Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja iliyo mezani kwetu. Kwanza, niwapongeze Waheshimiwa Mawaziri wote wawili, Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo na Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwa kuja na hotuba nzuri ambazo zimetupa mwelekeo wa kule tuendako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeza Mheshimiwa Rais kwa miongozo ambayo ameitoa kwa Wizara hizi na kuepelekea kuletwa kwa hotuba hiyo ambayo tunajadili sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita katika maeneo mawili. Nianze na Sekta ya Gesi Asilia. Naipongeza Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri ambayo inaifanya, lakini nina ushauri katika mambo matatu. Kwanza ni kuhusu mradi wa LNG, nimesoma kwenye mapendekezo ya mpango, kuna mikataba imeshaanza kusainiwa. Ni jambo zuri lakini wamekwenda mbali, kwamba kuna kampuni ya TPDC Likong’o LNG Company Limited imeanzishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba, shughuli hizi za LNG zifanyike kwenye eneo husika. Likong’o ni mtaa au ni kijiji katika Manispaa ya Lindi. Siyo busara sasa shughuli hizi zikaendelea kufanyika Dar es Salaam na Arusha, wakati eneo la mradi lipo. Kwa hiyo, naomba sasa Shughuli za LNG zihamie katika eneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la pili ni kuhusu Ujenzi wa Vituo vya CNG. Wote ni mashahidi sasa bei za mafuta duniani hazitabiriki. Sasa hivi kuna mpango mkubwa au kuna uhamasishaji wa watu tutumie gesi asilia katika vyombo vya usafiri lakini vituo hivi ni vichache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali sasa, kwanza naipongeza TPDC kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kwenye suala hili na EWURA. Sasa naomba Serikali itoe vivutio maalum kwa watu ambao wanataka kujenga vituo hivi ili viongezeke. Kwa sababu kwa sasa nafikiri tunavyo vinne tu. Kuna makampuni zaidi ya 30 wameomba, tuwe na special incentive ili hata kutoka Dar es Salaam kuja Dodoma kuwe na vituo vya CNG, kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza kuwe na Vituo vya CNG na maeneo mengine. Tutoe punguzo maalum, tutoe vivutio ili sasa wawekezaji wajikite katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la tatu ni usambazaji wa gesi viwandani na majumbani. Naipongeza TPDC kwa kazi ambayo wanaifanya vizuri, lakini TPDC hawapewi fungu la kutosha. Naomba mpango ujielekeze kwamba utatoa fedha za kutosha ili usambazaji huu sasa uende kwenye mikoa yote. Isiwe Mtwara, Lindi na Dar es Salaam tu, gesi asilia sasa iende kwenye mikoa yote. Niipongeze Wizara ya Nishati, imesaini mkataba jana wa kupeleka hii gesi kwenda Uganda, sasa ielekee Uganda lakini na mikoa ambayo bomba hili litapita inufaike na mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni kuhusu suala la elimu. Naipongeza Serikali kwamba imeidhinisha matumizi ya Sera Mpya ya Elimu ya 2014. Sera hii ya elimu ya 2014, kama mtakumbuka ilizinduliwa huko nyuma na imekaa miaka nane kabla ya utekelezaji wake kwa sababu ya kukosa funding. Naomba sasa Serikali ijielekeze katika ugharamiaji wa hii sera mpya ya elimu ambayo inakuja na mambo mengi sana ambayo yatabadilisha uendeshaji na usimamizi wa elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzia mwakani tunaanza kutekeleza mtaala mpya kwa wanafunzi wa darasa la tatu. Kwa maana hiyo, Mtihani wa Darasa Saba mwaka 2027 hautakuwepo. Kutakuwa na kitu kinaitwa National Assessment, lakini kwa sasa hivi kwa takwimu zilizopo kila inapofanika mtihani, wanafunzi takribani asilimia 25 hawaendelei na kidato cha kwanza. Tutakapofanya National Assessment ina maana wanafunzi wote wataingia kidato cha kwanza kwa hiyo, kuna mahitaji mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuchukulie mfano wa watahiniwa mwaka huu, tulikuwa na watahiniwa 1,397,370. Sasa asilimia 25 ambao kwa matokeo ya kawaida ya mtihani ni kama watoto 350,000 hivi hawataingia kidato cha kwanza. Tutakapoanza utekelezaji wa sera mpya, hawa 350,000 wataingia kidato cha kwanza. Tutahitaji madarasa mapya, walimu wapya na tutahitaji matundu ya vyoo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa wanafunzi hao 350,000 tunahitaji madarasa ya ziada 8,733, siyo mapya, ni ya ziada ukiacha haya yaliyopo sasa hivi. Tutahitaji matundu ya vyoo 17,497. Kwa hiyo, lazima mpango wetu ujikite katika education financing, tutapata wapi fedha za kugharamia huu mfumo mpya wa elimu, elimu isigharamiwe kama kawaida. Tukifanya kama tunavyotenga bajeti ya kawaida hatutaweza kujenga shule mpya za ufundi ambazo zinatakiwa. Kwa sababu kwa maelekezo ya mtaala wetu mpya, tutakuwa na mikondo miwili; ule mkondo wa kawaida wa taaluma na mkondo wa amali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkondo wa taaluma na mkondo amali ina maana kwamba sasa huku kwenye amali ni kitu kipya. Tutahitaji walimu wapya wa michezo, wa ufundi na walimu wapya wa sanaa. Hao walimu wanahitaji ajira, yaani itatakiwa ajira mpya ili waingie katika mfumo huu. Sasa pasipokuwa na fedha za kutosha hatutaweza kutekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wanahitaji maabara ambazo zimesheheni, siyo maabara ambazo kuna Bunsen burner na test tube. Inabidi tuwe na maabara ambazo mwanafunzi akiingia ajue kweli ameingia maabara. Kwa hiyo, hilo linahitaji uwekezaji, siyo hivyo tu, tunahitaji in service training kwa walimu. Hao Walimu sasa tunawaambia kwamba mtoto akiingia darasa la kwanza anafika form four. Hao waliopo kazini lazima tuwe na mafunzo kazini, tuwawezeshe kwenye mbinu mpya, tuwape maarifa mapya na tuwape ujuzi mpya. Tukigharamia kama tunavyofanya sasa hivi hatutaweza kutekeleza mtaala huo mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)