Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

Hon. Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kukushukuru wewe pamoja na Bunge lako Tukufu, vilevile nitumie nafasi hii kupongeza sana kazi nzuri ambayo imefanywa na Kamati hizi mbili ambazo hoja zipo Mezani hapa; Kamati ya Utawala, Sheria na Katiba, lakini vilevile Kamati ambayo mimi ni Mjumbe kwa nafasi yangu, Kamati ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Niwapongeze Wenyeviti wa Kamati hizi, Dkt. Mhagama pamoja na Mheshimiwa Londo na Wajumbe wa Kamati zote hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu leo utajikita katika sehemu mbili; sehemu ya kwanza ni miundombinu ya barabara ambayo inasimamiwa na Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) ambao Waheshimiwa Wabunge wengi pia nao walijikita sana katika michango yao kwenye kuchangia suala zima la barabara zetu za mijini na vijijini hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikiri changamoto zipo, changamoto hizo zimetokana na athari kubwa iliyoletwa na mvua za Elnino, mvua ambazo zilitabiriwa kuja nchini kwetu na zimekuja kwa kasi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme kwamba athari tunayoiona leo ni ndogo kulingana na ambavyo ingekuwa endapo TARURA ingekuwa haijafanya kazi yake vizuri katika miaka ya nyuma toka uanzishwaji wake, ni athari ndogo kuliko ambavyo ingekuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hapa TARURA ilipoanzishwa mwaka 2017 barabara za lami zilizokuwa chini ya mtandao wao zilikuwa ni kilometa 1,449 hivi sasa tunavyozungumza mwaka huu 2024 mtandao wa lami ni kilometa 3,224 ina maana zimeongezeka, lakini changarawe kutoka kilometa 24,405 hadi kilometa 41,107 lakini vilevile barabara ambazo ni za udongo kutoka kilometa 83,091 kwenda kilometa 100,098.13. Utaona hapa jitihada kubwa ambayo imefanyika na Serikali katika kuhakikisha barabara zetu za mijini na vijijini zinapitika vizuri na kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije katika suala ambalo limezungumziwa sana hapa. Suala zima kuhuzu upatikanaji wa fedha; ni kweli, wakati wa kuwasilisha taarifa katika Kamati ya Utekelezaji wa Bajeti ya nusu mwaka fedha ambayo ilikuwa imefika ilikuwa ni bilioni 82 katika taarifa ile iliyowasilishwa kwenye Kamati ya TAMISEMI. Lakini hadi hivi ninavyozungumza sasa jumla ya fedha ambayo TARURA imepokea kutoka wenzetu wa Wizara ya Fedha ni bilioni 309. Ni kuonesha ni namna gani ambavyo jitihada inafanyika kuhakikisha barabara zetu zinapitika na zinatengenezwa, hasa kipindi hiki ambacho nyingi zimepata madhara kutokana na mvua ambazo zinanyesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sawa na asilimia 43 ya bajeti ambayo imetengwa kwa ajili ya TARURA, na tayari jitihada zinaendelea, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa na Waziri wa Fedha Mheshimiwa Mwigulu Mchemba tayari wamekaa vikao mbalimbali vya kukubaliana ni namna gani tunazidi kupokea fedha na kuwapelekea wenzetu wa TARURA, ili barabara zetu ziweze kutengenezwa na kupitika kwa wakati.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ya dharura ambayo ilitengwa kwenye bajeti ilikuwa bilioni 21.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Salome Makamba.

TAARIFA

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachojaribu kukisema Mheshimiwa Waziri, anataka kuonesha kwamba, Wabunge au Wajumbe wa Kamati ni waongo au yeye ni muongo, kwa sababu Taarifa ambazo kamati inazo na mimi ni Mjumbe, mpaka tunaingia kwenye Bunge hili, pesa zilizopelekwa ni bilioni 89 tu na zile fedha za dharura. Hiyo bilioni mia tatu na ngapi ni taarifa ambayo anaisema hapa ambayo hakuna Mbunge yeyote katika Bunge hili anaweza kuthibitisha jambo hilo. Yaani anaijua yeye na most of the time kama pesa imeingia leo kuna hatihati ikawa ni exchequer hiyo, sio hela ambayo…

MWENYEKTI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi naomba tu yaani anachokisema hakuna anayeweza kukithibitisha, yaani ni fallacy, anatuletea hadithi ambayo sisi hatuwezi kukubaliana nayo.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Salome. Mheshimiwa Naibu Waziri Taarifa unaipokea?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa hiyo siipokei kwa sababu nilishasema kwamba Taarifa tuliyowasilisha kwenye Kamati ya nusu mwaka ya utekelezaji wa bajeti, Mheshimiwa Makamba amezungumza, ni sahihi ilikuwa ni bilioni 89, lakini nikikwambia kwamba, exchequer ikitolewa na Hazina wenzetu ni sawasawa na fedha ambayo imelipwa kwetu sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naendelea kukupa taarifa ya kwamba, ukiachilia exchequer ambayo ni bilioni 309 fedha iliyolipwa ni bilioni 262 hadi siku hii ya leo ambayo ni asilimia 85 ya fedha yote ambayo ilikuwa imetolewa exchequer, na bado tunavyozungumza Serikali ipo kazini ni kwamba, fedha hiyo inaendelea kulipwa. Ndio maana nasema taarifa ninazozitoa ni mpaka hivi sasa katika uchangiaji wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ambayo ilikuwa imetengwa kwa ajili ya dharura nchi nzima, ilikuwa bilioni 21, na mpaka sasa fedha yote hiyo imepokelewa, lakini baada ya tathmini kwa kumalizia, baada ya tathmini kufanyika iligundulika inahitajika bilioni 65 kwa ajili ya dharura ya hizi mvua ambazo zimeendelea sasa. Hivi sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Wizara ya Fedha na Mipango wanakaa katika kuona ni namna gani tunapata hiyo deficit ya bilioni 44 katika kipindi hiki kwa ajili ya kutengeneza barabara ambazo zimeathirika sana. Ahsante sana.