Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia mpango wetu wa Taifa kwa maendeleo pamoja na Mwongozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi ya kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa nafasi hii ya leo na nichukue nafasi hii ya pili kukushukuru wewe kwa jinsi unavyoendelea kuliongoza Bunge letu, kwa namna ya pekee nitakuwa mwizi wa fadhila katika kipindi hiki ambapo dunia inakabiliwa na misukosuko mikubwa ya kiuchumi inayotokana na athari za janga la UVIKO-19 na yanayotokana na vita vya Mataifa makubwa kama Urusi na Ukraine, lakini nchi yetu imeendelea na uchumi wake umeendelea kuwa stahimilivu chini ya Uongozi wa Jemedari Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambae amekuwa ni tulizo na Faraja kwa Watanzania kutokana na mipango mizuri ya kiuchumi anayoiweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo pia nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa jinsi anavyomsaidia Mheshimiwa Rais katika suala zima, siyo tu la kuweka mipango, lakini kukusanya kodi ambayo leo tunaona fahari, hata leo tutakapotoka kuhitimisha kikao hiki, tutakwenda kupokea magari ambayo ni matokeo ya kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitamshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu na Naibu Waziri Mkuu kwa kazi nzuri waliyoifanya baada ya kupokea kilio changu cha wananchi wa Kata ya Kitwai katika Wilaya ya Simanjiro ambapo walinielekeza kukutana na Mawaziri wa Wizara ya Ardhi, Wizara ya Maliasili, Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Maji pamoja na uratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango uliowekwa na Mawaziri hawa kutekeleza maelekezo ya Waziri Mkuu na Naibu Waziri Mkuu, hivi sasa ni faraja kwa wananchi wa Kitwai na nitakwenda Simanjiro kifua mbele nikijua kabisa tunakwenda kuweka mpango shirikishi utakaotekeleza malengo na maombi ya Serikali katika eneo lile na utakaojali maslahi na mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yetu ya Kitwai B.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni rai yangu pia kwamba siwezi kukaa tena, baada ya kazi nzuri iliyofanyika hivi karibuni ya kusainiwa kwa mikataba ya zaidi ya kilometa 2,000 za EPC+ Finance, kazi ambayo ni mfumo mpya uliobuniwa chini ya Waziri wa wakati huo Mheshimiwa Prof. Mbarawa akisaidiwa na Mtendaji Mkuu wa TANROADs na Kitengo cha EPC+ Finance, Eng. Kitahinda na baadaye maeneo yetu ya Mkoa wa Manyara ikiwemo Wilaya ya Simanjiro, Wilaya ya Arusha kwa Mkoa wa Arusha, Wilaya ya Kiteto na baadhi ya maeneo mengine ikiwemo Kongwa kwa Mheshimiwa Ndugai ambapo tutapata barabara ya kilometa 453.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpongeze sana Waziri wa Miundombinu wa wakati huo pamoja na Waziri wa Fedha ambao wamefanya kazi hiyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niazime maneno machache ya Prof. Kitila Alexander Mkumbo aliyoyatumia katika ukurasa wa tisa aliyokuwa anazungumza akisema hivi: “Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia usuli huo, ninapendekeza kuwa shabaha kuu ya Mpango wa Taifa wa Maendeleo Mwaka 2024/2025 na miaka ijayo, iwe ni kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi ambao ni jumuishi na unaopunguza umaskini, unaozalisha ajira kwa wingi, unaotengeneza utajiri na unaochochea mauzo ya bidhaa zilizoongezwa thamani nje ya nchi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kabisa kama tukijipanga vizuri katika kuendeleza kujenga uchumi wetu kwa namna jumuishi na kushughulisha na umaskini wa watu wetu kwa kuhakikisha kwamba tunaongeza thamani ya mazao yanayotokana na ufugaji, thamani ya mazao yanayotokana na kilimo, thamani ya mazao yanayotokana na uvuvi, thamani ya mazao yanayotokana na misitu na madini, nina hakika uchumi wetu unaomgusa mwananchi wa kawaida utaweza kukua na kila mmoja ataona faida yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa mantiki hiyo, rai yangu ni kwamba, ni vizuri tukawa na maendeleo jumuishi kwa nchi nzima. Tunapofikiria juu ya maendeleo ya nchi ni lazima tuangalie na baadhi ya jamii nyingine ambazo historia na jiografia imewaweka mahali pabaya na hasa ukizingatia kwamba kesho kutwa kwa maana ya mapema mwakani au katikati ya mwaka tutakaa na kupitisha bajeti ya 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunajua, mara nyingi tunapopitisha bajeti, tunazungumza habari ya asilimia 65 ya ajira za watumishi ambayo inalipa mishahara ya watumishi, uendeshaji wa Serikali na asilimia 35 ya maendeleo. Nataka niseme wazi jambo hili lieleweke vizuri, kwamba zipo jamii katika nchi hii ambao hawako katika mfumo wa ajira rasmi za Serikali kutokana na historia, kuchelewa kupata elimu, lakini wote leo wamesoma na hawamo kwenye mfumo wa ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapendekeza, Serikali ije na mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba hakuna jamii inayobaki nje ya uzio wa ajira rasmi ya umma ili kuhakikisha kwamba nchi nzima tunaitendea haki. Kutokufanya hivyo, jamii nyingine unaziacha zikiwa nje kabisa, hawapo kwenye utumishi wa umma na hili sio jambo zuri katika umoja na mshikamano wa Taifa letu kama ambavyo sote tunajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni rai yangu kwamba tunapofikiria jiografia katika maeneo mengine kama ya kwetu ambapo umbali kati ya kijiji na kijiji ni kati ya kilometa 40 mpaka 70 na shule za kata tunazo, hakuna mwanafunzi anayeweza kutembea kilometa 50 kwenda huko, ni lazima shule zile zote zingekuwa ni za hostel.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni Serikali ilikuwa imetenga fedha kwa ajili ya kusaidia shule hizo za bweni za msingi na sekondari, lakini sasa hivi imepunguza fedha hizo. Nataka niwaambie kwa kupunguza fedha hizo kwa upande wa Wizara ya TAMISEMI, mnatuingiza katika hali mbaya zaidi ya maendeleo ya watoto wetu katika shule hizo za sekondari na msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado naiomba Serikali yangu sikivu na hasa Waziri wa Fedha na Waziri wa TAMISEMI, mwone uwezekano wa kukamilisha mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuliahidiwa mabwawa yapatayo manne katika Wilaya ya Simanjiro lakini mabwawa mawili ambayo ni Kopokyoo na Anaryoo katika Kata ya Comoro na Kijiji cha Naruchugin na hiyo ya Kopokyoo iko katika Kijiji cha Lerumo Kata ya Ruremit. Tuliahidiwa kwamba mabwawa haya yangeweza kujengwa, lakini sasa ni mwaka wa tatu fedha hazitoki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningefurahi sana kama Wizara ya Mheshimiwa Mwigulu Nchemba itashirikiana na Wizara ya Mifugo ili fedha zile za mabwawa hayo mawili yaweze kutoka hata kabla ya yale mengine mawili ambayo hayajaweza kuwekwa kwenye bajeti ya miaka iliyopita. Ni ombi langu kwa Waziri mwenye dhamana ili hali hiyo iweze kushughulikiwa na mifugo yetu iweze kupata maji ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapofikiria maisha ya wafugaji kutoka ufugaji uliozoeleka kwenda katika ufugaji wa kisasa wenye nyama nyingi na maziwa mengi, pia tunazungumzia haja ya kuweka miundombinu rafiki kwa maana ya kupata maji, kwa maana ya kupata majosho, pia kwa maana ya kupata mbegu bora za Sahiwal, Friesian, Jersey, Ayrshire na Simmentals ambazo zitasaidia wafugaji hawa kufanya mapinduzi ya kuwa na ng’ombe wa kisasa wenye tija kubwa zaidi lakini miundombinu lazima irekebishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu katika eneo hilo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Mhandisi Stella Martin Manyanya, atafuatiwa na Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima na watoa hoja wajiandae.

Mheshimiwa Ole-Sendeka, umeshazima kisemeo?

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshazima muda mrefu sana, mtafuteni aliyejisahau.