ya Maandalizi ya Bajeti kwa Msimu unaokuja. Nasema kwamba ameandaa Mpango mzuri kwa sababu ukipitia hiyo rasimu imetambua uwepo wa baadhi ya miradi ambayo ilianza kutekelezwa miradi ya kimkakati. Pia ukiangalia ule Mpango umetambua uwepo wa rasilimali chache ili Mpango ule uweze kutekelezwa. Rasimu ile vile vile imetambua uwepo wa uwezekano wa kutumia Sekta Binafsi katika kutekeleza Mpango huu unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizingatia malengo ya Mpango wetu wa Miaka Mitano ambao unaishia 2025/2026, lengo kubwa ni kuhakikisha kwamba tunaingia kwenye Uchumi Shindani, Uchumi wa Viwanda, lakini siku ya mwisho tunatakiwa tuone kabisa kwamba katika uchumi wetu pato limeongezeka na wananchi wetu wameondokana na umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kulitekeleza hilo hii Rasimu ya Mpango ukiipitia imeweka vipaumbele mbalimbali vya kuvitekeleza ili tuweze kufikia malengo. Katika vipaumbele hivi vilivyowekwa, nitajikita sana kuelezea kwenye rasilimali zilizoandaliwa kutekeleza Mpango ambao utakuwa umeandaliwa. Rasilimali hizo kwanza ni mapato ya kikodi, lakini pia kuna misaada na mikopo mbalimbali ya ndani na nje, lakini pia kuna kutumia Sekta Binafsi ili kuhakikisha kwamba Mpango huu unatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiingia kwenye upande wa Kodi ya Mapato, ukiangalia Mpango wetu wa miaka mitano katika Kodi zetu mbalimbali ukizifanyia uchambuzi, kuanzia mwaka 2020/2021, 2022 hadi 2025/2026, unakuta kwamba kwa mfano kwenye kodi ya mapato, unaona kabisa makusanyo yetu ni asilimia 36 mpaka 37, lakini ukienda kwenye kodi ya ongezeko la thamani (VAT) makusanyo yetu ni asilimia 29 ya Kodi zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye mapato ya forodha, makusanyo yetu ni asilimia saba kuanzia ule mwaka 2021 hadi 2026. Ukienda kwenye ushuruu makusanyo yetu ni asilimia 15 na ukienda kwenye kodi zingine, makusanyo yetu ni asilimia 13 mpaka 12. Kwa hiyo ukifanya tathmini kwenye Kodi zetu na makusanyo unakuta kabisa una udhaifu katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Ili uone kabisa kwamba kuna udhaifu hivi karibuni tulipata taarifa kwamba baadhi ya Halmashauri zetu zimekusanya mapato ya ndani lakini kwa njia ambayo siyo halali. Kwa hiyo unaona kabisa kwamba kuna udhaifu katika ukusanyaji wa mapato ya ndani pamoja na kodi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweza sasa kudhibiti hilo na kuongeza wigo wa mapato, nilikuwa nashauri kwamba kwenye Sekta ya Madini inabidi tuongeze kodi tuangalie vyanzo mbalimbali vinavyotokana na Sekta ya Madini ili tuweze kuongeza kodi. Kwa mfano, nikichukulia kwenye Mradi wa Chuma na Makaa ya Mawe Mchuchuma na Liganga unakuta kwamba katika dunia sehemu ambayo unaweza ukapata makaa ya mawe na chuma ni Liganga peke yake katika dunia. Kwa hiyo wenzetu wanasafirisha makaa ya mawe kwenda Nje kwa ajili ya kuyeyusha chuma, lakini sisi tuna uwezo wa kuwekeza Liganga, tukayeyusha chuma na tukapata resource nyingi sana na fedha nyingi za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tungeweza kujenga Reli ya kutoka Mtwara kwenda Liganga na Mchuchuma, lakini vilevile kwenda Mbamba Bay ili kuhakikisha kwamba tunarahisisha usafirishaji wa chuma na makaa ya mawe lakini vile vile kuhakikisha kwamba tunaweza tukasafirisha kwenda nje kupitia Bandari ya Mbamba Bay. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo lingine tunaweza tukapata kodi kupitia gesi asilia inamaana tukiweka uwekezaji mkubwa kwenye gesi asilia tutakuwa na uhakika wa kupata pato la kutosha la kuweza kuendesha shughuli zetu katika nchi hii. Pia kwenye suala la ufugaji, wenzetu wafugaji ukiangalia takwimu za ufugaji unakuta Serikali inakosa mapato mengi kupitia ufugaji kwa sababu sehemu nyingi ufugaji wetu ni holela. Kwa hiyo niiombe Serikali itengeneze mfumo unaokubalika ambao utatusaidia kukusanya mapato kupitia kwa wenzetu wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ningeweza kushauri ambalo litatusaidia kupata mapato ya kutosha ili ku-finance mpango wetu pamoja na bajeti itakayoandaliwa, ni kwenye bidhaa za misitu. Tupo chini sana kudhibiti na kuhakikisha kwamba tunakusanya mapato kupitia bidhaa za misitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango mwingine ambao nataka kuchangia ni kwenye kuziba mianya kwenye mifumo mbalimbali ya kodi, kwa mfano, ukiangalia kodi zetu za mapato ya ndani, bado kuna mianya ambayo inafanya mapato haya yasipatikane kwa wingi, lakini hata ukiangalia kwenye takwimu alizozitoa Waziri kwenye kodi ya mapato na kodi zingine unakuta kabisa kwamba ongezeko au ukuaji wa uchumi wetu hauendi sambamba na mapato tunayoyapata. Kwa hiyo, hapa ningeshauri Serikali iweke mikakati na mifumo ambayo inasomana ya kutuhakikishia kwamba tutaweza kukusanya mapato yetu bila kuwa na matobo ya aina mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho, wenzetu wa Rwanda uchumi wao asilimia 31 unachangiwa na sekta binafsi, nafahamu kwamba huko nyuma tulishindwa kuitumia sekta binafsi kutokana na sheria zetu zilikuwa zinatubana lakini sasa hivi tumefanya marekebisho ya Sheria ya PPP kwa hiyo nina uhakika tukitumia vizuri na tukaondoa vile vikwazo ambavyo vinafanya sekta binafsi zisiwekeze, nina uhakika wawekezaji watakuwa wengi na tutapanua wigo wa mapato na tutapata mapato ya kutosha kupitia sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi naunga mkono hoja. (Makofi)